Hesabu 16 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Uasi wa Kora, Datani na Abiramu 1 Kisha Kora mwana wa Isihari mwana wa Kohati mwana wa Lawi, akatwaa watu pamoja na watu watatu wa ukoo wa Rubeni: Datani na Abiramu, wana wa Eliabu, na Oni mwana wa Peleti. 2 Hao wote waliungwa mukono na viongozi wenye heshima mia mbili makumi tano waliochaguliwa na Waisraeli, wakamwasi Musa. 3 Wakakusanyika mbele ya Musa na Haruni, wakawaambia: Ninyi mumepitisha kipimo! Waisraeli wote pamoja ni watakatifu; kila mumoja ni mutakatifu. Yawe yuko pamoja nasi wote. Mbona sasa ninyi munajifanya wakubwa kushinda watu wengine wa Yawe? 4 Musa aliposikia hayo, akajitupa uso mpaka chini. 5 Kisha akamwambia Kora na wafuasi wake: Kesho asubui, Yawe ataonyesha ni nani anayekuwa wake na ni nani anayekuwa mutakatifu, na yule atakayemuchagua, atamuwezesha kukaribia kwenye mazabahu. 6 Basi, mufanye hivi: asubui, wewe pamoja na wafuasi wako, mutatwaa vyetezo, 7 muweke makaa ya moto ndani na kutia ubani juu yake, kisha mutavipeleka mbele ya Yawe. Halafu tutaona ni nani aliyechaguliwa na Yawe. Ninyi Walawi mumepitisha kipimo! 8 Musa akaendelea kumwambia Kora: Musikilize, enyi Walawi! 9 Munaona ni jambo dogo kwenu kwamba Mungu wa Israeli amewachagua ninyi kati ya Waisraeli wote, kusudi muweze kumukaribia na kutumika katika hema la Yawe na kushugulika na kutumikia Waisraeli wote? 10 Amewapatia heshima ya kuwa karibu naye, ninyi pamoja na Walawi wenzenu wote. Sasa munataka vilevile kazi ya ukuhani? 11 Si Haruni tu munayemunungunikia, wewe na kundi lako, lakini kwa kweli munamwasi Yawe. 12 Musa akatuma ujumbe kwa Datani na Abiramu wana wa Eliabu kusudi waitwe, lakini wao wakasema: Hatutakuja! 13 Ni jambo dogo kwamba umetutoa Misri, inchi inayotiririka maziwa na asali, kusudi ukuje kutuua humu katika jangwa? Tena, unajifanya mukubwa wetu! 14 Zaidi ya hayo, haukutuleta katika inchi inayotiririka maziwa na asali, wala kutupatia urizi wa mashamba na mashamba ya mizabibu. Unafikiri utawafanya hawa watu kuwa vipofu? Hatutakuja! 15 Musa akakasirika sana, akamwambia Yawe: Usikubali sadaka za watu hawa. Mimi sijatwaa punda wa mutu yeyote, wala sijamuzuru mutu! 16 Musa akamwambia Kora: Kesho usikose kuja pamoja na wafuasi wako mbele ya Yawe. Haruni vilevile atakuwa pale. 17 Kila mumoja wenu atwae chetezo chake, na kutia ubani, kisha atakipeleka mbele ya Yawe; kwa jumla vitakuwa vyetezo mia mbili makumi tano; wewe vilevile na Haruni, kila mumoja atakuwa na chetezo chake. 18 Basi, kila mumoja wao akatwaa chetezo chake, akatia makaa ya moto na ubani, kisha wakaenda na kusimama kwenye mulango wa hema la mukutano, pamoja na Musa na Haruni. 19 Naye Kora akawakusanya watu wote pamoja, wakasimama mbele ya Musa na Haruni ambao walikuwa kwenye mulango wa hema la mukutano. Halafu utukufu wa Yawe ukawatokea watu wote. 20 Hapo Yawe akamwambia Musa na Haruni: 21 Mujitenge na watu hawa, niwaangamize sasa hivi. 22 Lakini Musa na Haruni wakajitupa uso mpaka chini na kusema: Ee Yawe unayekuwa asili ya uzima wa wanadamu wote. Mutu mumoja akikukosea, utakasirikia watu wote pamoja? 23 Yawe akamwambia Musa: 24 Uwaambie watu waondoke karibu na makao ya Kora, Datani na Abiramu. 25 Basi, Musa akaenda kwa Datani na Abiramu, akifuatwa na wazee wa Israeli. 26 Alipofika, akawaambia watu: Tafazali muondoke kwenye hema za watu hawa waovu na musiguse kitu chao chochote, musiangamizwe pamoja nao kwa sababu ya zambi zao zote. 27 Watu wakaondoka kwenye makao ya Kora, Datani na Abiramu. Datani na Abiramu wakatoka katika mahema yao na kusimama kwenye mulango wakiandamana na wake zao na watoto wao wote hata wale wanaonyonya. 28 Hapo Musa akawaambia watu: Hivi ndivyo mutakavyotambua kwamba Yawe ndiye aliyenituma kufanya mambo haya yote, wala siyo kwa mapenzi yangu mwenyewe. 29 Watu hawa wakikufa kifo cha kawaida, au wakipatwa na hasara kama watu wengine, basi mujue kwamba Yawe hakunituma. 30 Lakini Yawe akifanya jambo ambalo halijapata kutendeka, udongo ukifunguka na kuwameza watu hawa pamoja na kila kitu chao, na kwenda kuzimu wakiwa uzima, basi mutajua kwamba watu hawa wamemuzarau Yawe. 31 Mara tu alipomaliza kusema maneno hayo yote, udongo chini ya Datani na Abiramu ikafunuka 32 na kuwameza watu hao, jamaa zao, pamoja na wafuasi wote wa Kora na mali zao zote. 33 Basi, wao, pamoja na vyote vilivyokuwa vyao wakashuka kuzimu wakiwa wangali wazima. Udongo ukawafunika, wote wakatoweka. 34 Waisraeli wote wengine waliokuwa karibu waliposikia vilio vyao wakakimbia wakisema: Tukimbie, kusudi udongo usitumeze na sisi vilevile. 35 Kisha Yawe akashusha moto ukawateketeza wale watu mia mbili makumi tano waliokwenda kufukiza ubani. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo