Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

2 Petro 1 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Salamu

1 Barua hii inatoka kwangu mimi Simoni Petro, mutumishi na mutume wa Yesu Kristo. Ninawaandikia ninyi mulioshiriki pamoja nasi katika imani ile inayokuwa kubwa kwa njia ya haki ya Mungu wetu na Mwokozi Yesu Kristo.

2 Ninawatakia neema na amani kwa uwingi kufuatana na vile munavyomujua Mungu na Yesu Bwana wetu.


Mwito wa kuchaguliwa na Mungu

3 Kwa uwezo wake, Mungu ametujalia mambo yote tunayohitaji katika maisha yetu kusudi tupate kushikamana na kumwabudu yule aliyetuita kushiriki utukufu wa wema wake mwenyewe.

4 Kufuatana na hayo, ametupatia ahadi nzuri sana na kubwa mupate kuepuka uharibifu unaoletwa na tamaa mbaya za dunia na kushika hali yake ya kimungu.

5 Na kwa sababu hii, mufanye bidii ya kuongeza wema juu ya imani yenu, elimu juu ya wema wenu,

6 ukadirifu juu ya elimu yenu, uvumilivu juu ya ukadirifu, kushikamana na ibada juu ya uvumilivu,

7 undugu juu ya kushikamana na ibada, na upendo juu ya undugu wenu.

8 Kwa maana mukiwa na tabia hizi zote kwa uwingi, zitawawezesha kutumika na kuzaa matunda hata mupate kumujua Bwana wetu Yesu Kristo.

9 Lakini mutu asiyekuwa na tabia hizo ni kipofu, hawezi kuona. Yeye amesahau kwamba amekwisha kutakaswa zambi zake za zamani.

10 Kwa hiyo wandugu zangu, kufuatana na vile mulivyochaguliwa na kuitwa na Mungu, mufanye nguvu zaidi kwa kukamilika katika njia ile. Mukitenda mambo yale hamutaanguka hata kidogo.

11 Maana kwa kufanya vile, mutaruhusiwa kabisa kuingia katika Ufalme wa milele wa Bwana na Mwokozi wetu Yesu Kristo.

12 Kwa sababu hii, nitaendelea kuwakumbusha mambo haya siku zote ingawa mumekwisha kuyafahamu na kukamilika katika ukweli muliopokea.

13 Ninaona kwamba ni vema niwaamushe kwa njia ya kuwakumbusha mambo haya wakati wote wa maisha yangu.

14 Kwa maana ninajua kwamba ninakaribia kuacha mwili huu unaokuwa wa kufa kama vile Bwana wetu Yesu Kristo alivyonionyesha waziwazi.

15 Nitajikaza sana kuwapatia njia ya kuweza kukumbuka mambo haya siku zote kisha kufa kwangu.


Walioshuhudia utukufu wa Kristo

16 Basi, wakati tulipowajulisha uwezo na kurudia kwa Bwana wetu Yesu Kristo, sisi hatukutumia hadisi za uongo zilizotungwa kwa werevu. Lakini tulijionea na macho yetu sisi wenyewe uwezo wake.

17 Maana alipokea heshima na utukufu toka kwa Mungu Baba, wakati sauti yenye utukufu mukubwa toka kwa Mungu ilipomufikia ikisema: “Huyu ni Mwana wangu mupendwa, ninapendezwa naye sana!”

18 Sisi wenyewe tuliisikia sauti ile toka mbinguni tulipokuwa pamoja naye juu ya mulima mutakatifu.

19 Vilevile tunaamini ujumbe uliotangazwa na manabii. Ninyi munafanya vema mukishikamana nao. Ujumbe huo ni kama taa inayoangaza pahali pa giza, mpaka wakati wa mapambazuko na wakati nyota ya asubui itakapoangazia mioyo yenu.

20 Mbele ya yote, mujue kwamba hakuna mutu anayeweza kufasiria yeye mwenyewe unabii unaokuwa katika Maandiko Matakatifu.

21 Maana hakuna hata ujumbe wowote uliotetewa kwa mapenzi ya kimutu, lakini watu walipasha ujumbe wa Mungu wakiongozwa na Roho Mutakatifu.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ