Isaya 52 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu atakomboa Yerusalema 1 Amuka! Amuka! Ujipatie zile nguvu zako, ewe Sayuni! Uvae nguo yako nzuri, ewe Yerusalema, muji mutakatifu. Maana hawataingia tena kwako watu wasiotahiriwa na wachafu. 2 Ujikungute mavumbi, usimame, ewe Yerusalema uliyekuwa mufungwa! Ujifungue minyororo yako katika shingo, ewe binti Sayuni uliyekamatwa mateka. 3 Yawe anasema hivi: Ninyi muliuzishwa bure bila malipo yoyote, na mutakombolewa bila kulipa feza. 4 Tena zamani ninyi watu wangu mulikimbilia Misri mukakaa kule. Halafu nyuma Waasuria waliwagandamiza bila sababu yoyote. 5 Katika hali ya sasa ninapata faida gani kuwaona watu wangu wamepelekwa katika utumwa? –Ni ujumbe wa Yawe. Hao wanaowatawala wanajitapa. Nalo jina langu linaendelea kuzarauliwa kila siku. –Ni ujumbe wa Yawe. 6 Kwa hiyo watu wangu watajua mimi ni nani. Siku hiyo watajua kwamba ni mimi ninayesema: “Niko!” 7 Ni furaha kabisa! Mujumbe anatokea kwenye mulima. Anatangaza habari njema za amani, heri, na ukombozi. Anauambia Sayuni: Mungu wako anatawala! 8 Sikiliza sauti ya walinzi wako; wanaimba pamoja kwa furaha, maana wanaona kwa macho yao wenyewe kurudi kwa Yawe katika Sayuni. 9 Mupige kelele za shangwe, enyi mabomoko ya Yerusalema! Yawe amewafariji watu wake, ameukomboa Yerusalema. 10 Yawe ameonyesha nguvu yake tukufu, mbele ya mataifa yote. Atawaokoa watu wake, na ulimwengu wote utashuhudia. 11 Muondoke! Muondoke! Mutoke pale! Musiguse kitu chochote kichafu! Muondoke kule Babeli! Mujitakase, enyi munaobeba vyombo vya Yawe. 12 Mara hii hamutatoka kwa haraka, wala hamutaondoka mbiombio! Maana Yawe atawatangulia, Mungu wa Israeli atawalinda nyuma yenu. Mutumishi wa Yawe 13 Mungu anasema hivi: Mutumishi wangu atafanikiwa; atatukuzwa na kupewa cheo, atapata heshima kubwa. 14 Wengi waliomwona walishituka, kwa vile sura yake ilikuwa imeharibika; hakukuwa tena na umbo la mwanadamu! 15 Lakini sasa ameyashangaza mataifa mengi. Wafalme watapumbazika kwa sababu yake, maana wataona mambo ambayo hawajapata kuambiwa, na kufahamu mambo ambayo hawajapata kusikia. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo