Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kutoka 35 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kanuni za Sabato

1 Musa akakusanya Waisraeli wote pamoja, akawaambia: Haya ndiyo mambo ambayo Yawe amewaamuru kufanya:

2 Kwa siku sita mutafanya kazi zenu. Lakini siku ya saba ni Sabato, siku ya mapumziko ambayo ni takatifu kwa Yawe. Yeyote atakayefanya kazi siku hiyo lazima auawe.

3 Musiwashe hata moto katika makao yenu siku ya Sabato.


Matoleo kwa ajili ya hema takatifu
( Kut 25.1-9 )

4 Musa akawaambia Waisraeli wote: Hili ndilo jambo ambalo Yawe amewaamuru kufanya:

5 Mutatoa katika mali zenu muchango wa kumupa Yawe. Kila mutu mwenye moyo mwema atamuletea Yawe muchango: sadaka, feza, shaba;

6 sufu ya samawi, ya zambarau na nyekundu; kitani safi iliyosokotwa; manyoya ya mbuzi;

7 ngozi za kondoo dume zilizotiwa rangi nyekundu, ngozi za mbuzi; mbao za mujohoro,

8 mafuta kwa ajili ya taa, viungo kwa ajili ya mafuta ya kupakaa na kwa ajili ya ubani wenye harufu nzuri;

9 mawe vya sardoniki na mawe mengine kwa ajili ya mapambo ya kizibao na kifuko cha kifua.


Vifaa vya hema takatifu
( Kut 39.32-43 )

10 Kila mutu mwenye ujuzi wa kazi fulani kati yenu atakuja kufanya vitu vyote Yawe alivyoamuru:

11 kutengeneza hema takatifu, kifuniko chake na pazia lake, vifungio vyake, miti yake, vikalio vyake;

12 Sanduku la Agano pamoja na miti yake, kiti cha rehema, pazia la Pahali Patakatifu Sana;

13 meza na miti yake pamoja na vyombo vyake vyote, mikate iliyotolewa kwa Yawe;

14 vinara vya taa pamoja na vyombo vyake vyote, taa zake na mafuta yake;

15 mazabahu ya ubani na miti yake, mafuta ya kupakaa na ubani wenye harufu nzuri, pazia la mulango wa hema takatifu;

16 mazabahu ya sadaka za kuteketezwa pamoja na wavu wa shaba, miti yake pamoja na vyombo vyake vyote, birika na tako lake;

17 nguo za kiwanja, nguzo zake na vikalio vyake, pazia la mulango wa kiwanja;

18 misumari ya hema takatifu na ya kiwanja pamoja na kamba zake;

19 nguo zilizofumwa vizuri kabisa kwa ajili ya kazi ya Pahali Patakatifu, ni kusema nguo takatifu ya kuhani Haruni na ya wana wake, kwa ajili ya kazi yao ya ukuhani.


Watu wanaleta matoleo yao

20 Basi, Waisraeli wakaondoka mbele ya Musa.

21 Kila mutu aliyevutwa na kusukumwa ndani ya moyo wake alimutolea Mungu muchango wake kwa ajili ya hema la mukutano, kazi zake zote na nguo yake takatifu.

22 Hivyo wote wenye moyo safi, wanaume na wanawake, wakaleta pete za masikio na za muhuri, vikuku na kila aina ya mapambo ya zahabu. Kila mutu akamutolea Yawe kitu cha zahabu.

23 Kila mutu alileta kitu chochote alichokuwa nacho kama vile sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, au kitani safi, au manyoya ya mbuzi au ngozi ya kondoo iliyotiwa rangi nyekundu.

24 Kila mutu aliyeweza kutoa feza au shaba aliileta kwa Yawe kama matoleo yake. Tena mutu yeyote aliyekuwa na mbao za mujohoro alileta vilevile.

25 Wanawake wote waliokuwa na ujuzi wa kufuma walileta vitu walivyofuma kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu na kitani safi iliyosokotwa.

26 Na wanawake wote waliokuwa na ujuzi walisokota manyoya ya mbuzi.

27 Viongozi walileta mawe ya rangi na mawe mengine kwa ajili ya kizibao na kifuko cha kifua.

28 Walileta vilevile viungo na mafuta kwa ajili ya taa, mafuta ya kupakaa na ubani wenye harufu nzuri.

29 Waisraeli wote, wanaume na wanawake, ambao walivutwa ndani ya moyo wao kuleta kitu chochote kwa ajili ya kazi ambayo Yawe alikuwa amemwagiza Musa ifanyike, walileta vitu hivyo kwa mapenzi yao, kama vile muchango wa kumupa Yawe.


Wafundi kwa ajili ya hema la mukutano
( Kut 31.1-11 )

30 Musa akawaambia Waisraeli: Muangalie! Yawe amemuchagua Bezaleli mwana wa Uri mwana wa Huri, wa kabila la Yuda.

31 Amemujaza Roho wake, amemupa ujuzi, akili, maarifa na ufundi,

32 afanye michoro ya ufundi na kufanya kazi za kufua zahabu, feza na shaba;

33 achonge mawe ya kupamba na mbao kwa ajili ya kazi zingine zote za kifundi.

34 Vilevile amemwongoza yeye na Oholiabu mwana wa Ahisamaki, wa kabila la Dani wawafundishe wengine.

35 Amewapa ujuzi wa kufanya kila kazi ya ufundi au inayofanywa na watu wa akili au wafundi wa kushona kwa sufu ya rangi ya samawi, ya zambarau, nyekundu na kitani safi iliyosokotwa kwa kutumia ufundi wowote wa akili.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ