1 Samweli 31 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kifo cha Saulo na wana wake ( 1 Sik 10.1-12 ) 1 Basi, Wafilistini walipigana vita na Waisraeli; nao Waisraeli walikimbia mbele ya Wafilistini, na kuuawa katika mulima Gilboa. 2 Lakini Wafilistini wakamufuatilia Saulo na wana wake, kisha wakawaua Yonatani, Abinadabu na Malki-Sua, wana wa Saulo. 3 Vita ilikuwa kali sana upande wa Saulo. Wapiga mishale walipomwona wakamwumiza vibaya. 4 Halafu Saulo akamwambia mutu aliyemubebea silaha: “Chomoa upanga wako unichome nikufe, kusudi watu hawa wapagani wasikuje kunichoma upanga na kunichekelea.” Lakini yule aliyemubebea silaha hakusubutu kwa sababu aliogopa sana. Kwa hiyo, Saulo alitwaa upanga wake mwenyewe, na kuuangukia. 5 Halafu yule aliyemubebea silaha aliona kwamba Saulo amekufa, naye vilevile aliuangukia upanga wake, akakufa pamoja na Saulo. 6 Hivi ndivyo Saulo alivyokufa na wana wake watatu, vilevile na mutu aliyemubebea silaha pamoja na watu wake wote katika siku ileile moja. 7 Nao Waisraeli waliokuwa upande wa pili wa bonde, na wengine waliokuwa upande wa mashariki wa muto Yordani walipoona kwamba Waisraeli wamekimbia, naye Saulo na wana wake wamekufa, waliihama miji yao, wakakimbia. Wafilistini wakaenda na kukaa katika miji hiyo. 8 Kesho yake, Wafilistini walipokwenda kutwaa vitu vya wale waliouawa, waliikuta maiti ya Saulo na wana wake kwenye mulima Gilboa. 9 Walikata kichwa cha Saulo na kumuvua silaha zake. Halafu waliwatuma wajumbe katika inchi yao yote ya Filistia kutangaza habari njema katika nyumba ya sanamu zao na kwa watu. 10 Zile silaha zake waliziweka katika nyumba ya Astaroti. Kisha wakautundika mwili wake kwenye ukuta wa muji wa Betisani. 11 Lakini wakaaji wa muji wa Yabeshi-Gileadi waliposikia mambo Wafilistini waliyomutendea Saulo, 12 mashujaa wote waliondoka, wakasafiri usiku kucha, wakaondoa mwili wa Saulo na miili ya wana wake kutoka ukuta wa Betisani, wakakuja nayo mpaka Yabesi na kuiteketeza kwa moto kule. 13 Kisha, wakaitwaa mifupa yao na kuizika chini ya muti wa mukwaju kule Yabesi, nao wakafunga kula chakula kwa muda wa siku saba. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo