Kutoka 28 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Nguo za makuhani ( Kut 39.1-7 ) 1 Nawe Musa umulete kwangu Haruni ndugu yako, pamoja na wana wake: Nadabu, Abihu, Eleazari na Itamari. Utawachagua kati ya Waisraeli, kusudi wanitumikie kama vile makuhani. 2 Utamushonea ndugu yako Haruni nguo takatifu kusudi apate kuonekana mwenye utukufu na muzuri. 3 Uwaagize wafundi wote ambao nimewapa maarifa wamutengenezee Haruni nguo kusudi atakaswe kwa ajili ya kazi ya ukuhani. 4 Uwaambie wamutengenezee vitu hivi: kifuko cha kifua, kizibao, kanzu, na ingine yenye kupambwa vizuri, kofia na mukaba. Ndugu yako Haruni na wana wake watavaa nguo zile kusudi wanitumikie kama vile makuhani. 5 Hao wafundi watatumia sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na nyuzi za zahabu na kitani safi iliyosokotwa. Kizibao cha kuhani 6 Watatengeneza kizibao cha kuhani kwa nyuzi za zahabu na sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kupambwa vizuri. 7 Kitakuwa kamba mbili za kukifungia juu ya mabega zilizoshonewa kwenye incha zake mbili. 8 Mukaba wa kukishikia utatengenezwa kwa vifaa hivyohivyo: kwa nyuzi za zahabu, sufu ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa na kuwa kitu kimoja na kizibao kile. 9 Kisha utatwaa mawe mawili ya sardoniki ambayo utachora juu yake majina ya wana wa Israeli. 10 Majina sita katika jiwe la kwanza, na majina sita yaliyobakia katika jiwe la pili, majina yafuatane kadiri ya kuzaliwa kwao. 11 Utayachora majina yale juu ya yale mawe kama vile muchoraji anavyochora muhuri, kisha uyaingize katika kingo za zahabu. 12 Mawe hayo mawili yatawekwa juu ya mikaba ya kizibao kama vile ukumbusho wa makabila kumi na mawili ya Israeli. Hivyo Haruni atavaa majina hayo juu ya mabega yake mbele yangu mimi Yawe kama vile ukumbusho. 13 Utayatengenezea kingo mbili za zahabu, 14 na mikufu miwili ya zahabu safi iliyosokotwa kama kamba. Utafunga mikufu ile kwenye zile kingo. Kifuko cha kifua ( Kut 39.8-21 ) 15 Utatengeneza kifuko cha kifua cha maamuzi. Kitengenezwe kwa ufundi sawa vile kile kizibao kilivyotengenezwa: kwa zahabu, kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa. 16 Kifuko hicho ambacho kimekunjwa kitakuwa cha muraba, sentimetre makumi mbili na mbili. 17 Kitapambwa kwa mistari ine ya mawe ya bei kali. Mustari wa kwanza utakuwa wa akiki, topazi na almasi nyekundu; 18 mustari wa pili utakuwa wa zumaridi, yakuti samawi na almasi; 19 mustari wa tatu utakuwa wa yasinto, akiki nyekundu na ametisto; 20 na mustari wa ine utakuwa wa zabarajadi, shohamu na yaspi. Yote yatatiwa kwenye kingo za zahabu. 21 Basi, kutakuwa mawe kumi na mawili yaliyochorwa majina kumi na mawili ya wana wa Israeli. Kila moja litakuwa kama muhuri, kwa kusimamia makabila yale kumi na mawili. 22 Kwa ajili ya kifuko kile cha kifua, utatengeneza mikufu ya zahabu safi iliyosokotwa kama kamba. 23 Vilevile utatengeneza pete mbili za zahabu kwa ajili ya kifuko cha kifua na kuzitia kwenye incha mbili za kifuko hicho, 24 na mikufu miwili ya zahabu uifunge kwenye pete zile za kifuko cha kifua. 25 Zile incha mbili za mukufu wa zahabu utazishikamanisha kwenye zile kingo mbili za kile kifuko kusudi zishikamane na kipande cha mabega cha kizibao upande wa mbele. 26 Vilevile utatengeneza pete mbili za zahabu na kuzitia kwenye incha mbili za chini upande wa ndani wa kifuko cha kifua karibu na kizibao. 27 Kisha utatengeneza pete zingine mbili za zahabu na kuzitia mbele katika incha za chini za vipande vya kizibao, pahali kizibao kinapoungana na mukaba uliofumwa kwa ufundi. 28 Kifuko cha kifua kitafungwa kwenye kizibao kwa kufunganisha pete zake na kizibao kwa kamba ya rangi ya samawi, kusudi kifuko kile cha kifua kisiregee lakini kikalie ule mukaba uliofumwa kwa ufundi. 29 Haruni anapoingia Pahali Patakatifu, atavaa kifuko cha shauri ambacho juu yake kulichorwa majina ya makabila ya wana wa Israeli. Kwa namna hiyo mimi Yawe sitawasahau ninyi hata kidogo. 30 Kwenye kifuko hicho utatia mawe ya shauri yaninginie kwenye kifua cha Haruni kila mara anapokuja mbele yangu. Wakati ule anapaswa kila mara kuvaa kifuko kile, kusudi aweze kutambua mapenzi yangu juu ya Waisraeli. Ngua zingine za kikuhani ( Kut 39.22-31 ) 31 Utashona kanzu ya kuvalia chini ya kizibao ikiwa yote ya rangi ya samawi. 32 Kanzu ile itakuwa na nafasi ya kupitishia kichwa katikati na nafasi hiyo itazungushiwa utepe uliofumwa kusudi isichanike. 33 Kwenye upindo wake wa chini, kuzunguka pande zote, itapambwa kwa makomamanga ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu. Kutakuwa vilevile kengele za zahabu kati ya hayo makomamanga: 34 komamanga, kengele, komamanga, kengele, kuizunguka kanzu yote. 35 Haruni atavaa kanzu ile kwa kutimiza kazi yake ya kuhani na sauti yake itasikilika wakati anapoingia Pahali Patakatifu mbele yangu na wakati anapotoka, kengele hizo zitasikilika, naye hatauawa. 36 Kisha, utatengeneza bamba la zahabu safi na kuchora juu yake maneno haya kama vile mutu anavyochora muhuri: Takatifu kwa ajili ya Yawe. 37 Utalifungia bamba lile mbele ya kofia kwa mukaba wa rangi ya samawi. 38 Haruni atavaa bamba lile kwenye paji la uso wake. Kwa njia ya bamba lile atabeba mashitaki ya makosa ambayo Waisraeli wanaweza kuwa wamefanya katika kunitolea sadaka takatifu, nami nitakubali sadaka zao. 39 Utamutengenezea Haruni kanzu iliyochorwa kwa kitani safi na kumufumia kofia ya kitani safi na mukaba uliopambwa vizuri. 40 Utawatengenezea wana wa Haruni kanzu, mikaba na kofia kusudi waonekane wana utukufu na uzuri. 41 Utamuvalisha ndugu yako Haruni na wana wake nguo zile, kisha uwapakae mafuta na kuwawekea mikono kwa kuwatakasa wanitumikie kama vile makuhani. 42 Vilevile utawashonea makapitula za kitani zitakazowafunika tangu kwenye kiuno mpaka kwenye mapaja, kusudi wafunike uchi wao. 43 Haruni na wana wake watavaa makapitula hizo kila mara wanapoingia katika hema la mukutano, au wanapokaribia kwenye mazabahu, kufanya kazi za makuhani katika Pahali Patakatifu. Kwa njia hiyo hawataonyesha uchi wao na kuwa na hatari ya kuuawa. Hilo ni sharti la kufuatwa siku zote kwa Haruni na wazao wake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo