Kutoka 40 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Hema linasimikwa na kutakaswa 1 Yawe akamwambia Musa: 2 Katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza, utasimika hema takatifu la mukutano. 3 Ndani ya hema hilo utaweka lile Sanduku la Agano, kisha weka pazia mbele yake. 4 Utaingiza meza na kupanga vyombo vyake juu. Utaingiza kile kinara vilevile na kuweka taa zake juu yake. 5 Mazabahu ya zahabu ya kufukizia ubani utaiweka mbele ya Sanduku la Agano, kisha utatundika pazia kwenye mulango wa hema takatifu. 6 Ile mazabahu ya kuteketezea sadaka utaiweka mbele ya mulango wa hema takatifu la mukutano. 7 Birika la kunawia utaliweka katikati ya hema la mukutano na mazabahu na kulijaza maji. 8 Utazungusha upango na kutundika pazia kwenye mulango wake. 9 Kisha, utatakasa hema pamoja na vyombo vyake vyote kwa kuvipakaa yale mafuta ya kupakaa, nalo litakuwa takatifu. 10 Halafu, utatakasa mazabahu ya kuteketezea sadaka na vyombo vyake vyote kwa kuipakaa mafuta, nayo itakuwa takatifu kabisa. 11 Birika la kunawia na tako lake vilevile utalitakasa kwa namna hiyohiyo. 12 Utamwita Haruni na wana wake wakuje kwenye mulango wa hema la mukutano, kisha uwanawishe. 13 Utamuvalisha Haruni zile nguo takatifu. Utamupakaa mafuta na kumutakasa, kusudi aweze kunitumikia kama vile kuhani. 14 Utawaita wana wake na kuwavalisha zile kanzu. 15 Kisha uwapakae mafuta kama vile ulivyomupakaa baba yao, kusudi nao vilevile wanitumikie kama makuhani. Kupakwa mafuta huku kutawaingiza katika ukuhani wa kudumu katika vizazi vyao vyote. 16 Basi, Musa alitimiza kwa ukamilifu kabisa maagizo yote ya Yawe. 17 Katika siku ya kwanza ya mwezi wa kwanza mwaka wa pili kisha kutoka Misri, hema takatifu likasimikwa. 18 Musa akaweka vikalio vyake, akainua mbao zake, akashikamanisha miti yake na kusimamisha nguzo zake. 19 Akatandaza pazia juu ya hema takatifu na kuweka kifuniko cha hema juu yake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 20 Kisha akatwaa vile vibao viwili vya mawe na kuviweka katika lile sanduku. Akapitisha ile miti katika vikomo vya sanduku na kuweka kiti cha rehema juu yake. 21 Kisha akaweka lile Sanduku la Agano ndani ya hema na kutundika pazia, na kwa namna hiyo akafunika Sanduku la Agano, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 22 Akaweka meza ndani ya hema la mukutano, upande wa kaskazini, sehemu ya inje ya pazia, 23 na juu yake akapanga mikate iliyotolewa kwa Yawe, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 24 Akaweka kinara ndani ya hema la mukutano, upande wa kusini, kuelekea meza. 25 Mule, mbele ya Yawe, akawasha taa zake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 26 Akaweka ile mazabahu ya zahabu katika hema, mbele ya pazia, 27 na kufukiza ubani wenye harufu nzuri juu yake, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 28 Akatundika pazia kwenye mulango wa hema takatifu, 29 akaweka pale kwenye mulango wa hema takatifu mazabahu ya sadaka za kuteketezwa, akatolea juu yake sadaka ya kuteketezwa kwa moto na sadaka ya ngano, kama vile alivyoamuriwa na Yawe. 30 Akaweka birika la kunawia katikati ya hema la mukutano na mazabahu, na kutia maji ya kunawa. 31 Musa, Haruni na wana wake, wote wakanawa mikono na miguu yao mule. 32 Kila mara walipoingia ndani ya hema au walipokaribia ile mazabahu, walinawa, kama vile Musa alivyoamuriwa na Yawe. 33 Kwa mwisho Musa akatengeneza upango kuzunguka hema takatifu na mazabahu na kuweka pazia kwenye mulango wa upango. Hivyo, Musa akakamilisha kazi yote. Wingu juu ya hema la mukutano ( Hes 9.15-23 ) 34 Kisha, lile wingu likafunika lile hema la mukutano na utukufu wa Yawe ukajaza hema. 35 Musa akashindwa kuingia ndani ya hema la mukutano kwa sababu hilo wingu lilikaa juu yake na utukufu wa Yawe ukajaa mule. 36 Katika safari zao zote Waisraeli hawakuanza safari hata kidogo isipokuwa wakati wingu hilo lilipoinuliwa kutoka juu ya hema. 37 Kama wingu hilo halikuinuliwa wao hawakuanza safari. Walingoja mpaka wakati lilipoinuliwa. 38 Katika safari zao zote, Waisraeli waliweza kuliona lile wingu la Yawe juu ya hema wakati wa muchana na ule moto ukiwaka juu yake usiku. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo