Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Hesabu 4 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Kazi ya Wakohati

1 Yawe akamwambia Musa na Haruni:

2 Uhesabu watu wa ukoo wa Kohati, toka katika ukoo za Lawi, kufuatana na jamaa zao na ukoo zao;

3 utahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano wanaofaa kujiunga na kazi ya hema la mukutano.

4 Hii ndiyo itakayokuwa kazi ya wana wa Kohati, kuelekea vitu vitakatifu kabisa.

5 Wakati wa kuvunja kambi, Haruni na wana wake wataingia katika hema, na kushusha pazia linalokuwa mbele ya Sanduku la Agano, kisha walifunike kwa pazia hilo.

6 Juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi, kisha watatandaza juu yake kitambaa cha rangi ya samawi tupu. Halafu wataingiza miti ya kulibebea sanduku hilo.

7 Juu ya meza ya kutolea mikate inayowekwa mbele ya Yawe watatandaza kitambaa cha rangi ya samawi na juu yake wataweka sahani, visahani vya ubani, bakuli na bilauri, kwa ajili ya kutolea sadaka za kinywaji. Siku zote kutakuwa mukate juu ya meza.

8 Kisha, watavifunika vyombo hivi vyote kwa kitambaa chekundu, na juu yake wataweka kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza miti yake ya kulibebea.

9 Watatwaa kitambaa cha rangi ya samawi ambacho watafunikia kinara cha taa na taa zake, makasi zake, sinia zake na vyombo vyote vinavyotumiwa kukiwekea mafuta.

10 Watakiweka pamoja na vyombo vyake vyote ndani ya ngozi laini ya mbuzi na kukiweka juu ya miti ya kubebea.

11 Halafu watatandaza kitambaa cha rangi ya samawi juu ya mazabahu ya zahabu na kuifunika kwa ngozi laini ya mbuzi. Halafu wataingiza miti yake ya kuibebea.

12 Watatwaa vyombo vyote vinavyotumika katika Pahali Patakatifu, watavifunga kwa kitambaa cha rangi ya samawi na kuvifunika kwa ngozi laini ya mbuzi, kisha wataviweka juu ya miti yake ya kubebea.

13 Wataondoa majivu juu ya mazabahu na juu yake watatandaza kitambaa cha rangi ya zambarau.

14 Juu yake wataweka vyombo vyote vinavyotumika katika ibada kwenye mazabahu: vyetezo, makanya, miiko na mabakuli. Kisha, juu yake watatandaza kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi na kuiingiza miti yake ya kulibebea.

15 Kisha Haruni na wana wake kufunika Pahali Patakatifu pamoja na vyombo na vifaa vyake vyote, wakiwa tayari kuanza safari, watu wa ukoo wa Kohati watakuja na kuvibeba. Lakini wao, hawaruhusiwi kabisa kugusa vyombo hivyo vitakatifu, kusudi wasikufe. Hiyo ndiyo kazi ya ukoo wa Kohati kila wakati hema la mukutano linapohamishwa.

16 Eleazari mwana wa kuhani Haruni atatunza mafuta ya taa, ubani wa kufukiza, sadaka za vyakula za kila siku, mafuta ya kupakaa kwa kutakasa na kila kitu kilichotakaswa katika hema hilo.

17 Kisha Yawe akawaambia Musa na Haruni:

18 Musiache ukoo wa jamaa za Kohati kati ya Walawi uangamizwe.

19 Basi, kwa kuwaepusha wasipate kuuawa kwa kukaribia vyombo hivyo vitakatifu sana utafanya hivi: Haruni na wana wake wataingia na kumupangia kila mumoja wao mapaswa yake na kazi yake.

20 Lakini wazao wa Kohati hawataingia kwa kutazama vitu hivyo vitakatifu sana wakifanya hivyo watakufa.


Kazi za Walawi wa ukoo wa Wagersoni

21 Yawe akamwambia Musa:

22 Uhesabu watu wa ukoo wa Gersoni kufuatana na jamaa na ukoo zao;

23 utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano wanaofaa kujiunga na kazi ya hema la mukutano.

24 Utumishi wao utakuwa huu:

25 watabeba mapazia ya hema takatifu na hema la mukutano pamoja na kifuniko chake, kifuniko cha ngozi laini ya mbuzi kinachokuwa juu yake, pazia la mulango,

26 mapazia na kamba za upango unaokuwa kandokando ya hema na mazabahu, mapazia ya mulango wa kiwanja, na vifaa vyote vinavyotumika pamoja na vitu hivi. Wao watashugulika na mambo yote yanayoelekea vitu hivi.

27 Haruni na wana wake makuhani ndio watakaoamrisha kazi zote za Wagersoni juu ya vitu watakavyobeba na kazi watakazofanya. Utawapangia vitu vyote vile ambavyo wanapaswa kubeba.

28 Hii ndiyo kazi ya jamaa za Gersoni kwenye hema la mukutano; watafanya kazi chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni.


Kazi za Walawi wa ukoo wa Wamerari

29 Vilevile, utawahesabu wana wa Merari, kufuatana na jamaa zao na ukoo zao.

30 Utawahesabu wanaume wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, wanaofaa kujiunga kwa kazi ya hema la mukutano.

31 Wao watakuwa na kazi ya kubeba mbao, miti, nguzo na misingi ya hema la mukutano.

32 Vilevile watabeba nguzo za upango za kuzunguka pande zote, viikalio, misumari na kamba pamoja na vifaa vyake vyote na vyombo vyake vingine vyote. Nawe utawapangia kufuatana na majina yao vitu watakavyopaswa kubeba.

33 Hii ndiyo itakayokuwa kazi ya wana wa ukoo wa Merari katika utumishi wao wote ndani ya hema la mukutano, chini ya uongozi wa Itamari mwana wa kuhani Haruni.


Hesabu ya Walawi

34 Basi, Musa, Haruni na viongozi wa Waisraeli wakafanya hesabu ya watu wa ukoo wa Kohati, kufuatana na jamaa zao,

35 wakawahesabu watu wote wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, kila mutu aliyefaa kuingia katika kazi ya hema la mukutano.

36 Hesabu yao kufuatana na jamaa zao ilikuwa watu elfu mbili mia saba na makumi tano.

37 Hii ndiyo hesabu ya watu wa jamaa ya Wakohati, ambao walitumika katika hema la mukutano, ambao Musa na Haruni wakawahesabu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa.

38 Hesabu ya watu wa ukoo wa Gersoni kufuatana na jamaa zao,

39 wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, waliofaa kutumika katika hema la mukutano,

40 ilikuwa watu elfu mbili mia sita na makumi tatu.

41 Hii ndiyo iliyokuwa hesabu ya watu wa jamaa za wana wa Gersoni wote waliotumika katika hema la mukutano, ambao Musa na Haruni waliwahesabu kama vile Yawe alivyowaamuru.

42 Hesabu ya watu wa ukoo wa Merari kufuatana na jamaa zao na nyumba zao,

43 wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano waliofaa kutumika katika hema la mukutano,

44 ilikuwa watu elfu tatu na mia mbili.

45 Hii ndiyo hesabu ya watu wa ukoo wa Merari ambao Musa na Haruni waliwahesabu kama vile Yawe alivyomwamuru Musa.

46 Hivyo, Walawi wote waliohesabiwa na Musa, Haruni na viongozi wa watu, kwa kufuata jamaa zao na ukoo zao,

47 wenye umri kati ya miaka makumi tatu na makumi tano, na ambao walifaa kwa kazi na ubebaji katika hema la mukutano,

48 kwa jumla walikuwa watu elfu nane na mia tano na makumi nane.

49 Kila mumoja alipewa kazi yake ya kufanya juu ya kubeba hema la mukutano, kama vile Yawe alivyomwamuru Musa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ