Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Hesabu 18 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002

1 Basi, Yawe akamwambia Haruni: Wewe na wana wako na ukoo wako mutabeba lazima ya kazi za hema takatifu; vilevile na makosa yanayoambatana na ukuhani wako wewe mwenyewe na wana wako.

2 Wewe, wana wako na wazao wako wote mutatumika kama vile makuhani; wandugu zako wengine wa kabila lako watafanya kazi pamoja nawe mbele ya hema la kuchunga vibao vya agano.

3 Wao watafanya kazi utakazowapa na kutimiza mapaswa yao juu ya hema. Lakini hawana ruhusa ya kugusa vyombo vya hema, wala kukaribia mazabahu, kusudi wasikufe, nawe vilevile usikufe.

4 Wao watajiunga nawe katika kazi na kutimiza mapaswa yao kwa ukamilifu juu ya kazi zote za hema, wala kusikuwe mutu mwingine atakayekukaribia mule.

5 Ninyi mutafanya kazi za Pahali Patakatifu na mazabahu, kusudi kasirani yangu isiwatokee tena Waisraeli.

6 Ni mimi niliyewachagua wandugu zenu Walawi kati ya Waisraeli kama vile toleo kwenu. Wao wametengwa kwa ajili yangu mimi Yawe, kusudi wafanye kazi katika hema la mukutano.

7 Lakini wewe peke yako na wana wako mutafanya kazi zote za kikuhani kwa ajili ya mazabahu na vyote vinavyokuwa ndani ya pazia. Hayo ni mapaswa yenu, kwa sababu ninawapa zawadi ya ukuhani. Mutu yeyote asiyestahili atakayekaribia vyombo vya hema, atauawa.


Fungu la makuhani

8 Yawe akamwambia Haruni: Ninakupatia matoleo Waisraeli waliyonipa, vitu vyote vitakatifu walivyonipa: vitu vyote vilivyotakaswa na Waisraeli. Ninakupa vitu vyote wewe na wazao wako kuwa fungu lenu, na hiyo ni haki yenu milele.

9 Kati ya vitu vitakatifu kabisa ambavyo haviteketezwi kwa moto, hivi vitakuwa vyenu: sadaka za vyakula, sadaka kwa ajili ya zambi na sadaka za kosa. Kila kitu watu watakachonitolea kama vile sadaka takatifu kitakuwa chako na wana wako.

10 Mutavikula vitu hivyo kama vitu vitakatifu kabisa, na ni wanaume tu ndio watakaovikula; vitu hivyo ni vitakatifu kwenu.

11 Vilevile, vitu vingine vyote Waisraeli watakavyonitolea kama vile sadaka za kutikiswa, vitakuwa vyako. Ninakupa wewe, wana wako na wabinti zako kuwa haki yenu milele. Mutu yeyote katika jamaa yako asiyekuwa muchafu anaweza kula vitu hivyo.

12 Ninakupa vitu vyote vizuri vinavyotokana na malimbuko ambayo Waisraeli wananitolea: mafuta safi, divai na ngano.

13 Mazao yote ya kwanza ya matunda mabichi ya mashamba yao ambayo wataniletea mimi, yatakuwa yako. Kila mutu asiyekuwa muchafu katika jamaa yako anaweza kula.

14 Kila kitu kilichotakaswa katika inchi ya Israeli kitakuwa chenu.

15 Kila muzaliwa wa kwanza ambaye Waisraeli watanitolea, akiwa muzaliwa wa kwanza wa wanadamu, au wa nyama, atakuwa wako. Lakini unaweza kuwakomboa wazaliwa wa kwanza wote wa wanadamu, na kila muzaliwa wa kwanza wa nyama anayekuwa muchafu.

16 Wazaliwa hao wa kwanza watakombolewa wakiwa wenye umri wa mwezi mumoja kwa kulipiwa feza shekeli tano, kulingana na vipimo vya hema takatifu.

17 Lakini wazaliwa wa kwanza wa ngombe, kondoo au mbuzi wasikombolewe; hao ni watakatifu. Damu yao utainyunyizia mazabahu na mafuta yao utayateketeza kuwa sadaka ya kuteketezwa ambayo ni harufu nzuri inayonipendeza mimi Yawe.

18 Nyama yao unaweza kuikula, kama vile kilali na muguu wa nyuma wa kuume vinavyotolewa kama vile sadaka ya kutikiswa.

19 Ninakupa wewe, wana wako na wabinti zako, vitu vyote ambavyo watu wa Israeli wananitolea; hivyo ni haki yenu siku zote. Hili ni agano la milele mbele yangu ambalo ni kwa ajili yako na wazao wako.

20 Yawe akamwambia Haruni: Wewe hautakuwa na urizi wowote katika inchi yao, wala kuwa na fungu lako kati yao; mimi ni fungu lako na urizi wako kati ya Waisraeli.


Fungu la Walawi

21 Kuelekea Walawi, hao nimewapa sehemu ya kumi ya kila kitu Waisraeli wanachonitolea kuwa urizi wao. Haya yatakuwa malipo yao kwa kazi wanayotoa katika kulitunza hema la mukutano.

22 Na tangu sasa, watu wengine wa Israeli wasikaribie hema la mukutano kusudi wasitende zambi na kujiletea kifo.

23 Lakini Walawi peke yao ndio watakaotumika katika hema la mukutano; na kuwa na mapaswa kwa ukamilifu juu yake. Hili ni sharti la kufuata siku zote katika vizazi vyenu vyote. Walawi hawatakuwa na mali ya kurizi katika inchi ya Israeli,

24 kwa sababu sehemu ya kumi Waisraeli wanayonitolea nimewapa kuwa urizi wao. Ndiyo maana nimesema kwamba wao hawatakuwa na urizi kati ya Waisraeli.


Zaka ya Walawi

25 Kisha, Yawe akamwambia Musa:

26 Tena utawaambia Walawi maagizo haya: Wakati mutakapopokea sehemu ya kumi ambayo Yawe amewapa kutoka kwa Waisraeli ikuwe urizi wenu, mutanitolea mimi Yawe sehemu moja ya kumi ya vitu hivyo.

27 Sadaka hii yenu itakubaliwa kuwa kama malimbuko ya ngano au kama zabibu mulimaji anazonitolea.

28 Basi, ndivyo, mutakavyonitolea mimi Yawe sadaka ya sehemu ya kumi mutakazopokea kutoka kwa Waisraeli. Sehemu hiyo ya kumi mutakayonitolea mimi Yawe mutamupa kuhani Haruni.

29 Kutokana na matoleo yote mutakayopokea, mutamutolea Yawe sehemu inayokuwa bora kuliko zote na takatifu.

30 Kwa hiyo utawaambia: Mukisha kunitolea sehemu bora kuliko zote, sehemu itakayobakia itakuwa yenu, kama vile inavyokuwa kwa mulimaji anatwaa kinachobakia kisha kutoa sadaka zake za mazao ya kwanza ya ngano na zabibu.

31 Nanyi mutakula kilichotolewa mukiwa pahali popote pamoja na jamaa zenu maana ni mushahara wenu kwa sababu ya kazi yenu katika hema la mukutano.

32 Hamutakuwa na kosa lolote mukikula vitu hivyo, ikiwa kama mumemutolea Yawe sehemu bora kuliko zote, nanyi hamutachafua vitu vitakatifu vya Waisraeli na kufa.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ