2 Wafalme 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Elisha akamujibu: “Sikiliza neno la Yawe: Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.” 2 Jemedari mulinzi wa mufalme akamwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Elisha akamujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.” Waaskari wa Aramu wanaondoka 3 Kulikuwa watu wane wenye ugonjwa wa ukoma waliokuwa inje ya milango ya muji wa Samaria ambao walisemezana, wao kwa wao: “Mbona tunakaa hapa tukikufa na njaa? 4 Hakuna maana ya kuingia katika muji kwa sababu kule tutakufa. Kwa hiyo kumbe tuende kwenye kambi ya Waaramu. Kama wakituacha kuishi, tutaishi; kama wakituua, tutakufa tu.” 5 Hivyo, giza lilipoanza kuingia, wakaenda kwa kambi ya Waaramu, lakini walipofika kule, hakukuwa mutu. 6 Maana Yawe alikuwa amewasikilizisha waaskari wa Waaramu sauti kama ya kundi kubwa lililokuwa na magari na farasi. Waaramu wakazani kwamba mufalme wa Israeli amelipa waaskari wa Wahiti na Wamisri kuja kuwashambulia. 7 Basi, katika usiku ule, Waaramu walikimbia wote kwa kuyaokoa maisha yao wakiacha mahema yao, farasi na punda wao, na hata kambi yao jinsi ilivyokuwa. 8 Wale watu wane wenye ukoma walipofika pembeni ya kambi, waliingia ndani ya hema moja, wakakula na kunywa vile walivyopata mule, wakatwaa feza, zahabu na nguo, wakaenda kuzificha. Wakaingia katika hema ingine na kufanya vivyo hivyo. 9 Lakini wakaambiana: “Tunalofanya si sawa! Hii ni habari njema tunayokuwa nayo leo, na ikiwa tutangoja mpaka asubui, bila shaka tutaazibiwa. Tuende mara moja tuwaambie watu wa nyumba ya mufalme!” 10 Hivyo, wakaondoka katika kambi ya Waaramu na kuwaita walinda milango ya muji na kuwaambia: “Tulikwenda katika kambi ya Waaramu na hatukuweza kumwona wala kumusikia mutu yeyote. Farasi na punda wangali wanafungwa, na mahema yako kama walivyoyaacha.” 11 Walinda milango wakaita mutu mumoja kupasha habari hii katika nyumba ya mufalme. 12 Ingawa kulikuwa bado giza, mufalme aliamuka na kuwaambia wakubwa wa waaskari wake: “Mimi ninajua mupango wa Waaramu! Wanajua tuna njaa katika muji. Sasa wameacha kambi yao kwenda kujificha kusudi tutakapokwenda kutafuta chakula, watukamate wote tungali wazima na kuuteka muji.” 13 Mumoja kati ya wakubwa wake akasema: “Tafazali, utume watu wachache na farasi watano wa wale waliobaki kusudi waende kuona kumetokea nini. Matokeo yao hayatakuwa mabaya zaidi kuliko Waisraeli wote wanaoangamia hapa.” 14 Wakachagua watu na kuwapa magari mawili. Mufalme akawatuma kuwafuata Waaramu, akisema: “Mwende muwaone.” 15 Watu hao wakaenda mpaka Yordani na katika njia waliona nguo na vifaa vingine Waaramu walivyoacha walipokuwa wanakimbia. Wakarudi na kumupasha mufalme habari. 16 Watu wa Samaria wakatoka na kuteka kambi ya Waaramu. Kama vile Yawe alivyosema, kilo tatu za unga bora wa ngano zilinunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza. 17 Naye mufalme alikuwa amemuweka jemadari mulinzi wake kwa kulinda mulango wa muji. Jemadari yule alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa kama vile Elisha mutu wa Mungu alivyotabiri wakati mufalme alipokwenda kumwona. 18 Elisha alikuwa amemwambia mufalme kwamba “Kesho kwa wakati kama huu, humu Samaria kilo tatu za unga bora wa ngano zitanunuliwa kwa kipande kimoja cha feza, na kilo sita za shayiri kwa kipande kimoja cha feza.” 19 Yule jemedari mulinzi wa mufalme alikuwa amemwambia Elisha: “Hata kama Yawe mwenyewe angefanya madirisha mbinguni, jambo hilo litawezekana?” Naye Elisha alikuwa amemujibu: “Utaona kwa macho yako mwenyewe, lakini wewe hautakula.” 20 Na hivi ndivyo ilivyotokea: alikanyagwa na watu palepale kwenye mulango, akakufa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo