2 Mambo ya Siku 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Safari ya malkia wa Seba ( 1 Fal 10.1-10 ) 1 Malkia wa Seba aliposikia sifa za Solomono, basi akafika Yerusalema kwa kumujaribu Solomono kwa maulizo magumu. Alifika Yerusalema akisindikizwa na watu wengi sana, pamoja na ngamia waliobeba marasi, zahabu nyingi sana na mawe ya bei kali. Na alipofika kwa Solomono, akamwuliza maulizo yote aliyokuwa nayo ndani ya moyo wake. 2 Solomono akajibu maulizo yote, hakukuwa jambo lolote aliloshindwa kumwelezea. 3 Malkia wa Seba alishangaa sana kuona hekima ya Solomono, nyumba aliyokuwa ameijenga, 4 chakula kilichotayarishwa kwenye meza yake, jinsi wakubwa wake walivyokaa kwenye meza, kazi ya watumishi wake na namna walivyovaa, wenye kuleta vinywaji na jinsi walivyovaa, na sadaka za kuteketeza ambazo alitoa katika nyumba ya Yawe. 5 Akamwambia mufalme: “Yote niliyosikia katika inchi yangu juu ya kazi zako na hekima yako ni ya kweli! 6 Lakini sikuweza kuamini habari zao mpaka nilipofika na kujionea mwenyewe, na kumbe niliambiwa nusu tu; hekima yako na fanaka ni zaidi ya yale niliyosikia. 7 Heri kwa wake zako! Heri kwa hawa watumishi wako ambao wanasimama siku zote mbele yako na kusikiliza hekima yako! 8 Na asifiwe Yawe, Mungu wako, ambaye amependezwa nawe, akakuikalisha juu ya kiti chake cha kifalme, ukuwe mufalme kwa jina la Yawe, Mungu wako. Kwa sababu Mungu wako amewapenda Waisraeli na kuwaimarisha milele, amekuweka wewe ukuwe mufalme juu yao kusudi uimarishe uhaki na sheria ya Mungu.” 9 Kisha akamupa mufalme zaidi ya kilo elfu ine za zahabu, na kiasi kikubwa cha marasi na mawe ya bei kali. Aina ya marasi ambayo yule malkia wa Seba alimupatia mufalme Solomono, yalikuwa ya pekee. 10 Vilevile, watumishi wa Hiramu pamoja na watumishi wa Solomono walioleta zahabu kutoka Ofiri, walileta vilevile miti ya musandali na mawe ya bei kali. 11 Solomono alitumia miti hiyo kwa kutengeneza madari ya nyumba ya Yawe na nyumba ya kifalme, na tena kwa kutengeneza vinubi na vinanda vya waimbaji. Mpaka wakati ule miti hiyo ilikuwa haijaonekana katika inchi ya Yuda. 12 Naye mufalme Solomono alimupatia malkia wa Seba kila kitu alichotamani, kitu chochote alichoomba zaidi ya vitu alivyomuletea mufalme. Kisha malkia akaondoka na kurudi katika inchi yake akiwa pamoja na watumishi wake. Utajiri wa mufalme Solomono ( 1 Fal 10.14-25 ) 13 Kila mwaka, Solomono alipelekewa zahabu kadiri ya kilo elfu makumi mbili na mbili, 14 zaidi ya zahabu aliyopokea kutoka kwa wafanya biashara na wachuuzi, tena kutoka kwa wafalme wote wa Arabia na watawala wa inchi ya Israeli. 15 Mufalme Solomono alitengeneza ngao kubwa mia mbili; kila moja ilipakwa kadiri ya kilo saba za zahabu iliyofuliwa. 16 Vilevile alitengeneza ngao ndogondogo mia tatu, kila moja ilipakwa zahabu yapata kilo tatu, halafu mufalme akaziweka katika jengo lililoitwa Nyumba ya Pori la Lebanoni. 17 Tena mufalme alitengeneza kiti cha kifalme kikubwa cha pembe, na akakipakaa zahabu safi. 18 Kiti hicho kilikuwa na ngazi sita na kiti cha kuegemea miguu cha zahabu, vyote hivyo vilikuwa vimeshikamanishwa na kiti hicho cha kifalme; na kila upande kilikuwa na pahali pa kuegemeza mikono tena kilikuwa na sanamu mbili za simba karibu na pahali pale pa kuegemeza mikono. 19 Palikuwa sanamu kumi na mbili za simba waliosimama kwa mwisho wa kila ngazi. Kiti kama hicho kilikuwa bado kutengenezwa katika ufalme wowote. 20 Vikombe vyote vya mufalme Solomono vilikuwa vya zahabu, na vyombo vyote vilivyokuwa katika Nyumba ya Pori ya Lebanoni vilikuwa vya zahabu safi. Feza haikuhesabiwa kuwa kitu cha bei kali katika siku za Solomono. 21 Solomono alikuwa na mashua zilizosafiri mpaka Tarsisi na watumishi wa Hiramu, na kisha kila miaka mitatu, mashua zile zilirudi zikimuletea zahabu, feza, pembe, kima na ndege wanaoitwa tausi. 22 Hivyo basi, mufalme Solomono aliwapita wafalme wote katika dunia kwa mali na kwa hekima. 23 Nao wafalme wa inchi zote walikuwa na hamu ya kumwendea Solomono kwa kusikiliza hekima yake ambayo Mungu alikuwa amemujalia. 24 Kila mumoja wao alimuletea zawadi, vyombo vya feza na vya zahabu, nguo na silaha marasi, farasi na nyumbu. Zawadi hizi alizipokea kila mwaka. 25 Mufalme Solomono akakuwa na vibanda elfu ine vya kuwekea farasi na magari, na waaskari wapanda-farasi elfu kumi na mbili ambao aliwaweka katika miji yenye vituo vya magari ya farasi na kwake katika Yerusalema. 26 Aliwatawala wafalme wote waliokuwa kuanzia muto Furati, mpaka inchi ya Wafilistini na mpaka kwenye mupaka na Misri. 27 Basi Solomono alifanya feza katika Yerusalema kuwa kitu cha kawaida kama mawe katika Yerusalema, na mbao za mierezi zilipatikana kwa wingi kama mikuyu inayokuwa Sefela. 28 Solomono aliletewa farasi walionunuliwa kutoka Misri na katika inchi zingine. Kifupi cha utawala wa Solomono ( 1 Fal 11.41-43 ) 29 Matendo mengine ya Solomono, kutoka mwanzo mpaka mwisho, yameandikwa katika kitabu cha “Historia ya Nabii Natani,” katika “Unabii wa Ahiya wa Shilo,” na katika “Maono ya Ido Mwonaji,” juu ya Yeroboamu mwana wa Nebati. 30 Solomono alitawala inchi yote ya Israeli kwa miaka makumi ine. 31 Kisha Solomono akakufa na kuzikwa katika muji wa baba yake Daudi. Mwana wake Rehoboamu akatawala kwa pahali pake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo