Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Kumbukumbu la Sheria 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Utangulizi

1 Kitabu hiki kina maneno ambayo Musa aliwaambia watu wote wa Israeli wakati walipokuwa katika jangwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Walikuwa katika bonde la Yordani karibu na Sufu, kati ya muji wa Parani upande mumoja na miji ya Tofeli, Labani, Hazeroti na Dizahabu upande mwingine.

2 (Ni mwendo wa siku kumi na moja kutoka mulima Horebu mpaka Kadesi-Barnea kwa njia ya mulima Seiri.)

3 Siku ya kwanza ya mwezi wa kumi na moja, mwaka wa makumi ine nyuma ya kutoka Misri, Musa akawaambia watu kila kitu ambacho Yawe alimwamuru awaambie.

4 Alifanya hivyo kisha Yawe kumushinda mufalme Sihoni wa Waamori ambaye alikuwa anakaa katika muji wa Hesiboni, na mufalme Ogi wa Basani ambaye alikuwa anakaa katika muji wa Astaroti na Edirei.

5 Musa akaanza kuwaelezea watu sheria ya Mungu wakati walipokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani. Akawaambia hivi:

6 “Tulipokuwa kwenye mulima Sinai, Yawe, Mungu wetu, alituambia hivi: ‘Mumekaa muda wa kutosha kwenye mulima huu.

7 Sasa muvunje kambi yenu muendelee na safari. Muende kwenye inchi ya milima ya Waamori na maeneo ya inchi jirani katika Araba, kwenye milima na mabonde, huko Negebu na sehemu za pembeni ya bahari. Muende mpaka inchi ya Kanana, na inchi ya Lebanoni, mpaka kwenye ule muto mukubwa Furati.

8 Inchi hii yote nimeiweka mbele yenu. Basi, muende kutwaa inchi hiyo ambayo mimi Yawe niliapa kuwapa wazee wenu Abrahamu, Isaka, Yakobo na wazao wao.’ ”


Musa anachagua waamuzi
( Kut 18.13-27 )

9 Musa akawaambia watu: “Tulipokuwa tungali kwenye mulima Sinai, mimi niliwaambia hivi: ‘Siwezi mimi mwenyewe kubeba muzigo wa kuwaongoza ninyi peke yangu.

10 Yawe, Mungu wenu, amewafanya mukuwe wengi; leo mumekuwa wengi kama vile nyota za mbinguni.

11 Yawe, Mungu wa babu zenu, awafanye muzidi kuongezeka mara elfu zaidi ya vile munavyokuwa sasa na kuwabariki kama vile alivyoahidi!

12 Lakini mimi peke yangu nitaweza namna gani kubeba muzigo wa kuamua matatizo yenu, mashitaki yenu na magomvi yenu?

13 Muchague kutoka katika kila kabila watu wenye hekima, akili na ujuzi kusudi niwafanye wakuwe viongozi wenu.’

14 Ninyi mulikubali, mukanijibu hivi: ‘Jambo ulilosema ni jema kwetu kufanya’.

15 Hivyo nikatwaa wale viongozi wenye hekima, akili na ujuzi ambao muliwachagua kutoka katika makabila yenu, nikawaweka kuwa viongozi wenu. Nikawaweka wengine kuwa majemadari wa makundi ya watu elfu moja moja, ya watu mia moja moja, ya watu makumi tano tano na ya watu kumi kumi. Nikachagua vilevile wakubwa wengine wa kuchunga kila kabila.

16 “Wakati uleule nikawapa waamuzi wenu maagizo haya: ‘Musikilize maneno ya watu wenu. Mutoe hukumu za haki katika maneno kati ya kila mumoja na ndugu yake au na wageni wanaoishi pamoja nanyi.

17 Musipendelee mutu yeyote katika kutoa hukumu; mutawasikiliza bila upendeleo, wakubwa kwa wadogo. Musiogopeshwe na sura ya mutu, maana ninyi mutapaswa kuhukumu kwa ajili ya Mungu. Kukikuwa maneno ambayo ni magumu sana kwenu, mutayafikisha kwangu nami nitayasikiliza.’

18 Wakati huohuo, nikawaagiza mambo yote munayopaswa kufanya.


Uasi wa Israeli juu ya inchi ya ahadi
( Hes 13.1-33 )

19 “Basi, kama vile Yawe, Mungu wetu, alivyotuamuru, tukaanza safari yetu kutoka mulima Horebu, tukapita katika lile jangwa kubwa la kutisha munalojua, kwa kufuata njia inayoelekea inchi ya milima ya Waamori. Tulipofika Kadesi-Barnea,

20 mimi nikawaambia: ‘Sasa mumefika katika inchi ya milima ya Waamori ambayo Yawe, Mungu wetu, ametupatia.

21 Muangalie, Yawe, Mungu wenu, ameiweka inchi hii mbele yenu. Basi! Muende, muirizi kama vile Yawe, Mungu wa wazee wenu alivyowaambia. Musiogope wala musifazaike!’

22 “Kisha wote mukakuja karibu nami mukaniambia: ‘Tutume watu watutangulie, wapeleleze inchi, halafu warudi kutujulisha njia bora ya kufuata na miji gani tutakuta huko.’

23 Jambo hilo likaonekana kuwa zuri kwangu, nikawachagua watu kumi na wawili, mutu mumoja kutoka katika kila kabila.

24 Watu hao wakakwenda katika inchi ile ya milima, wakafika kwenye bonde la Eskoli na kulipeleleza.

25 Waliporudi, wakatuletea matunda mamoja ya inchi hiyo na wakatuarifu kwamba inchi hiyo Yawe, Mungu wetu, anayotupatia ni nzuri.

26 “Lakini ninyi hamukufuata agizo la Yawe, Mungu wenu; mulikataa kwenda katika inchi hiyo.

27 Mulinungunika ndani ya mahema yenu mukisema: ‘Yawe anatuchukia na ndiyo maana alitutoa katika inchi ya Misri. Alitaka kututia katika mikono ya Waamori kusudi atuangamize.

28 Kwa nini tuende huko wakati tumevunjika moyo kwa hofu? Wametuambia kwamba watu wa huko ni wakubwa na warefu kuliko sisi, na kwamba miji yao ni mikubwa na yenye kuta zinazofika katika mawingu. Tena wamesema kwamba waliwaona wale wazao wa Anaki!’

29 “Lakini mimi nikawaambia hivi: ‘Musikuwe na hofu wala musiwaogope watu hao.’

30 Yawe, Mungu wenu, ambaye anawatangulia, yeye mwenyewe atapigana kwa ajili yenu kama vile alivyofanya mbele yenu kule Misri na

31 kule katika jangwa ambako muliona jinsi alivyowabeba safari hiyo yote kama vile baba anavyobeba mwana wake, mpaka mukafika hapa.

32 Lakini ingawa nilisema hayo yote, ninyi hamukumwamini Yawe, Mungu wenu,

33 ambaye aliwatangulia katika njia na kuwatafutia pahali pa kupiga kambi zenu. Usiku aliwatangulia kwa moto na muchana kwa wingu, kwa kuwaonyesha njia.

34 “Yawe akasikia manunguniko yenu, akakasirika, akaapa akisema:

35 ‘Hakuna hata mumoja wenu katika kizazi hiki kiovu atakayeingia katika ile inchi nzuri niliyoahidi kuwapa wazee wenu.

36 Kalebu mwana wa Yefune, ndiye tu atakayeiona. Nami nitamupatia inchi hiyo aliyokanyaga ndani ikuwe yake yeye na wazao wake kwa sababu amekuwa mwaminifu kabisa kwangu.’

37 Yawe akanikasirikia mimi vilevile kwa sababu yenu, akasema: ‘Hata wewe Musa hautaingia katika inchi hiyo.

38 Lakini musaidizi wako Yoshua mwana wa Nuni ataingia humo. Basi, umutie moyo maana yeye atawaongoza watu wa Israeli wairizi inchi hiyo’.

39 Kisha Yawe akatuambia sisi wote: ‘Hao watoto wenu munaoogopa kwamba watakuwa mateka za waadui zenu, hakika hao wanaokuwa wadogo ambao hawajui bado kupambanua kati ya mazuri na mabaya, hao ndio watakaoingia huko, nami nitawapa wao inchi hiyo ikuwe yao.

40 Lakini ninyi, mugeuke na kurudi katika jangwa kuelekea bahari Nyekundu.’

41 “Kisha mukanijibu: ‘Sisi tumemutendea Yawe zambi, lakini sasa tutakwenda na kupigana kama vile Yawe, Mungu wetu alivyotuamuru’. Hivyo, kila mumoja wenu akajitayarisha kupigana vita, maana mulifikiri kwamba lingekuwa jambo jepesi kuishambulia inchi hiyo ya milima.

42 Naye Yawe akaniambia: ‘Uwaambie hao watu wasiende kupigana kwa sababu siko pamoja nao. Wasiende, kusudi wasishindwe na waadui zao’.

43 Basi, mimi nikawaambia hivyo, lakini ninyi hamukusikia. Pahali pake mukakataa kufuata agizo la Yawe. Bila kujali mukaingia katika inchi hiyo ya milima.

44 Hapo, Waamori waliokuwa wanaishi katika eneo hilo la milima wakateremuka kuwashambulia na kama vile nyuki wanavyofanya wakawapiga huko Seiri mpaka Horma.

45 Ndipo muliporudi, mukamulilia Yawe, lakini hakuwasikiliza wala hakuwajali.

46 Basi, mukabaki kule Kadesi kwa muda murefu ambao mulikaa kule.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ