Isaya 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu ataiazibu inchi ya Kushi 1 Ole, kwa inchi iliyojaa muvumo wa mabawa, inchi inayokuwa ngambo ya mito ya Kushi! 2 Inatuma wajumbe ambao wanasafiri ndani ya muto Nili, wamepanda ndani ya mitumbwi iliyotengenezwa na matete. Muende, enyi wajumbe wepesi, kwa taifa kubwa na hodari, la watu warefu wenye ngozi laini, wanaotisha kwa karibu na kwa mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo inchi yake imegawanywa na mito. 3 Enyi wakaaji wote katika ulimwengu, nanyi munaojaza dunia! Bendera itakaposimikwa kwenye mulima, muangalie! Baragumu itakapopigwa, musikilize. 4 Maana, Yawe ameniambia hivi: Tokea juu kwenye makao yangu nitaangalia yanayotukia, nikitulia kama joto katika mwangaza wa jua, kama wingu la umande wakati wa mavuno. 5 Maana, mbele ya mavuno, wakati wa kuchanua umekwisha, maua yameanguka na kuwa zabibu yenye kukomaa, Mungu atakata chipukizi kwa upanga, na kuyakwanyua matawi. 6 Yote yataachiwa ndege wa milima na nyama wengine wa pori. Ndege wakali watakaa humo wakati wa jua, na nyama wa pori watafanya makao humo wakati wa baridi. 7 Wakati huo, Yawe wa majeshi ataletewa sadaka kutoka kwa watu warefu na wenye ngozi laini, watu wanaotisha kwa karibu na kwa mbali, taifa la watu wenye nguvu na ushindi, ambalo inchi yake imegawanywa na mito. Ataletewa sadaka hizo kwenye mulima Sayuni anapoabudiwa yeye Yawe wa majeshi. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo