Isaya 31 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Misri haitaweza kusaidia 1 Ole kwao wale wanaokwenda Misri kuomba musaada! Wanategemea farasi, wanategemea wingi wa magari ya vita na nguvu za waaskari wao wapanda-farasi. Lakini hawamutegemei Mutakatifu wa Israeli, wala hawamwombi Yawe shauri! 2 Mungu ni mwenye hekima na analeta maangamizi. Habadilishi masemi yake; lakini yuko tayari kuwaazibu watu waovu vilevile na wasaidizi wa watenda mabaya. 3 Wamisri ni wanadamu tu wala si miungu; farasi wao nao ni nyama tu, si roho. Yawe akiunyoosha mukono wake, taifa linalotoa musaada litajikwaa, na lile linalosaidiwa litaanguka; yote mawili yataangamia pamoja. Mungu ataulinda Yerusalema 4 Yawe aliniambia hivi: Simba mukali ananguruma kwa kukinga nyama aliyemukamata; hata kundi la wachungaji likiitwa kwa kumufukuza, hatishiki kwa kelele zao, wala hashituki kwa sauti zao. Ni vile Yawe wa majeshi atakavyoshuka kupigana juu ya mulima Sayuni na kilima chake. 5 Kama vile ndege anavyonyoosha mabawa juu ya vitoto vyake, ni vile Yawe atakavyolinda Yerusalema. Ataulinda na kuukomboa, ataukinga na kuuokoa. 6 Enyi Waisraeli, mumurudilie yule muliyemwacha kabisa. 7 Wakati utafika ambapo ninyi wote mutatupilia mbali sanamu zenu za feza na zahabu ambazo mumejitengenezea kwa mikono yenu inayowakosesha. 8 Hapo Waasuria watauawa kwa upanga, lakini si upanga wa watu; wataangamizwa kwa upanga ambao ni zaidi ya ule wa wanadamu. Waasuria watakimbia na vijana wao watatumikishwa kazi za kitumwa. 9 Mufalme wao atatoroka kwa ajili ya hofu, na wakubwa wao wataiacha bendera yao kwa ajili ya woga. –Ni ujumbe wa Yawe ambaye moto wake uko katika Sayuni, ambaye furu lake liko katika Yerusalema. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo