Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kumbukumbu la Sheria 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Taifa chaguliwa la Yawe
( Kut 34.11-16 )

1 “Yawe, Mungu wenu atawafikisha kwenye inchi ambayo mutakwenda kufanya makao yenu na atafukuza mataifa mengi kutoka inchi hiyo. Mutakapoingia, atafukuza mbele yenu mataifa saba makubwa na yenye nguvu kuliko ninyi: Wahiti, Wagirgasi, Waamori, Wakanana, Waperizi, Wahivi, na Wayebusi.

2 Vilevile, kisha Yawe, Mungu wenu, kuyatia katika mikono yenu, mutayashinda na kuyaangamiza kabisa. Musifanye agano lolote nayo wala musiyahurumie.

3 Musioane nayo, wala musiyaoeshee wabinti zenu au wana wenu.

4 Mukifanya hivyo wao watawapotosha watoto wenu wasimufuate Yawe, na kuwafanya waabudu miungu mingine, nayo hasira ya Yawe itawaka juu yenu, halafu atawaangamiza mara moja.

5 Lakini muwatendee hivi: Mutavunja mazabahu zao na kubomoa nguzo zao. Na sanamu za Ashera mutakata na kuchoma sanamu zao za kuchonga.

6 Mufanye hivyo kwa sababu ninyi mumetakaswa kwa Yawe, Mungu wenu. Kati ya watu wote katika ulimwengu aliwachagua ninyi kusudi mukuwe taifa lake mwenyewe.

7 “Yawe hakuwapenda ninyi na kuwachagua kwa sababu ninyi ni wengi sana kuliko watu wengine; ninyi mulikuwa wachache kuliko mataifa mengine katika dunia.

8 Lakini ni kwa sababu Yawe anawapenda na anashika kiapo alichowaapia babu zenu, ndiyo maana aliwaokoa kwa nguvu zake kubwa na kuwaokoa toka katika utumwa, toka mikono ya mufalme wa Misri.

9 Basi, mujue kwamba Yawe, Mungu wenu, ndiye Mungu. Yeye ni Mungu mwaminifu, anayeshika agano lake na kutenda mema kwa vizazi vingi vya wale wanaomupenda na kushika amri zake.

10 Lakini hatasita kuwaazibu wale wanaomuchukia.

11 Kwa hiyo mukuwe waangalifu kushika amri, masharti na maagizo ninayowaamuru leo.


Inchi nzuri ya kurizi
( Kumb 28.1-14 )

12 “Mukisikiliza maagizo haya na kuyashika hata kuyatenda, Yawe, Mungu wenu, atashika agano lake nanyi na kuwatendea mema kama vile alivyowaahidi babu zenu.

13 Atawapenda na kuwabariki, nanyi mutaongezeka na kuwa na wazao wengi. Atabariki mashamba yenu kusudi mupate ngano, divai na mafuta. Atawabariki kwa kuwapa ngombe na kondoo wengi katika inchi aliyowaahidi babu zenu kwamba atawapa ninyi.

14 Mutabarikiwa kuliko watu wengine wote katika ulimwengu. Kati yenu hakutakuwa mwanaume wala mwanamuke tasa.

15 Yawe atawaondolea magonjwa yote na hamutapatwa na magonjwa yoyote ya kutisha kama yaliyowapata huko Misri, lakini atawapa waadui zenu magonjwa hayo.

16 Muangamize taifa lolote ambalo Yawe, Mungu wenu atalitia katika mikono yenu, wala musilionee huruma. Musiabudu miungu yao, maana jambo hili litakuwa mutego kwenu.

17 “Musijisemeshe ndani mioyo yenu: ‘Watu hawa ni wengi kuliko sisi, tunaweza namna gani kuwafukuza toka katika inchi?’

18 Musiwaogope, mukumbuke vile Yawe, Mungu wenu, alivyomutendea mufalme wa Misri na inchi nzima ya Misri.

19 Mukumbuke ugonjwa mukali muliouona kwa macho yenu, miujiza na maajabu na nguvu kubwa na uwezo mukubwa, ambavyo Yawe, Mungu wenu alitumia kwa kuwakomboa; vile ndivyo atakavyowatendea watu munaowaogopa.

20 Zaidi ya hayo, Yawe, Mungu wenu, atatuma nyuki kati yao na kuwaangamiza wale ambao watawatoroka kwa kujificha.

21 Basi, musiwaogope, kwa sababu Yawe, Mungu wenu, yuko kati yenu. Yeye ni Mungu mukubwa na wa kutisha.

22 Yawe, Mungu wenu, atafukuza mataifa haya kadiri munavyosonga mbele kidogokidogo. Hamutaweza kuyaangamiza yote kwa mara moja, kwa sababu mukifanya hivyo hesabu ya nyama wa pori itazidi na kuwa kitisho kwenu.

23 Yawe, Mungu wenu, atawatia waadui zenu katika mikono yenu na atawafanya wahangaike mpaka waangamie.

24 Atawatia wafalme wao katika mikono yenu. Mutawaua, nao watasahaulika. Hakuna mutu yeyote atakayeweza kuwazuia, mpaka mutakapowaangamiza.

25 Muteketeze kwa moto sanamu za miungu yao. Musitamani feza wala zahabu yao, wala musiitwae na kuifanya mali yenu. Kufanya hivyo ni mutego kwenu na ni chukizo kwa Yawe, Mungu wenu.

26 Musipeleke sanamu zozote katika nyumba zenu, kama sivyo, mutalaaniwa kama sanamu hizo. Muzichukie na kuzizarau kwa sababu ni vitu vilivyolaaniwa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ