1 Wakorinto 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Wakati mutu mumoja kati yenu anapokuwa na ugomvi na ndugu mwenzake mwamini, atasubutu namna gani kwenda kumushitaki mbele ya waamuzi wapagani pahali pa kumushitaki mbele ya watu wa Mungu? 2 Hamujui kwamba watu wa Mungu ndio watakaohukumu dunia? Na kama ikiwapasa kuhukumu dunia, hamuwezi hata kuhukumu mambo ya burebure? 3 Ninyi hamujui kwamba tutawahukumu wamalaika? Basi, ninyi munaweza kuhukumu zaidi mambo ya maisha haya! 4 Basi ikiwa muna magomvi juu ya mambo ya namna hii, kwa nini munayapeleka mbele ya waamuzi wasiokuwa na madaraka katika kanisa? 5 Ninasema hivi kwa kuwapatisha haya. Hakika kati yenu hakuna hata mutu mumoja mwenye hekima anayeweza kukata maneno kati ya wandugu zake waamini? 6 Lakini sasa ndugu mwamini anamushitaki mwenzake mbele ya waamuzi wasioamini. 7 Kweli mambo haya ya kuwa na mashitaki kati yenu yanahakikisha kwamba mumeshindwa kabisa. Si ingekuwa vizuri zaidi kwenu kuvumilia ubaya? Si ingekuwa vizuri zaidi kunyanganywa mali zenu? 8 Lakini, ni ninyi ndio munaotenda vibaya na kunyanganya mali ya wengine, nao munaowatendea vile ni wandugu zenu waamini. 9 Ninyi munajua hakika kwamba watenda mabaya hawatapata urizi katika Ufalme wa Mungu. Musidanganyike: waasherati, wenye kuabudu sanamu, wazinzi, waasherati wa muke kwa muke na mume kwa mume, 10 wizi, wenye tamaa, walevi, watukanaji, wanyanganyi, watu wale wote hawatapata urizi katika Ufalme wa Mungu. 11 Na wamoja kati yenu walikuwa kama wao. Lakini mumesafishwa toka zambi, mumetakaswa na kuhesabiwa haki mbele ya Mungu kwa jina la Bwana Yesu Kristo na kwa Roho wa Mungu wetu. Miili ya waamini ni viungo vya Kristo 12 Wamoja kati yenu wanasema: “Vitu vyote vinaruhusiwa kwangu.” Ndiyo, lakini vyote si vyenye kufaa kwenu. Ninaweza kusema kwamba vitu vyote vinaruhusiwa kwangu, lakini sitakubali kuwa mutumwa wa kitu chochote. 13 Nanyi munasema vilevile: “Chakula kiliumbwa kwa ajili ya tumbo nayo tumbo kwa ajili ya chakula.” Ndiyo, lakini Mungu ataharibu vyote viwili. Lakini mwili haukuumbwa kwa ajili ya uasherati. Mwili uliumbwa kwa ajili ya Bwana nao ni wake. 14 Mungu aliyemufufua Bwana Yesu atatufufua nasi vilevile kwa uwezo wake. 15 Munajua kwamba miili yenu ni viungo vya mwili wa Kristo. Basi nitatwaa kiungo cha mwili wa Kristo kwa kukifanya kuwa kiungo cha kahaba? Hapana hata kidogo! 16 Au hamujui kwamba mutu yule anayeungana na kahaba amekwisha kuwa mwili mumoja naye? Kwa maana Maandiko Matakatifu yanasema: “Hao wawili watakuwa mwili mumoja.” 17 Lakini anayeungana na Bwana anageuka kuwa mumoja naye kiroho. 18 Muepuke uzinzi! Zambi ingine yoyote mutu anayofanya haigusi mwili wake, lakini yule anayefanya uzinzi anafanya zambi juu ya mwili wake mwenyewe. 19 Hamujui kwamba mwili wenu ni hekalu la Roho Mutakatifu anayekuwa ndani yenu, yule muliyepewa na Mungu? Na ninyi si mali yenu wenyewe. 20 Kwa sababu mulinunuliwa na Mungu kwa bei kali. Basi mutumie miili yenu na roho zenu kwa utukufu wa Mungu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo