Hesabu 3 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wana wa Haruni 1 Hawa ndio wazao wa Haruni na Musa wakati Yawe alipozungumuza na Musa kwenye mulima Sinai. 2 Haya ndiyo majina ya wana wa Haruni: Nadabu, muzaliwa wake wa kwanza, Abihu, Eleazari na Itamari. 3 Hawa walitakaswa kwa kupakwa mafuta wakuwe makuhani. 4 Lakini Nadabu na Abihu walikufa mbele ya Yawe, wakati walipomutolea Yawe moto usiokuwa mutakatifu katika jangwa la Sinai. Wao hawakukuwa na watoto. Kwa hiyo Eleazari na Itamari wakatumika kama vile makuhani chini ya uongozi wa baba yao Haruni. Walawi wanachaguliwa kwa kutumikia makuhani 5 Yawe akamwambia Musa: 6 Uwalete karibu watu wa kabila la Lawi, uwaweke mbele ya kuhani Haruni wapate kumutumikia. 7 Watafanya kazi kwa pahali pake na pa Waisraeli wote pamoja kwenye hema la mukutano wanapotumika pale. 8 Watatunza vyombo vyote vya hema la mukutano na kuwasaidia Waisraeli wanapofanya kazi zao kwenye hema takatifu. 9 Utamupatia Haruni Walawi na wazao wake makuhani; hao wametolewa kwake kabisa kati ya Waisraeli. 10 Utachagua Haruni na wana wake kusudi waweze kutimiza kazi zao za ukuhani; lakini kama mutu yeyote mwingine akikaribia, atauawa. 11 Yawe akaendelea kumwambia Musa: 12 Sasa nimechagua Walawi kati ya Waisraeli wote, pahali pa kila muzaliwa wa kwanza mwanaume anayefungua tumbo la mama yake katika kila jamaa ya Israeli. Walawi ni wangu, 13 maana kila muzaliwa wa kwanza katika Israeli ni wangu. Wakati nilipowaua wazaliwa wa kwanza wote wa Wamisri nilijitakasia kila muzaliwa wa kwanza katika Israeli; kila muzaliwa wa kwanza wa mwanadamu hata wa nyama; wao watakuwa wangu. Mimi ni Yawe. Kuhesabiwa kwa Walawi 14 Yawe akamwambia Musa katika jangwa la Sinai: 15 Uwahesabu wana wa Walawi wote kulingana na ukoo zao na jamaa zao, kila mwanaume kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi. 16 Basi, Musa akawahesabu kufuatana na neno la Yawe, kama vile alivyomwamuru. 17 Hawa ndio waliokuwa wana wa Lawi: Gersoni, Kohati na Merari. 18 Na haya ndiyo majina ya wana wa Gersoni kwa kufuata jamaa zao: Libuni na Simei. 19 Wana wa Kohati kwa kufuata jamaa zao: Amuramu, Isihari, Hebroni na Uzieli. 20 Wana wa Merari kwa kufuata jamaa zao: Mali na Musi. Hizi zilikuwa jamaa za Walawi kulingana na ukoo zao. 21 Jamaa za Walibuni na Wasimei zilitokana na Gersoni; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wagersoni. 22 Hesabu yao kwa kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia waliokuwa na mwezi mumoja na zaidi ni elfu saba na mia tano. 23 Ilipasa kwa jamaa za Wagersoni kupiga kambi yao upande wa magaribi, nyuma ya hema takatifu 24 naye Eliasafu mwana wa Laeli akiwa mukubwa wa ukoo wa Wagersoni. 25 Kazi ya wana wa Gersoni ilikuwa kutunza hema takatifu, hema pamoja na kifuniko chake, pazia la mulango wa hema la mukutano, 26 mapazia ya upango unaokuwa kati ya hema takatifu na mazabahu, na pazia la mulango wa upango, na kamba zake. Kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa zao. 27 Jamaa za Waamuramu, Waisari, Wahebroni na Wauzieli zilitokana na Kohati; hizi ndizo zilizokuwa jamaa za Wakohati. 28 Kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ilikuwa elfu nane na mia sita, waliotumika katika Pahali Patakatifu. 29 Jamaa za wana wa Kohati watapiga kambi yao upande wa kusini wa hema takatifu, 30 naye Elisafani, akiwa mukubwa wa ukoo huo wa jamaa za Wakohati. 31 Wao walioshugulika na kazi ya kutunza Sanduku la Agano, meza, kinara cha taa, mazabahu, vyombo makuhani wanavyotumia hema takatifu na pazia; kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa zao. 32 Naye Eleazari mwana wa kuhani Haruni aliwekwa kuwa mukubwa wa wakubwa wa Walawi, na musimamizi wa watumishi wote wa Pahali Patakatifu. 33 Jamaa za Wamali na Wamusi zilitokana na Merari; 34 hizi ndizo jamaa za Merari. Hesabu yao kadiri ya hesabu ya wanaume wote kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ilikuwa watu elfu sita na mia mbili. 35 Mukubwa wa ukoo wa jamaa za Merari alikuwa Surieli mwana wa Abihaili; hawa watapiga kambi yao upande wa kaskazini wa hema takatifu. 36 Wao walipewa kazi ya kutunza mbao za hema takatifu, miti yake, nguzo, vitako na vifaa vyote vya kushikilia hema; kazi zote zilizoelekea vitu hivi zilikuwa juu yao. 37 Vielvile walihitajika kutunza nguzo za upango zilizouzunguka na vitako vyake, misumari na kamba zake. 38 Musa na Haruni na wana wao watapiga kambi yao mbele ya hema takatifu upande wa mashariki, ni kusema mbele ya hema la mukutano kuelekea upande linakotokea jua. Kazi yao itakuwa kutumika kwenye Pahali Patakatifu kwa jambo lolote lililohitajika kufanyika kwa ajili ya Waisraeli. Mutu mwingine yeyote aliyesogea karibu alipaswa kuuawa. 39 Hesabu ya Walawi kulingana na jamaa zao, wanaume wote kuanzia watoto wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi ambao Musa na Haruni waliwahesabu kwa amri ya Yawe, ilikuwa watu elfu makumi mbili na mbili. Walawi pahali pa wazaliwa wa kwanza 40 Kisha Yawe akamwambia Musa: Uwahesabu kwa majina wazaliwa wa kwanza wanaume wote wa Waisraeli kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi. 41 Nawe utatenga Walawi kwa ajili yangu mimi Yawe; vilevile utatenga kwa ajili yangu mifugo yote ya Walawi pahali pa wazaliwa wa kwanza wa ngombe za watu wa Israeli. 42 Basi, Musa akawahesabu wazaliwa wa kwanza wote wa watu wa Israeli kama vile Yawe alivyomwamuru. 43 Wote wazaliwa wa kwanza wanaume kadiri ya hesabu ya majina, kuanzia wenye umri wa mwezi mumoja na zaidi, kufuata jinsi walivyohesabiwa, walikuwa elfu makumi mbili na mbili mia mbili makumi saba na tatu. 44 Yawe akamwambia Musa: 45 Sasa, utenge Walawi wote kuwa wangu pahali pa wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli. Vilevile, utenge ngombe wa Walawi wote pahali pa wazaliwa wa kwanza wa ngombe wa Waisraeli. Mimi ni Yawe. 46 Kwa ajili ya malipo ya wazaliwa wa kwanza wanaume wa watu wa Israeli mia mbili makumi saba na watatu, wanaozidi hesabu ya wanaume Walawi, 47 utapokea kwa kila mwanaume feza shekeli tano, kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu, ambayo ni sawa na gera makumi mbili, 48 na feza hizo kwa ajili ya malipo ya hao waliozidi hesabu yao utamupa Haruni na wana wake. 49 Musa akatii, akatwaa feza hizo za malipo ya hao waliozidi hesabu ya waliolipiwa na Walawi; 50 akapokea kutoka wazaliwa wa kwanza wa Waisraeli feza kiasi cha shekeli elfu moja mia tatu makumi sita na tano, kulingana na kipimo cha Pahali Patakatifu, 51 akawapa Haruni na wana wake feza hizo za malipo sawa na neno la Yawe, kama vile alivyomwamuru. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo