Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

2 Samweli 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Unabii wa Natani kwa Daudi
( 1 Sik 17.1-15 )

1 Wakati mufalme Daudi alipokuwa akikaa katika nyumba yake ya kifalme, naye Yawe amemwezesha kuwa na amani na waadui zake kila upande,

2 mufalme Daudi akamwambia nabii Natani: “Angalia, mimi ninakaa katika nyumba iliyojengwa na miti ya mierezi, lakini Sanduku la Mungu linakaa ndani ya hema.”

3 Natani akamwambia mufalme: “Kwenda ufanye chochote unachokifikiri ndani ya moyo wako, kwa maana Yawe yuko pamoja nawe.”

4 Lakini usiku uleule neno la Yawe lilimufikia Natani kusema hivi:

5 “Kwenda umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe anasema hivi: Si wewe utakayenijengea nyumba ya kukaa.

6 Tangu siku ile nilipowatoa Waisraeli katika inchi ya Misri mpaka hivi leo sijaishi kwenye nyumba. Nimetembea kila pahali nikiwa ninakaa katika hema.

7 Kila pahali ambako nimekwenda na Waisraeli wote, sikumwuliza mwamuzi yeyote wa Israeli ambaye nilimwamuru awachunge watu wa Israeli: ‘Kwa nini haujanijengea nyumba ya mierezi?’

8 Kwa hiyo basi, umwambie mutumishi wangu Daudi: Yawe wa majeshi anasema hivi: Nilikutoa katika shamba la malisho ya nyama ulimokuwa unawachunga kondoo, kusudi ukuwe mukubwa wa watu wangu Waisraeli.

9 Tangu wakati ule nimekuwa pamoja nawe kokote ulikokwenda na nimewaangamiza waadui zako wote mbele yako. Nitakufanya kuwa mwenye utukufu kama wakubwa wengine katika dunia.

10 Nami nitawachagulia watu wangu wa Israeli pahali pa kuishi niwapandikize kusudi waishi pahali pao wenyewe, wasisumbuliwe tena. Nao watu wakali hawatawatesa tena kama zamani,

11 wakati nilipowachagua waamuzi juu ya watu wangu Waisraeli. Nami nitakulinda kutokana na waadui zako wote. Zaidi ya hayo, mimi Yawe ninakutangazia kwamba nitakujengea nyumba.

12 “Siku zako zitakapotimia na utakapokufa na kujiunga na babu zako, nitamufanya mumoja wa watoto wako wewe mwenyewe akuwe mufalme, nami nitauimarisha ufalme wake.

13 Yeye ndiye atakayejenga nyumba kwa ajili ya jina langu na kiti chake cha kifalme cha ufalme wake nitakiimarisha milele.

14 Mimi nitakuwa baba yake, naye atakuwa mwana wangu. Akifanya maovu, nitamwazibu kama vile wanadamu wanavyowaazibu watoto wao kwa fimbo.

15 Lakini sitaacha kumutendea mema yangu kama vile nilivyoacha kwa Saulo, niliyemwondoa mbele yako.

16 Ukoo wako na ufalme wako vitadumu imara siku zote. Kiti chako cha kifalme kitakuwa imara milele.”

17 Natani alimwelezea Daudi kila kitu ambacho alionyeshwa katika maono hayo na Mungu.


Maombi ya shukrani ya Daudi
( 1 Sik 17.16-27 )

18 Kisha mufalme Daudi akaingia ndani na kuikaa mbele ya Yawe; halafu akaomba: “Mimi ni nani, ee Bwana wangu Yawe, na jamaa yangu ni nini hata ukaniinua mpaka hapa ninapokuwa leo!

19 Tena jambo hili lilikuwa dogo mbele ya macho yako. Zaidi ya hayo, Bwana wangu Yawe, umeahidi kuchunga jamaa yangu kwa miaka mingi inayokuja na kunijulisha hivyo, ee Bwana wangu Yawe.

20 Nikuambie nini zaidi, mimi Daudi? Maana wewe unanijua mimi mutumishi wako, ee Bwana wangu Yawe!

21 Kutokana na ahadi yako na kulingana na moyo wako, umetenda makubwa hayo yote kusudi unijulishe mimi mutumishi wako.

22 Kutokana na yale tuliyosikia, wewe Yawe ni mukubwa. Hakuna anayekuwa kama wewe, na hakuna Mungu mwingine lakini wewe.

23 Tena, hakuna watu katika dunia ambao wanaweza kufananishwa na watu wako Waisraeli. Ulikwenda kuwakomboa kutoka Misri na miungu yake kusudi wakuwe watu wako. Ukawafanyia jina na kuwatendea mambo makubwa na ya ajabu.

24 Hata umewaimarisha watu wako Waisraeli kwa ajili yako mwenyewe, kusudi wakuwe watu wako milele; nawe ee Yawe umekuwa Mungu wao.

25 Basi, sasa, ee Yawe Mungu, uikamilishe ile ahadi uliyosema juu yangu mimi mutumishi wako na juu ya jamaa yangu.

26 Nalo jina lako litatukuzwa milele, nao watu watasema: ‘Yawe wa majeshi ni Mungu juu ya Israeli!’ Na jamaa yangu, mimi Daudi mutumishi wako, itaimarika mbele yako.

27 Maana wewe, ee Yawe wa majeshi, Mungu wa Israeli, umenifunulia mimi mutumishi wako, ukisema: ‘Nitakujengea nyumba’; ndiyo maana nina uhodari wa kutoa ombi hili mbele yako.

28 Sasa, ee Bwana wangu Yawe, wewe ndiwe Mungu, na maneno yako ni kweli. Umeniahidi mimi mutumishi wako jambo hili jema.

29 Kwa hiyo, ninakuomba nyumba yangu mimi mutumishi wako ipate kudumu milele mbele yako. Wewe umesema. Kwa baraka zako nyumba yangu itabarikiwa milele.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ