Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kutoka 32 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Sanamu ya mwana-ngombe wa zahabu
( Kumb 9.6-29 )

1 Watu walipoona kwamba Musa amechelewa kurudi kutoka juu ya mulima, wakakusanyika mbele ya Haruni na kumwambia: Basi! Ututengenezee miungu itakayotuongoza, maana hatujui jambo lililomupata yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri.

2 Haruni akawajibu: Mutwae pete za zahabu za masikio ya wake zenu, wana wenu na wabinti zenu, muniletee.

3 Basi, watu wote wakatoa pete zote za zahabu za masikio yao, wakamuletea Haruni.

4 Naye akazitwaa akaziyeyusha, akatengeneza sanamu ya mwana-ngombe. Watu wakapaaza sauti wakasema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri.

5 Kisha Haruni akamujengea yule mwana-ngombe mazabahu, halafu akatangaza: Kesho kutakuwa sikukuu kwa ajili ya Yawe.

6 Kesho yake watu wakaamuka mapema wakatoa sadaka za kuteketezwa na sadaka za amani. Watu wakaikaa chini kwa kula na kunywa, kisha wakasimama na kucheza.

7 Yawe akamwambia Musa: Teremuka chini kwa maana watu wako uliowaleta kutoka inchi ya Misri wamejipotosha wenyewe.

8 Wameacha mara moja njia niliyowaamuru, wakajifanyia sanamu ya mwana-ngombe, nao wamemwabudu na kumutolea sadaka wakisema: Ee Israeli, huyu ndiye mungu wetu aliyetutoa katika inchi ya Misri!

9 Ninawafahamu watu hawa. Wao wana vichwa vigumu.

10 Sasa, usijaribu kunizuia. Uniache niwaangamize kwa kasirani kali. Kisha kutokana nawe nitaunda taifa kubwa.

11 Lakini Musa akamusihi Yawe, Mungu wake, akisema: Ee Yawe, kwa nini hasira yako inawaka vikali juu ya watu wako uliowatoa katika inchi ya Misri kwa uwezo mukubwa na mukono wenye nguvu?

12 Ukifanya hivyo, hakika Wamisri watasema: Aliwatoa kwa nia mbaya kwa kuwaua kwenye mulima na kuwateketeza kabisa katika dunia. Ee Yawe, tuliza hasira yako kali na kuacha jambo hilo baya ulilokusudia kufanya juu ya watu wako.

13 Uwakumbuke watumishi wako, Abrahamu, Isaka na Israeli, ambao uliwaapia kwa nafsi yako mwenyewe, ukisema: Nitawazidisha wazao wenu kama nyota za mbinguni na inchi yote hii niliyowaahidia nitawapa vizazi vyenu wairizi milele.

14 Basi, Yawe akaacha kuwafanyia watu wake lile jambo baya alilokuwa amesema.

15 Kisha Musa akashuka kutoka juu ya mulima akiwa na vile vibao viwili vya agano katika mikono yake, vimeandikwa amri za Mungu pande zote.

16 Vibao hivyo vilikuwa kazi ya Mungu mwenyewe na maandiko hayo Mungu mwenyewe aliyachora.

17 Yoshua aliposikia kelele za watu, akamwambia Musa: Kuna kelele za vita ndani ya kambi.

18 Lakini Musa akamujibu: Si kelele ya ushindi au kushindwa, lakini kelele ninayosikia ni kelele ya watu wanaoimba.

19 Mara tu walipokaribia kambi walimwona yule mwana-ngombe na watu wakicheza. Hapo hasira ya Musa ikawaka kama moto, akatupa chini vile vibao kutoka mikono yake na kuvivunja pale chini ya mulima.

20 Basi, akamutwaa yule mwana-ngombe akamuchoma kwa moto, akamusaga mpaka akakuwa unga, akakoroga unga huo katika maji na kuwalazimisha Waisraeli wakunywe.

21 Musa akamwuliza Haruni: Walikufanya nini watu hawa hata ukawaingiza katika zambi kubwa hivyo?

22 Haruni akamujibu: Ninakuomba, ee bwana wangu, hasira yako isiniwakie mimi mutumishi wako. Unafahamu jinsi watu hawa wanavyokuwa tayari kutenda maovu.

23 Walikuja wakaniambia: Utufanyie miungu ambayo itatuongoza, maana yule Musa aliyetutoa katika inchi ya Misri hatujui jambo lililomupata.

24 Nami nikawaambia, kila mumoja aliyekuwa na pete za zahabu azilete. Basi, wakaniletea, nami nikaziyeyusha juu ya moto na huyu mwana-ngombe akatokea.

25 Basi, Musa alipoona kwamba watu wameasi na kufanya wanavyopenda (kwa kuwa Haruni aliwafanya waasi na kufanya wanavyopenda na kujiletea haya mbele ya waadui zao),

26 Musa akasimama mbele ya mulango wa kambi na kuuliza: Ni nani anayekuwa upande wa Yawe? Akuje kwangu. Wana wote wa Lawi wakakusanyika pamoja mbele yake.

27 Akawaambia: Yawe, Mungu wa Israeli, anasema hivi: Kila mutu ajifungie upanga wake kwenye kiuno, azunguke kila pahali katika kambi, kutoka mulango moja mpaka mwingine, na kila mumoja amwue ndugu yake, rafiki yake na jirani yake.

28 Wana wa Lawi wakafanya kama vile Musa alivyowaagiza. Siku hiyo watu yapata elfu tatu waliuawa.

29 Musa akasema: Leo mumejitakasa ninyi wenyewe kwa kumutumikia Yawe, kwa vile hamukusita hata kuwaua watoto wenu au wandugu zenu. Mungu awajalie baraka leo hii.


Musa anawaombea Waisraeli

30 Kesho yake Musa akawaambia watu: Mumetenda zambi kubwa! Sasa nitamwendea Yawe juu kwenye mulima; labda nitafanya upatanisho kwa ajili ya zambi yenu.

31 Hivyo Musa akarudi kwa Yawe, akamwambia: Ninasikitika! Watu hawa wametenda zambi kubwa. Wamejifanyia wenyewe miungu ya zahabu.

32 Lakini sasa, ninakuomba uwasamehe zambi yao. Ikiwa hautawasamehe, ninakusihi unifute mimi katika kitabu chako ambamo uliwaandika watu wako.

33 Lakini Yawe akamwambia Musa: Nitamufuta katika kitabu changu mutu yeyote aliyenitendea zambi.

34 Lakini sasa kwenda uwaongoze watu mpaka pahali nilipokuambia. Malaika wangu atakutangulia. Hata hivyo, siku nitakapowafikia, nitawaazibu kwa sababu ya zambi yao.

35 Yawe akawaletea watu ugonjwa mukali, kwa kuwa walimwomba Haruni awafanyie yule mwana-ngombe wa zahabu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ