Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kutoka 30 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Mazabahu ya kufukizia ubani
( Kut 37.25-28 )

1 Utatengeneza mazabahu kwa mbao za mujohoro kusudi pawe pahali pa kufukizia ubani.

2 Mazabahu hiyo ikuwe ya muraba, urefu na upana wake sentimetre makumi ine na tano, na urefu kwenda juu sentimetre makumi tisa. Pembe zake za juu zitatokeza zote zikiwa kitu kimoja na mazabahu yenyewe.

3 Yote utaipakaa zahabu safi: upande wake wa juu, pande zake zote za ubavu na pembe zake. Vilevile utaizungushia ukingo wa zahabu.

4 Utaitengenezea pete mbili za zahabu na kuzitia chini ya ukingo wake kwenye pande mbili zinazoelekeana. Hizo pete zitatumiwa kwa kushikilia miti wakati wa kuibeba.

5 Miti hiyo ikuwe ya mujohoro na ipakwe zahabu.

6 Mazabahu hiyo iwekwe mbele ya pazia kando ya Sanduku la Agano, mbele ya kiti cha rehema ambapo nitakutana nawe.

7 Kila siku Haruni anapoingia kwa kutayarisha taa zinazokuwa pale, atafukiza ubani wenye harufu nzuri juu ya mazabahu hiyo.

8 Tena atafukiza ubani wakati wa magaribi anapowasha taa. Sadaka hii ya ubani itatolewa siku zote bila kukoma katika vizazi vyenu vyote.

9 Kwenye mazabahu hiyo, musifukize hata kidogo ubani usiokuwa mutakatifu, wala musitoe sadaka ya kuteketezwa, wala sadaka ya ngano, wala kumimina juu yake sadaka ya kinywaji.

10 Haruni atafanya upatanisho juu ya pembe za mazabahu hiyo mara moja kwa mwaka. Ataifanyia upatanisho kwa damu ya sadaka ya maondoleo ya zambi mara moja kila mwaka katika vizazi vyenu vyote, maana mazabahu hiyo ni takatifu kabisa kwangu, mimi Yawe.


Matoleo za hema la mukutano

11 Yawe akamwambia Musa:

12 Kila mara utakapowahesabu Waisraeli, kila mumoja atatoa malipo kwa Yawe kwa ajili ya nafsi yake kusudi kusikuwe hasara kati yao wakati wa kuhesabiwa.

13 Kila mumoja atakayehesabiwa anapaswa kulipa nusu ya shekeli kulingana na vipimo vya hema la mukutano. Hii ni sadaka yake atakayonitolea.

14 Kila mumoja atakayehesabiwa, tangu umri wa miaka makumi mbili na zaidi, atanitolea sadaka hiyo.

15 Tajiri asitoe zaidi wala masikini asitoe chini ya nusu ya shekeli wakati munaponitolea sadaka hiyo kwa kufanya upatanisho.

16 Wewe utaipokea feza hiyo ya upatanisho kutoka kwa Waisraeli, nawe utaitumia kwa shuguli za kazi za hema takatifu, nayo ikuwe ni ukumbusho wa Waisraeli mbele yangu, malipo ya maisha yenu.

17 Yawe akamwambia Musa:

18 Utatengeneza birika la shaba kwa kuoga lenye tako la shaba, uliweke katikati ya hema la mukutano na mazabahu, na kutia maji ndani yake.

19 Haruni na wana wake watatumia maji hayo kwa kunawa mikono na miguu,

20 mbele ya kuingia kwenye hema la mukutano au kukaribia mazabahu kwa kunitolea sadaka mimi Yawe, sadaka za kuteketezwa kwa moto. Watafanya hivyo kusudi wasikufe.

21 Wanapaswa kunawa mikono na miguu yao kusudi wasikufe. Hili ni sharti kwao siku zote, tangu Haruni na uzao wake, vizazi kwa vizazi.


Mafuta ya kupakaa

22 Yawe akamwambia Musa:

23 Utatwaa viungo bora kabisa kama hivi: manemane ya maji kilo sita, mudalasini wenye harufu nzuri kilo tatu, miwa yenye harufu nzuri kilo tatu,

24 na aina nyingine ya mudalasini kilo sita – vipimo hivyo vyote vikuwe kufuatana na vipimo vya hema takatifu. Twaa vilevile litre ine za mafuta.

25 Kutokana na viungo hivyo utatengeneza mafuta matakatifu uyachanganye kama vile fundi wa manukato anavyofanya. Hayo yatatumika kwa kutakasa vitu.

26 Kisha utamiminia hema la mukutano mafuta hayo, Sanduku la Agano,

27 meza na vyombo vyake vyote, kinara cha taa na vyombo vyake, mazabahu ya kufukizia ubani,

28 mazabahu ya sadaka za kuteketezwa kwa moto na vyombo vyake vyote, na birika na tako lake.

29 Utavitakasa, kusudi vikuwe vitakatifu kabisa. Chochote kitakachogusa vifaa hivyo, kitakuwa kitakatifu.

30 Kisha umupakae Haruni mafuta na wana wake na kuwatakasa kusudi wanitumikie kama vile makuhani.

31 Uwaambie Waisraeli kwamba haya yatakuwa mafuta yangu matakatifu ya kupakaa katika vizazi vyenu vyote.

32 Mafuta haya yasimiminiwe hata kidogo mutu yeyote wa kawaida, wala kusitengenezwe mafuta mengine ya aina hii. Haya ni mafuta matakatifu na yanapaswa kuwa siku zote matakatifu kwenu.

33 Yeyote atakayetengeneza mafuta kama haya, au kumupakaa mutu asiyestahili kupakwa mafuta haya, mutu huyu atatengwa mbali na watu wake.

34 Yawe akamwambia Musa: Utatwaa vipimo vinavyolingana vya viungo vitamu hivi: utomvu wa natafi, utomvu wa shekeleti, utomvu wa kelbena na ubani safi.

35 Utatumia vitu hivyo kwa kutengeneza ubani kama vile unavyotengenezwa na fundi wa manukato, utiwe chumvi upate kuwa safi na mutakatifu.

36 Kisha utasagwa na kufanya unga laini, upate kutumiwa ndani ya hema la mukutano na kulipakaa Sanduku la Agano, pahali nitakapokutana nawe. Huo utakuwa ubani mutakatifu kabisa kwenu.

37 Musifanye hata kidogo ubani wa muchanganyiko huo kwa matumizi yenu wenyewe maana ubani huo utakuwa mutakatifu mbele yangu.

38 Yeyote atakayejitengenezea ubani wa aina hiyo na kuutumia kama manukato yake pekee, atatengwa mbali na watu wake.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ