Hesabu 21 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ushindi kule Horma 1 Mufalme mumoja Mukanana wa Aradi aliyeishi kule Negebu alipopata habari kwamba Waisraeli walikuwa wanakuja kwa njia ya Atarimu, akakwenda kuwashambulia na kuwateka wamoja kati yao. 2 Hapo, Waisraeli wakamwekea Yawe kiapo wakisema: Kama ukiwatia watu hawa katika mikono yetu, basi tutaangamiza kabisa miji yao. 3 Yawe akasikia ombi lao, akawapa ushindi juu ya Wakanana. Waisraeli wakaangamiza kabisa Wakanana pamoja na miji yao. Kwa hiyo pahali pale pakaitwa Horma, ni kusema “Maangamizi”. Nyoka wa shaba 4 Waisraeli wakafunga safari kutoka mulima Hori, wakapitia njia inayoelekea bahari Nyekundu kusudi wazunguke inchi ya Edomu. Lakini katika njia watu wakavunjika moyo. 5 Basi, wakaanza kumunungunikia Mungu na Musa, wakisema: Kwa nini mumetutoa Misri tukuje tukufie humu katika jangwa? Humu hamuna chakula wala maji; nasi tumechokeshwa na chakula hiki cha bure. 6 Hapo Yawe akatuma nyoka wenye sumu kati ya watu, wakawauma hata Waisraeli wengi wakakufa. 7 Basi, watu wakamwendea Musa, wakamwambia: Tumetenda zambi kwa kumunungunikia Yawe na wewe vilevile. Umwombe Yawe atuondolee nyoka hawa. Kwa hiyo, Musa akawaombea watu. 8 Halafu Yawe akamwambia Musa: Tengeneza nyoka wa shaba, umutundike juu ya muti. Mutu yeyote atakayeumwa na nyoka, akiangalia kwenye nyoka huyo wa shaba, atapona. 9 Basi, Musa akatengeneza nyoka wa shaba, akamutundika juu ya muti. Kila mutu aliyeumwa na nyoka alipomuangalia nyoka huyo wa shaba, alipona. Safari mpaka bonde la Wamoabu 10 Waisraeli wakaendelea na safari yao, wakapiga kambi kule Oboti. 11 Kutoka kule wakasafiri mpaka Iye-Abarimu, katika jangwa upande wa mashariki wa Moabu. 12 Kutoka kule wakasafiri wakapiga kambi yao katika bonde la Zeredi. 13 Kutoka huko wakasafiri, wakapiga kambi upande wa kaskazini wa muto Arnoni, ambao unatiririka kutoka katika inchi ya Waamori na kupitia katika jangwa. Muto Arnoni ulikuwa mupaka kati ya Wamoabu na Waamori. 14 Kwa sababu hiyo, imeandikwa katika kitabu cha vita za Yawe: “Muji wa Wahebu katika inchi ya Sufa, na mabonde ya Arnoni, 15 na muteremuko wa mabonde unaofika mpaka muji wa Ari, na kuelekea kwenye mupaka wa Moabu.” 16 Kutoka huko Waisraeli wakasafiri mpaka Beri; ni kusema kisima ambapo Yawe alimwambia Musa: Uwakusanye watu pamoja, nami nitawapa maji. 17 Hapo Waisraeli wakaimba wimbo huu: Bubujika maji, ee kisima! Muimbe! 18 Kisima kilichochimbwa na wakubwa kilichochimbwa sana na wenye cheo, kwa fimbo zao za utukufu na bakora. Kutoka katika jangwa wakasafiri mpaka Matana, 19 kutoka Matana mpaka Nahalieli, kutoka Nahalieli mpaka Bamoti, 20 na kutoka Bamoti mpaka kwenye bonde linaloingia katika inchi ya Moabu, kwenye kilele cha mulima Pisiga, kinachoelekea chini katika jangwa. Waisraeli wanashinda wafalme Sihoni na Ogi ( Kumb 2.26–3.11 ) 21 Waisraeli wakamupelekea mufalme Sihoni wa Waamori, ujumbe huu: 22 Uturuhusu tupite katika inchi yako; hatutakwenda pembeni na kuingia katika mashamba au katika mashamba ya mizabibu, wala hatutakunywa maji ya visima vyenu; tutapita moja kwa moja katika barabara kubwa ya mufalme mpaka tutakapoondoka katika inchi yako. 23 Lakini Sihoni hakuwaruhusu Waisraeli wapite katika inchi yake. Akawakusanya watu wake, akaenda Yahasa katika jangwa kwa kuwashambulia Waisraeli. 24 Lakini Waisraeli wakamwua kwa makali ya upanga, wakatwaa inchi yake, tangu muto Arnoni mpaka muto Yaboki, mpaka inchi ya Waamoni; nao mupaka wa inchi ya Amoni ulikuwa unalindwa sana. 25 Waisraeli wakaiteka miji hii yote nao wakaishi katika miji ya Waamori katika Hesiboni na vijiji vyake. 26 Hesiboni ulikuwa muji wa Sihoni mufalme wa Waamori, ambaye mbele alikuwa amepigana na mufalme wa Moabu na kuteka inchi yake yote mpaka muto Arnoni. 27 Ndiyo maana washairi wetu wanaimba: Mukuje Hesiboni na kujenga. Muji wa Sihoni ujengwe na kuimarishwa. 28 Maana moto ulitoka Hesiboni, miali ya moto ilitoka katika muji kwa Sihoni, ukauteketeza muji wa Ari wa Moabu, ukaiangamiza milima ya muto Arnoni. 29 Ole wenu watu wa Moabu! Mumeangamizwa, enyi watu wa mungu Kemosi! Umewafanya watoto wenu wanaume kuwa wakimbizi, wabinti zako umewaacha watwaliwe mateka mpaka kwa Sihoni, mufalme wa Amori. 30 Lakini sasa wazao wao wameangamizwa, kutoka Hesiboni mpaka Diboni, kutoka Nasimu mpaka Nofa, karibu na Medeba. 31 Basi, Waisraeli wakakaa katika inchi ya Waamori. 32 Kisha Musa akatuma watu wapeleleze muji wa Yazeri; wakauteka pamoja na vijiji vyake, wakawafukuza Waamori waliokaa humo. 33 Waisraeli wakageuka wakafuata njia inayoenda Basani. Mufalme Ogi wa Basani akatoka na jeshi lake kwa kuwashambulia huko Edirei. 34 Lakini Yawe akamwambia Musa: Usimwogope, maana nimemutia katika mikono yako pamoja na watu wake wote na inchi yake yote. Utamutendea kama ulivyomutendea Sihoni, mufalme wa Waamori, aliyekuwa anakaa Hesiboni. 35 Basi, Waisraeli wakamwua Ogi, wana wake na watu wake wote, bila kumwacha hata mutu mumoja, kisha wakatwaa inchi yake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo