Hosea 11 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Upendo wa Mungu unapita hasira yake 1 Israeli alipokuwa mutoto, nilimupenda. Kutoka Misri nilimwita mwana wangu. 2 Lakini kadiri nilivyozidi kuwaita, ndivyo walivyozidi kwenda mbali nami; waliendelea kuyatambikia Mabali, na kuvifukizia ubani sanamu za miungu. 3 Mimi ndiye niliyemufundisha watu wa Efuraimu kutembea! Mimi mwenyewe niliwatwaa katika mikono yangu; lakini hawakutambua kwamba mimi ndiye niliyewatunza. 4 Niliwaongoza kwa huruma, nilishikamana nao kwa upendo; kama baba anavyomunyanyua mutoto mpaka kwenye shavu lake, ndivyo nami nilivyokuwa kwao. Mimi niliinama chini na kuwakulisha. 5 Basi, watarudi katika inchi ya Misri; watatawaliwa na mufalme wa Asuria, kwa sababu wamekataa kunirudilia. 6 Upanga utavuma katika miji yao, utavunjavunja miimo ya milango yake na kuwaangamiza katika kuta zao. 7 Watu wangu wamekusudia kuniacha mimi, wakiitwa kusimama wapande juu, hakuna hata mumoja anayeweza. 8 Ewe Efuraimu, ninaweza kukuacha namna gani? Ninaweza kukutupilia, ewe Israeli namna gani? Nitaweza namna gani kukufanya kama muji wa Adama? Nitaweza namna gani kukutendea kama Zeboimu! Ninazuizwa na moyo wangu; huruma yangu imezidi kuwa motomoto. 9 Nitaizuia hasira yangu kali; sitamwangamiza tena Efuraimu, maana mimi ni Mungu, wala si mwanadamu. Mimi ndimi Mutakatifu kati yenu, nami sitakuja kuwaangamiza. 10 Watanifuata mimi Yawe ninayenguruma kama simba; nitakaponguruma watanifikia toka magaribi wakitetemeka. 11 Watakuja kutoka Misri wakitetemeka kama ndege, wataruka kutoka Asuria kama njiwa nami nitawarudisha kwao. –Ni ujumbe wa Yawe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo