Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

Hesabu 17 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Vyetezo

1 Nyuma ya hayo, Yawe akamwambia Musa:

2 Umwambie Eleazari mwana wa kuhani Haruni atoe hivyo vyetezo kwenye moto, atupe mbali moto unaokuwa ndani, maana vyetezo hivyo ni vitakatifu.

3 Vimekuwa vitakatifu kwa sababu watu hawa walivileta kwenye mazabahu ya Yawe. Basi, utwae vyetezo vya watu hao waliouawa kwa sababu ya zambi zao, vifuliwe kuwa vyembamba kusudi vikuwe kifuniko cha mazabahu. Hili litakuwa onyo kwa Waisraeli wote.

4 Basi, kuhani Eleazari akatwaa vyetezo hivyo vya shaba ambavyo vililetwa mbele ya Yawe na wale watu walioteketezwa vikafuliwa kuwa kifuniko cha mazabahu.

5 Hili lilikuwa onyo kwa Waisraeli kwamba mutu yeyote ambaye si kuhani, maana yake asiyekuwa wa ukoo wa Haruni asiende kwenye mazabahu kwa kumufukizia Yawe ubani. Kama sivyo ataangamizwa kama Kora na wafuasi wake. Haya yote yalitendeka kama vile Yawe alivyomwambia Eleazari kwa njia ya Musa.


Haruni anaokoa watu

6 Kesho yake, Waisraeli wote pamoja wakamunungunikia Musa na Haruni wakisema: Mumewaua watu wa Yawe.

7 Walipokusanyika mbele ya Musa na Haruni kwa kutoa malalamiko yao, wakageuka kuelekea hema la mukutano, wakaona kwamba wingu limeifunika hema na utukufu wa Yawe ulikuwa umetokea pale.

8 Musa na Haruni wakakwenda, wakasimama mbele ya hema la mukutano,

9 na Yawe akamwambia Musa:

10 Ujitenge na watu hawa, niwaangamize mara moja! Lakini wao wakajitupa uso mpaka chini.

11 Musa akamwambia Haruni: Twaa chetezo chako, utie moto ndani yake na kukiweka kando ya mazabahu, kisha utie ubani halafu uende nacho haraka kwa watu na kuwafanyia upatanisho. Fanya haraka! Kasirani ya Yawe imekwisha kuwafikia na pigo limeanza kuwashambulia.

12 Basi, Haruni akafanya kama vile alivyoambiwa na Musa. Akatwaa chetezo chake na kukimbia mpaka katikati ya watu waliokuwa wamekusanyika pamoja. Alipoona kwamba pigo limekwisha kuanza, akatia ubani katika chetezo na kuwafanyia watu upatanisho.

13 Alipofanya hivyo, pigo hilo likakoma, naye akabaki katikati ya waliokufa na waliokuwa wazima.

14 Hesabu ya watu waliokufa kwa pigo ilikuwa elfu kumi na ine mia saba, bila kuhesabu wale waliokufa kutokana na uasi wa Kora.

15 Pigo lilipokoma, Haruni akarudi kwa Musa kwenye mulango wa hema la mukutano.


Fimbo ya Haruni

16 Kisha Yawe akamwambia Musa:

17 Uwaambie Waisraeli wakuletee fimbo kumi na mbili, kila kiongozi wa kabila fimbo moja. Uandike jina la kila mumoja wao kwenye fimbo yake,

18 na jina la Haruni uliandike juu ya fimbo inayosimamia kabila la Lawi. Kutakuwa fimbo moja kwa kila kiongozi wa kabila.

19 Upeleke fimbo hizo katika hema la mukutano na kuziweka mbele ya Sanduku la Agano, pahali ambapo mimi ninakutana nawe.

20 Fimbo ya mutu nitakayemuchagua itachipuka. Kwa njia hii nitakomesha manunguniko ya Waisraeli juu yenu.

21 Musa akaongea na watu wa Israeli. Viongozi wao wote wakamupa kila mumoja fimbo yake kulingana na kabila lake kwa jumla zikakuwa fimbo kumi na mbili. Fimbo ya Haruni ikawekwa pamoja na fimbo hizo.

22 Musa akaziweka fimbo hizo zote mbele ya Yawe katika hema la mukutano.

23 Kesho yake asubui, Musa akakwenda katika hema la mukutano. Mule, akakuta fimbo ya Haruni wa kabila la Lawi, imechipuka na kutoa vifundo vilivyochanua maua na kuzaa matunda mabichi ya lozi.

24 Kisha Musa akatoa fimbo zote hapo mbele ya Yawe, akawaonyesha Waisraeli wote, na kila kiongozi akatwaa fimbo yake.

25 Yawe akamwambia Musa: Urudishe fimbo ya Haruni mbele ya Sanduku la Agano. Hiyo itatunzwa pahali pale, na ni onyo kwa waasi hao kwamba wasipoacha kuninungunikia, watakufa.

26 Musa akafanya kama vile alivyoamriwa na Yawe.

27 Waisraeli wakamwambia Musa: Angalia sasa! Tunaangamia! Tumekwisha! Wote tumekwisha.

28 Kila mutu atakayekaribia hema la Yawe atakufa. Tutaangamia sisi wote?

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ