Kumbukumbu la Sheria 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 “Mutakuwa waangalifu kwa kutenda amri zote ninazowapa leo, kusudi mupate kuishi na kuongezeka, na muingie na kuirizi inchi ile ambayo Yawe aliapa kuwapa babu zenu. 2 Mukumbuke jinsi Yawe, Mungu wenu, alivyowaongoza katika safari ndefu kupitia katika jangwa kwa muda wa miaka hiyo makumi ine, kusudi awanyenyekeze na kuwajaribu kusudi ajue yanayokuwa ndani ya mioyo yenu, na kama mungeshika amri zake au hapana. 3 Aliwazarau akawaacha muone njaa na kisha akawapa mana mukule, chakula ambacho hamukukijua, wala babu zenu hawajapata kukijua. Alifanya hivyo kusudi apate kuwafundisha kwamba mwanadamu haishi kwa mukate tu, lakini kwa kila neno Yawe analosema. 4 Wakati huo wa miaka makumi ine nguo zenu hazikuchakaa, wala miguu yenu haikuvimba. 5 Mukumbuke kwamba Yawe, Mungu wenu, anawaazibu kama vile baba anavyoazibu mwana wake. 6 Hivyo, mushike amri za Yawe, Mungu wenu, mupate kufuata njia zake na kumwogopa yeye. 7 Yawe, Mungu wenu, anawaleta kwenye inchi nzuri, inchi yenye vijito na chemichemi, na maji yanayobubujika kutoka bonde na milima; 8 inchi yenye ngano na shayiri, mizabibu, mitini, mikomamanga, mizeituni na asali. 9 Huko mutapata chakula tele na hamutapungukiwa kitu. Mawe yake yana chuma, na kwenye milima yake munaweza kuchimba shaba. 10 Mutakula na kushiba, mutamushukuru Yawe, Mungu wenu, kwa inchi nzuri aliyowapa. Onyo juu ya kumusahau Yawe 11 “Muhakikishe kwamba hamutamusahau Yawe, Mungu wenu, kwa kutoshika amri zake, maagizo yake na masharti yake ninayowaamuru leo. 12 Mukisha kula na kushiba, kujijengea nyumba nzuri na kuishi humo, 13 na wakati ambapo ngombe na kondoo wenu, zahabu na feza yenu, na kila kitu munachokuwa nacho kitakuwa kimeongezeka, 14 musikuwe na kiburi na kumusahau Yawe, Mungu wenu, aliyewatoa katika inchi ya Misri, pahali mulipokuwa watumwa. 15 Ni yeye aliyewaongoza katika lile jangwa kubwa na la kutisha, lenye nyoka wenye sumu na nge katika inchi ile yenye kukauka isiyokuwa na maji, aliwatolea maji kutoka kwenye jiwe gumu. 16 Tena ni yeye aliyewakulisha mana katika jangwa, chakula ambacho babu zenu hawajapata kukijua. Alifanya hayo yote kusudi awanyenyekeze na kuwajaribu kwa kuwapima apate kuwajalia mema kwa mwisho. 17 Hivyo mufanye angalisho kusudi musijisemeshe ndani ya mioyo yenu: ‘Tumejitajirisha kwa uwezo na nguvu zetu wenyewe’. 18 Mukumbuke kwamba Yawe, Mungu wenu, ndiye anayewapa uwezo wa kupata utajiri. Anafanya hivyo kwa kuimarisha agano alilofanya na babu zenu mpaka leo. 19 Lakini mukimusahau Yawe, Mungu wenu, na kufuata miungu mingine kwa kuitumikia na kuiabudu, ninawaonya vikali leo hii kwamba hakika mutaangamia. 20 Musipomutii Yawe, mutaangamia kama vile mataifa ambayo anayaangamiza mbele yenu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo