Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kutoka 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Musa anamulilia Yawe

1 Lakini Yawe akamujibu Musa: “Sasa utaona jinsi nitakavyomutendea mufalme wa Misri. Kwa nguvu atalazimishwa kuwaacha watu wangu watoke. Kwa nguvu atawafukuza waondoke katika inchi yake.”


Mungu anamwita Musa

2 Mungu akamwambia Musa: “Mimi ni Yawe.

3 Nilimutokea Abrahamu, Isaka, na Yakobo nikijulikana kama Mungu Mwenye Nguvu, ingawa sikuwajulisha jina langu, Yawe.

4 Tena nilifanya agano nao kwamba nitawapa inchi ya Kanana ambako waliishi kama wageni.

5 Zaidi ya hayo, nimesikia kilio cha Waisraeli ambao wamelazimishwa kufanya kazi za kitumwa na Wamisri, nikalikumbuka agano langu.

6 Kwa hiyo, uwaambie Waisraeli hivi: ‘Mimi ni Yawe! Mimi nitawatoa katika nira mulizowekewa na Wamisri. Nitawaokoa toka utumwa wenu. Nitanyoosha mukono wangu wenye nguvu na kuwaazibu vikali Wamisri na kuwakomboa ninyi.

7 Nitawafanya kuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wenu. Ninyi mutatambua kwamba mimi ni Yawe, Mungu wenu, niliyewatoa katika nira za Wamisri.

8 Nami nitawapeleka katika inchi ile niliyoapa kumupa Abrahamu, Isaka, na Yakobo. Nitawapa inchi hiyo ikuwe yenu. Mimi ni Yawe.’ ”

9 Musa akawaelezea Waisraeli maneno hayo. Lakini wao hawakumusikiliza kwa sababu walikuwa wamekufa moyo kutokana na utumwa mukali.

10 Kisha Yawe akamwambia Musa:

11 “Kwenda kwa mufalme wa Misri, umwambie awaache Waisraeli waondoke katika inchi yake.”

12 Lakini Musa akamwambia Yawe: “Angalia, Waisraeli hawanisikilizi mimi. Namna gani mufalme wa Misri atanisikia! Tena mimi ni mutu asiyekuwa na ujuzi wa kuongea!”

13 Lakini Yawe akaongea na Musa na Haruni, akawaagiza waende kwa mufalme wa Misri, na kuwatoa Waisraeli kutoka inchi ya Misri.


Ukoo wa Musa na Haruni

14 Haya ndiyo majina ya wakubwa wa jamaa za Waisraeli. Wana wa Rubeni, muzaliwa wa kwanza wa Israeli: Hanoki, Palu, Hesironi na Karmi. Hao walikuwa babu za jamaa za Rubeni.

15 Wana wa Simeoni walikuwa: Yemueli, Yamini, Ohadi, Yakini, Sohari na Sauli. Huyu wa mwisho alikuwa mutoto wa mwanamuke wa Kanana. Hao walikuwa babu za jamaa za Simeoni.

16 Sasa haya ni majina ya wana wa Lawi na wazao wao: Gersoni, Kohati na Merari. Lawi aliishi miaka mia moja makumi tatu na saba.

17 Wana wa Gersoni walikuwa: Libuni na Simei. Hao walikuwa babu za jamaa zao.

18 Wana wa Kohati walikuwa: Amuramu, Izihari, Hebroni na Uzieli. Kohati aliishi miaka mia moja makuni tatu na mitatu.

19 Wana wa Merari walikuwa: Mali na Musi. Hao ndio babu za jamaa za Walawi.

20 Amuramu alimwoa Yokebedi, shangazi yake, naye akamuzalia Haruni na Musa. Amuramu aliishi miaka mia moja makumi tatu na saba.

21 Na wana wa Izihari walikuwa: Kora, Nefegi na Zikiri.

22 Wana wa Uzieli walikuwa: Misaeli, Elisafani na Sitri.

23 Haruni alimwoa Eliseba, binti ya Aminadabu, dada ya Nasoni; naye akamuzalia Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari.

24 Nao wana wa Kora walikuwa: Asiri, Elkana na Abiasafu, ambao walikuwa babu za jamaa za Kora.

25 Eleazari mwana wa Haruni, alimwoa mumoja wa wabinti za Putieli, naye akamuzalia Finehasi. Hawa ndio waliokuwa wakubwa wa jamaa za Lawi.

26 Haruni na Musa ndio walioambiwa na Yawe: “Mutoe watu wa Israeli kutoka inchi ya Misri, vikundi kwa vikundi.”

27 Ndio haohao Musa na Haruni walioongea na mufalme wa Misri, juu ya kuwatoa Waisraeli kutoka inchi ya Misri.

28 Siku ile Yawe alipoongea na Musa katika inchi ya Misri,

29 alimwambia: “Mimi ni Yawe. Umwambie mufalme wa Misri maneno yote ninayokuambia.”

30 Lakini Musa akamwambia Yawe: “Mimi sina ujuzi wa kuongea. Mufalme wa Misri atanisikiliza namna gani?”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ