Kutoka 27 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mazabahu ( Kut 38.1-7 ) 1 Utatengeneza mazabahu kwa mbao za mujohoro. Mazabahu ile itakuwa ya muraba, urefu wake metre mbili na sentimetre makumi mbili, na upana wake metre mbili na sentimetre makumi mbili. Urefu kwenda juu utakuwa metre moja na sentimetre makumi mbili. 2 Katika kila pembe ya mazabahu ile utatengeneza upembe ambao utakuwa umeundwa kutokana na mazabahu yenyewe. Mazabahu ile yote utaipakaa shaba. 3 Utaitengenezea vyombo vyake: vyungu vya kuwekea majivu, majembe, na mabeseni, na kanya na visahani vya kutwalia moto. Vyombo vyake vyote utavitengeneza kwa shaba. 4 Kisha utatengeneza wavu wa shaba wenye pete ine za shaba kwenye pembe zake ine. 5 Wavu ule utauweka kwenye ukingo wa mazabahu upande wa chini kusudi ufike katikati ya mazabahu. 6 Utatengeneza vilevile miti ya mujohoro ya kubebea mazabahu, nayo utaipakaa shaba. 7 Miti ile itaingizwa kwenye zile pete kila upande wa mazabahu wakati wa kuibeba. 8 Utatengeneza mazabahu kwa mbao, ikuwe wazi ndani, kulingana na mufano niliokuonyesha juu ya mulima. Kiwanja cha hema la mukutano ( Kut 38.9-20 ) 9 Utatengeneza kiwanja cha hema la mukutano. Kwa upande wa kusini wa kiwanja kutakuwa nguo zilizotengenezwa kwa kitani safi iliyosokotwa ambazo zitakuwa na urefu wa metre makumi ine na ine kwa upande mumoja. 10 Nguo zile zitashikiliwa na nguzo makumi mbili za shaba zenye vikalio vya shaba. Lakini vifungio vya nguzo zile na kamba zake vitakuwa vya feza. 11 Vilevile upande wa kaskazini, urefu wa nguo utakuwa metre makumi ine na ine, na nguzo zake makumi mbili za shaba, lakini vifungio vya nguzo na kamba zake vitakuwa vya feza. 12 Upande wa magaribi wa kiwanja utakuwa na nguo yenye urefu wa metre makumi mbili na mbili na nguzo zake kumi na vikalio vyake kumi. 13 Upande wa mashariki kunakokuwa mulango, kiwanja kitakuwa na upana wa metre makumi mbili na mbili. 14 Nguo ya upande mumoja wa mulango itakuwa na upana wa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. 15 Vilevile katika upande wa pili wa mulango nguo itakuwa metre sita na nusu, pamoja na nguzo tatu na vikalio vyake vitatu. 16 Mulango wenyewe wa kiwanja utakuwa na pazia zito lenye urefu wa metre tisa, lililotengenezwa kwa sufu ya rangi ya samawi, zambarau na nyekundu, na kitani safi iliyosokotwa, na kuchorwa vizuri. Pazia lile litashikiliwa na nguzo ine zenye vikalio vine. 17 Nguzo zote kuzunguka kiwanja zitashikamanishwa kwa fito za feza. Vifungio vyake vitakuwa vya feza na vikalio vyake vitakuwa vya shaba. 18 Kiwanja kile kitakuwa na urefu wa metre makumi ine na ine, upana wa metre makumi mbili na mbili, na urefu kwenda juu wa metre mbili na sentimetre makumi mbili. Nguo zake zitakuwa za kitani safi na vikalio vyake vya shaba. 19 Vyombo vyote vya hema takatifu vya matumizi ya kila aina, pamoja na misumari vyote na hata vile vya kiwanja, vitakuwa vya shaba. Taa ( Law 24.1-4 ) 20 Utawaamuru Waisraeli wakuletee mafuta safi kwa ajili ya taa, kuwe taa inayowaka siku zote. 21 Hiyo itakuwa ndani ya hema la mukutano inje ya pazia lile mbele ya Sanduku la Agano na Haruni na wana wake wataitunza mbele yangu tangu magaribi mpaka asubui. Sharti hili lifuatwe siku zote na Waisraeli wote, kizazi kwa kizazi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo