Kutoka 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Yetro anamutembelea Musa Vita na Waamaleki 1 Yetro, kuhani wa Midiani, baba mukwe wa Musa, alisikia juu ya mambo yote ambayo Yawe alimutendea Musa na Waisraeli alipowatoa katika inchi ya Misri. 2 Kwa hiyo Yetro, akiwa na Sipora muke wa Musa ambaye Musa alikuwa amemurudisha kwa baba yake, alimwendea Musa, 3 pamoja na watoto wawili wa Musa. Mutoto wa kwanza aliitwa Gersomi. Musa alimupa jina hili kwa vile alisema: “Nimekimbilia katika inchi ya kigeni.” 4 Wa pili aliitwa Eliezeri, kwa vile Musa alisema: “Mungu wa baba yangu ndiye aliyenisaidia nisiuawe na mufalme wa Misri.” 5 Yetro, baba mukwe wa Musa, alikuja pamoja na binti yake, ni kusema muke wa Musa, pamoja na watoto. Akamukuta Musa katika jangwa alikokuwa amepiga kambi kwenye mulima wa Mungu. 6 Musa alipoambiwa kwamba baba mukwe wake pamoja na muke wake na wana wake wawili wanakuja, 7 akatoka kwenda kumupokea baba mukwe wake, akiinama mbele yake na kumubusu. Wakasalimiana, kisha wakaingia ndani ya hema. 8 Musa akamwelezea baba mukwe wake mambo yote Yawe aliyomutendea mufalme wa Misri na Wamisri kwa ajili ya Waisraeli. Akamwambia vilevile juu ya shida zote zilizowapata katika safari na jinsi Yawe alivyowaokoa. 9 Yetro akafurahishwa na yote Yawe aliyotenda kwa ajili ya Waisraeli, kwa kuwaokoa toka katika mikono ya Wamisri. 10 Yetro akasema: “Atukuzwe Yawe ambaye amewaokoa toka katika mikono ya Wamisri na kutoka katika mukono wa mufalme wa Misri. 11 Sasa ninajua kwamba Yawe ni mukubwa kuliko miungu yote, maana amewakomboa watu hawa toka katika mikono ya Wamisri ambao waliwatendea ubaya.” 12 Halafu Yetro, baba mukwe wa Musa, akamutolea Mungu sadaka za kuteketezwa kwa moto na sadaka zingine. Naye Haruni akakuja pamoja na wazee wa Israeli kwa kula chakula pamoja na Yetro, mbele ya Yawe. Kuchaguliwa kwa waamuzi ( Kumb 1.9-18 ) 13 Kesho yake, Musa akaikaa kwa kuamua matatizo ya Waisraeli, nao wakasimama wakiwa wamemuzunguka, tangu asubui mpaka magaribi. 14 Yetro, baba mukwe wa Musa, alipoona mambo yote ambayo Musa aliwafanyia Waisraeli, akamwuliza: “Kwa nini unawafanyia watu mambo haya? Mbona unaikaa peke yako wakati watu wamekuzunguka tangu asubui mpaka magaribi?” 15 Musa akamujibu baba mukwe wake: “Kwa sababu watu wanakuja kwangu kuuliza mapenzi ya Mungu. 16 Wakiwa na ugomvi wowote wao wanakuja kwangu nami ninaamua kati ya mutu na mwenzake na kuwafundisha masharti ya Mungu na maamuzi yake.” 17 Basi, Yetro akamwambia Musa: “Unavyofanya si vizuri! 18 Utajichokesha mwenyewe na hawa watu, maana hii ni kazi ngumu usiyoweza kuifanya peke yako. 19 Sikiliza shauri langu kwako na Mungu akuwe pamoja nawe. Wewe utawasimamia watu mbele ya Mungu na kumuletea Mungu matatizo yao. 20 Vilevile utawafundisha masharti na sheria ya Mungu na kuwaonyesha jinsi inavyowapasa kuishi na kufanya. 21 Lakini juu ya mambo mengine, chagua kati ya watu wote, watu wanaostahili, watu wanaomwogopa Mungu, waaminifu na wanaochukia kituliro. Uwape hao mamlaka, wakuwe na kazi ya kuwasimamia watu katika makundi ya watu elfu, mia, makumi tano na kumikumi. 22 Hao ndio watakaokuwa na vikao kila siku kutatua matatizo ya watu. Matatizo magumu watakuletea wewe, lakini yale madogomadogo watayaamua wenyewe. Kwa njia hiyo utaweza kufanya kazi yako kuwa nyepesi kwa vile watashirikiana nawe katika kazi hiyo. 23 Ukifanya hivyo na kama ndivyo Mungu anavyotaka, utaweza kuvumilia na watu hawa wote wataweza kurudi kwao kwa amani.” 24 Musa akasikiliza shauri lile la baba mukwe wake na kufanya kama vile alivyoshauriwa. 25 Basi, akachagua watu wenye uwezo kati ya Waisraeli, akawafanya kuwa viongozi wa makundi ya watu elfu, watu mia, watu makumi tano na watu kumikumi. 26 Nao wakakuwa wanaamua matatizo ya watu kila wakati. Matatizo magumu walimuletea Musa, lakini yale madogomadogo waliyatatua wao wenyewe. 27 Kisha kufanya hivyo, Musa na baba mukwe wake wakaagana, naye Yetro akarudi katika inchi yake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo