Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Luka 12 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Maonyo juu ya unafiki
( Mat 10.26-27 )

1 Wakati ule ule makundi mengi ya maelfu ya watu walikusanyika hata wakakanyaganakanyagana. Yesu akaanza kwanza kusema na wanafunzi wake, akiwaambia: “Mufanye angalisho na chachu ya Wafarisayo, maana yake unafiki wao.

2 Hakuna kitu chochote kinachofichwa kitakachokosa kuvumbulikana wala hakuna siri itakayokosa kujulikana.

3 Ni hivi maneno yote mutakayosema katika giza yatasikilika muchana kati. Vilevile maneno yote mutakayosema kwa siri ndani ya chumba chenye kufichama, yatatangazwa juu ya paa la nyumba.


Yule anayepaswa kuogopwa
( Mat 10.28-31 )

4 “Ninawaambia ninyi warafiki zangu: musiwaogope wale wanaoua mwili tu lakini hawawezi kufanya kitu kingine zaidi.

5 Nitawaonyesha yule munayepaswa kumwogopa; mumwogope Mungu, kwa sababu kisha kuuawa ni yeye anayekuwa na uwezo wa kumutupa mutu katika jehenamu. Hakika ninawaambia, ni huyo munayepaswa kumwogopa!

6 “Ndege watano wadogo, si wanauzishwa kwa bei chini kabisa? Hata vile Mungu hasahau hata mumoja wao.

7 Lakini hata nywele za vichwa vyenu zimehesabiwa zote. Basi musiogope kwa sababu ninyi ni bora zaidi kuliko ndege wengi!


Kumwitikia na kumukana Kristo
( Mat 10.32-33 ; 12.32 ; 10.19-20 )

8 “Nami ninawaambia: kila mutu anayenikubali mbele ya watu, Mwana wa Mutu atamukubali vilevile mbele ya wamalaika wa Mungu.

9 Lakini mutu yeyote anayenikana mbele ya watu, yule atakanwa mbele ya wamalaika wa Mungu.

10 “Na kila mutu anayesema vibaya juu ya Mwana wa Mutu atasamehewa, lakini kila mutu anayemutukana Roho Mutakatifu, hatasamehewa.

11 “Wakati watakapowapeleka kwa kuhukumiwa katika nyumba za kuabudia, au mbele ya watawala na ya wakubwa, musijihangaishe juu ya maneno mutakayojibu au yale mutakayosema,

12 kwa sababu Roho Mutakatifu atawafundisha saa ile ile maneno munayopaswa kusema.”


Mufano wa tajiri mupumbafu

13 Mutu mumoja katika kundi akamwambia Yesu: “Mwalimu, umwambie ndugu yangu anipe sehemu yangu ya urizi, baba aliotuachia.”

14 Yesu akamujibu: “Ewe bwana, ni nani aliyeniweka kuwa mwamuzi wenu au mutu wa kuwagawanyia mali zenu?”

15 Kisha Yesu akawaambia watu wote: “Muangalie, mujilinde na tamaa yote ya mali, kwa sababu mali haiwezi kukinga uzima wa mutu, hata akiwa tajiri sana.”

16 Halafu akawaambia mufano huu: “Kulikuwa tajiri mumoja aliyekuwa na shamba lenye kutoa mavuno mengi.

17 Yeye akawaza na kusema: ‘Nitafanya nini hivi ninakosewa nafasi ya kuwekea mavuno yangu yote?’

18 Kisha akajisemesha: ‘Nitafanya hivi: nitabomoa gala zangu na nitajenga zingine kubwa zaidi, na mule nitaweka mavuno yangu yote na mali zangu zingine.’

19 Kisha nitajisemesha hivi juu yangu mwenyewe: ‘Uko na mali nyingi ulizoweka akiba kwa miaka mingi. Sasa utulizane, ukule na kunywa na kujifurahisha.’

20 Lakini Mungu akamwambia: ‘Mupumbafu wewe! Leo leo usiku utakufa. Na sasa, vitu hivi vyote ulivyojitayarishia vitakuwa vya nani?’ ”

21 Yesu akaongeza kusema: “Ni hivi inavyokuwa kwa yule anayejiwekea mali mengi, lakini mbele ya Mungu hahesabiwi kuwa na kitu.”


Kumutumainia Mungu
( Mat 6.25-34 )

22 Kisha Yesu akawaambia wanafunzi wake: “Ni kwa sababu hii ninawaambia: musijisumbue kwa ajili ya maisha yenu, kwamba mutakula nini; wala musijisumbue kwa ajili ya miili yenu, kwamba mutavaa nini.

23 Uzima unapita chakula, nao mwili ni wa lazima kuliko nguo.

24 Mufikiri juu ya kibombobombo: ndege hao hawapandi mbegu, hawavuni, hawana gala wala nafasi yoyote ya kuwekea mavuno, lakini Mungu anawalisha. Ninyi ni wa lazima zaidi kuliko ndege!

25 Nani kati yenu, kwa ajili ya kujisumbua kwake, anaweza kujiongezea hata siku moja kupita muda wa maisha yake?

26 Basi ikiwa hamuwezi kufanya kitu kidogo kama hiki, kwa nini munajisumbua juu ya vitu vingine?

27 Mufikiri juu ya namna maua yanavyoota. Hayasumbuki wala kujisukia nguo. Lakini ninawaambia kwamba hata mufalme Solomono katika utukufu wote aliokuwa nao, hakuvaa nguo inayoweza kulinganishwa na uzuri wa moja la maua.

28 Basi ikiwa Mungu anavalisha majani kama hivi, yanayoonekana pale leo na kesho yanatoweka na kutupwa, hatawavalisha vizuri zaidi ninyi wenye imani ndogo?

29 Basi musijisumbue kwa kutafuta chakula au kinywaji.

30 Ni wapagani ndio wanaotafutatafuta vitu hivyo vyote. Baba yenu anajua kwamba munahitaji vitu hivyo.

31 Hivi ninyi mutafute Ufalme wake, naye atawaongezea vitu hivi vyote.


Kujiwekea akiba katika mbingu
( Mat 6.19-21 )

32 “Musiogope ninyi kundi dogo! Kwa kuwa Baba yenu amependelea kuwapa ninyi ule Ufalme wake.

33 Muuzishe vitu munavyokuwa navyo, muwasaidie wamasikini. Mujiwekee feza zisizoweza kuwa na upungufu, nayo akiba isiyoweza kumalizika katika mbingu. Kule wizi hawawezi kukaribia wala nondo hawaharibu.

34 Kwa maana pahali akiba yenu inapokuwa, ni pale roho zenu zinapokuwa vilevile.


Watumishi waangalifu

35 “Mukuwe tayari kwa kutumika na kuacha taa zenu zikiwaka.

36 Mukuwe kama watumishi wanaomungojea bwana wao arudie kutoka katika karamu ya ndoa, kusudi wakati anapofika na kupiga hodi wamufungulie mulango mara moja.

37 Heri watumishi wale bwana wao atakaowakuta wakikesha wakati anapofika! Kweli ninawaambia: atafunga mukaba wake vizuri na kuwakaribisha kula chakula, na kubakia pale akiwashugulikia.

38 Heri watumishi wale atakaowakuta wakikesha hata akifika katikati ya usiku au nyuma ya saa ile.

39 Munajua vema kwamba mwenye nyumba angejua saa gani mwizi atakapokuja kumwiba, asingeacha nyumba yake ibomolewe.

40 Kwa hiyo ninyi vilevile mukuwe tayari, kwa sababu Mwana wa Mutu atarudia saa musiyozania.”


Mutumishi mwaminifu na asiyekuwa mwaminifu
( Mat 24.45-51 )

41 Halafu Petro akamwuliza Yesu: “Bwana, mufano huu unatuelekea sisi wenyewe au unawaelekea watu wote?”

42 Bwana akajibu: “Ni nani basi anayekuwa musimamizi mwaminifu na mwenye akili? Ni yule bwana wake aliyemuweka kwa kuwasimamia watumishi wake wengine na kumwamuru kuwapatia posho lao kwa wakati uliopangwa.

43 Heri mutumishi yule, ikiwa saa bwana wake anaporudia, anamukuta akifanya kazi ile.

44 Kweli ninawaambia: bwana wake atamuweka mutumishi yule kuwa musimamizi wa mali yake yote.

45 Lakini kama mutumishi yule akijisemesha mwenyewe kwamba bwana wake anakawia kurudia; na halafu anaanza kuwapiga watumishi wenzake, wanaume na wanawake, naye anakula na kunywa na kulewa.

46 Basi bwana wa mutumishi yule atakuja siku asiyozania, na saa asiyoijua. Naye atamupiga vikali na kumwazibu sawa na watu wasiokuwa waaminifu.

47 “Mutumishi anayejua mapenzi ya bwana wake, lakini anakosa kujiweka tayari na kutofanya sawa na mapenzi ya bwana yule, atapigwa fimbo nyingi.

48 Lakini kwa ngambo ingine, yule asiyejua mapenzi ya bwana yake, na anayefanya mambo yanayostahili azabu, atapigwa fimbo chache. Kwa maana kila mutu aliyepewa vingi, ataombwa kutoa vingi zaidi; na aliyepewa madaraka mengi, ataulizwa mengi zaidi.


Yesu ni sababu ya matengano
( Mat 10.34-36 )

49 “Nimekuja kuleta moto katika dunia, nami ningetaka sana kuona ukiwa umekwisha kuwaka!

50 Niko na muzigo wa mateso ninaopaswa kubeba, nami ninasongwa sana mpaka mapaswa hayo yatakapotimizwa!

51 Munazania kwamba mimi nimekuja kuleta amani katika dunia? Ninawaambia ninyi: si vile, nimekuja kuleta matengano.

52 Kwa maana tangu sasa watu watano wa jamaa moja watatengana; watatu watapingana na wawili, na wawili watapingana na watatu.

53 Baba atapingana na mwana wake, na mwana atapingana na baba yake. Mama atapingana na binti yake, na binti atapingana na mama yake. Mama mukwe atapingana na muke wa mutoto wake, na muke yule atapingana na mama mukwe yake.”


Vitambulisho vya nyakati
( Mat 16.2-3 )

54 Yesu akawaambia makundi vilevile: “Wakati munapoona mawingu yakitokea upande wa magaribi, mara moja munasema kwamba mvua itanyesha, na ni vile inavyokuwa.

55 Na wakati munapoona upepo ukivuma toka upande wa kusini, munasema kwamba jua litakuwa kali, na ni vile inavyokuwa.

56 Ninyi wanafiki! Munajua kutambua hali ya inchi na ya anga, namna gani munashindwa kutambua nyakati hizi za sasa?


Hasara ya kutogeuka toka katika zambi
( Mat 5.25-26 )

57 “Sababu gani ninyi wenyewe hamuwezi kujiamulia jambo la haki?

58 Unapokwenda kwa tribinali na mupinzani wako, ujikaze upatane naye mungali katika njia. Kama si vile atakupeleka mbele ya mwamuzi, na mwamuzi atakutoa kwa askari, na askari atakutupa katika kifungo.

59 Ninakuambia: hautatoka mule mpaka utakapomaliza kulipa sengi la mwisho.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ