1 Samweli 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 20021 Kisha, watu wa Kiriati-Yearimu wakaenda na kulikamata Sanduku la Yawe, wakalipeleka katika nyumba ya Abinadabu, aliyeishi kwenye milima. Wakamutakasa mwana wake aliyeitwa Eleazari kusudi alitunze Sanduku hilo. Samweli anatawala Israeli 2 Tangu Sanduku la Yawe lilipopelekwa katika muji wa Kiriati-Yearimu, kulipita muda murefu, miaka makumi mbili hivi. Wakati huo Waisraeli wote walimulilia Yawe. 3 Samweli akawaambia Waisraeli: “Kama munamurudilia Yawe kwa moyo wenu wote, basi mutupilie mbali miungu ya kigeni na sanamu za Astaroti. Muelekeze mioyo yenu kwa Yawe, na kumutumikia yeye peke yake; naye atawaokoa kutoka katika mikono ya Wafilistini.” 4 Hivyo, Waisraeli wakatupilia mbali sanamu za Mabali na Maastaroti, wakamutumikia Yawe peke yake. 5 Kisha, Samweli akawaita Waisraeli wote wakutane kule Misipa, akawaambia: “Kule nitamwomba Yawe kwa ajili yenu.” 6 Hivyo, Waisraeli wote wakakusanyika kule Misipa. Walichota maji na kuyamimina mbele ya Yawe, wakafunga kula chakula siku ile yote na kusema: “Tumetenda zambi mbele ya Yawe.” Samweli akakuwa mwamuzi wa Waisraeli kule Misipa. 7 Wafilistini waliposikia kwamba Waisraeli wamekusanyika kule Misipa, wakubwa watano wa Wafilistini wakaenda kuwashambulia. Waisraeli waliposikia juu ya jambo lile waliwaogopa Wafilistini. 8 Basi, wakamwambia Samweli: “Usiache kumulilia Yawe, Mungu wetu, kwa ajili yetu. Endelea kumulilia atuokoe kutokana na Wafilistini.” 9 Kwa hiyo Samweli alitwaa mwana-kondoo anayenyonya akamutolea Yawe kama sadaka ya kuteketezwa. Kisha Samweli akamulilia Yawe kwa ajili ya Waisraeli, naye akajibu kilio chake. 10 Samweli alipokuwa anatolea ile sadaka ya kuteketezwa, Wafilistini walikaribia kuwashambulia Waisraeli. Lakini Yawe akatoa sauti kubwa ya ngurumo juu ya Wafilistini, na kuwavuruga Wafilistini, nao wakashindwa mbele ya Waisraeli. 11 Waisraeli walitoka Misipa na kuwafuatilia Wafilistini mpaka karibu na muji wa Beti-kari, wakawaangamiza. 12 Kisha, Samweli alitwaa jiwe na kulisimamisha kati ya Misipa na Seni, akaliita jiwe hilo “jiwe la musaada”, akisema: “Yawe ametusaidia mpaka sasa.” 13 Siku hiyo Wafilistini walishindwa na Yawe aliwazuia Wafilistini kuishambulia inchi ya Israeli wakati wote Samweli alipokuwa anaishi. 14 Miji yote ya Waisraeli ambayo Wafilistini waliiteka kati ya Ekuroni na Gati ilirudishiwa kwa Waisraeli. Waisraeli walikomboa inchi yao kutoka kwa Wafilistini. Tena kulikuwa amani kati ya Waisraeli na Waamori. 15 Samweli alikuwa mwamuzi wa Israeli maisha yake yote. 16 Kila mwaka Samweli alitembelea Beteli, Gilgali na Misipa, na kuwaamulia Waisraeli haki zao katika miji hiyo yote. 17 Kisha, alikuwa akirudi Rama, maana kule ndiko kulikuwa kwake. Aliwaamulia Waisraeli haki zao kule, na kumujengea Yawe mazabahu kule. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo