Luka 16 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mufano wa mulinzi wa mali 1 Yesu akawaambia wanafunzi wake mufano huu: “Kulikuwa mutu mumoja tajiri aliyekuwa na mulinzi wa mali yake. Yule mulinzi akachongewa kwa bwana wake kwamba anaponda mali yake. 2 Halafu bwana wake akamwita na kumwambia: ‘Ni habari gani ile waliyonielezea juu yako? Ninakuomba unifanyie hesabu yote ya mali yangu, kwa sababu hauwezi tena kuwa mulinzi wa mali yangu.’ 3 Yule mulinzi akajiuliza: ‘Sasa nitafanya nini? Bwana wangu ananifukuza kwa kazi. Kulima, mimi siwezi; na kuombaomba, ninasikia haya. 4 Sasa ninajua jinsi nitakavyofanya kusudi wakati nitafukuzwa kwa kazi yangu ya ulinzi, watu wapate kunikaribisha katika nyumba zao.’ 5 Halafu akamwita kila mutu aliyekuwa na deni ya bwana wake. Akamwuliza kwanza: ‘Deni ya bwana wangu unayokuwa nayo ni yapata gani?’ 6 Naye akamujibu: ‘Madebe mia moja ya mafuta ya muzeituni.’ Yule mulinzi wa mali akamwambia: ‘Kamata barua yako ya mapatano ya deni, ikaa upesi na uandike makumi tano.’ 7 Kisha akamwuliza mwingine: ‘Na wewe uko na deni yapata gani?’ Naye akajibu: ‘Saki mia moja za ngano.’ Yule mulinzi akamwambia: ‘Kamata barua yako ya mapatano na uandike saki makumi nane.’ 8 Basi bwana wa yule mulinzi akamusifu kwa sababu alitenda kwa werevu. Kwa maana watu wa dunia hii wanatengeneza maneno yao na wenzao kwa werevu sana kuliko watu wanaopenda kuishi katika mwangaza.” 9 Yesu akaongeza kusema: “Nami ninawaambia: mutumie mali ya dunia hii kwa kuunga urafiki, kusudi wakati mali ile itakapokosekana, mupate kupokelewa kwenye makao ya milele. 10 Yule anayekuwa mwaminifu katika vitu vichache, yuko mwaminifu vilevile katika vitu vingi. Na yule asiyekuwa mwaminifu katika vitu vichache, hayuko mwaminifu vilevile katika vitu vingi. 11 Basi kama ninyi hamukukuwa waaminifu kwa kulinda mali ya dunia hii, ni nani atakayeweza kuwatumainia kwa kulinda mali ya kweli? 12 Na kama hamuwezi kulinda mali ya mutu mwingine kwa uaminifu, ni nani atakayewapa mali yenu ya pekee? 13 “Hakuna mutumishi anayeweza kutumikia wabwana wawili. Kwa maana atamuchukia mumoja na kumupenda mwingine; au atashikamana na mumoja na kumuzarau mwingine. Hamuwezi kumutumikia Mungu na kutumikia mali vilevile.” Mafundisho mbalimbali ya Yesu ( Mat 11.12-13 ; 5.31-32 ; Mk 10.11-12 ) 14 Wakati Wafarisayo waliposikia maneno haya yote wakamuzarau Yesu, kwa sababu walikuwa wapenda feza. 15 Yesu akawaambia: “Ninyi ni watu wanaojionyesha kuwa wenye haki mbele ya watu, lakini Mungu anajua yanayokuwa ndani ya mioyo yenu. Kwa maana mambo yanayosifiwa na watu ni machukizo mbele ya Mungu. 16 “Sheria ya Musa na maandiko ya manabii yalitangazwa mpaka kuja kwa Yoane. Tangu wakati ule, Habari Njema ya Ufalme wa Mungu inahubiriwa, na kila mutu anajiingiza kwa kinguvu ndani ya ufalme ule. 17 Lakini ni vyepesi zaidi kwa mbingu na dunia kutoweka kuliko hata nukta moja ya Sheria kuondoshwa. 18 “Kila mutu anayemufukuza muke wake na kuoa mwingine, anazini; na mutu anayemwoa yule muke aliyefukuzwa anazini vilevile. Mufano wa tajiri na Lazaro 19 “Kulikuwa mutu mumoja tajiri aliyezoea kuvaa nguo zenye kuwa laini sana za bei kali zaidi na aliyeishi katika raha siku zote. 20 Vilevile kulikuwa masikini mumoja aliyeitwa Lazaro aliyekuwa na vidonda mwili wote, alibaki akilala mbele ya mulango wa nyumba ya yule tajiri. 21 Yeye alikuwa akitamani kula makombo yaliyoanguka toka juu ya meza ya yule tajiri. Hata imbwa walikuja kulambulalambula vile vidonda vyake. 22 Siku moja yule masikini akakufa, na wamalaika wakamupeleka mpaka pembeni ya Abrahamu. Na yule tajiri akakufa vilevile na kuzikwa. 23 Alipokuwa katika jehenamu akiteswa sana, akainua macho, akamwona Abrahamu kwa mbali na Lazaro akiwa pembeni yake. 24 Basi akalalamika, akisema: ‘Baba Abrahamu, unisikilie huruma; umutume Lazaro achovye incha ya kidole chake katika maji, anipoleshe ulimi wangu, kwa sababu ninateswa sana katika moto huu.’ 25 Lakini Abrahamu akamujibu: ‘Mutoto wangu, kumbuka kwamba umekwisha kupewa mema yaliyokupasa wakati ulipoishi katika dunia, na Lazaro alipata taabu. Na sasa yeye anatulizwa, lakini wewe unateswa. 26 Na zaidi ya hii kuna shimo kubwa sana kati yetu na ninyi. Hivi wale wanaokuwa huku wakitaka kufika kule kwenu hawawezi, wala wale wanaokuwa kule hawawezi kuvuka kwa kufika huku kwetu.’ 27 Halafu tajiri akasema: ‘Basi, baba ninakuomba umutume Lazaro kwa nyumba ya baba yangu, 28 kwa maana niko na wandugu watano. Aende kuwaonya, kusudi nao vilevile wasikuje katika nafasi hii ya mateso.’ 29 Abrahamu akajibu: ‘Wandugu zako wako na maandiko ya Musa na ya manabii, wayasikilize!’ 30 Naye tajiri akasema tena: ‘Ee Abrahamu, ile haitoshi. Lakini kama mutu mumoja akifufuka na kuwaendea, watageuka toka katika zambi zao.’ 31 Lakini Abrahamu akamwambia: ‘Kama wandugu zako hawasikilizi maonyo ya Musa na ya manabii, hawatasadiki hata mutu aliyefufuka.’ ” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo