Biblia Todo Logo
အွန်လိုင်း သမ္မာကျမ်းစာ

- ကြော်ငြာတွေ -

1 Samweli 27 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Daudi kati ya Wafilistini

1 Daudi akajisemesha ndani ya moyo: “Siku moja, Saulo ataniangamiza. Jambo zuri kwangu ni kukimbilia katika inchi ya Wafilistini. Saulo atakata tamaa kunitafuta ndani ya mipaka ya inchi ya Israeli, nami nitakuwa salama kutoka katika mikono yake.”

2 Kwa hiyo, mara moja Daudi na watu wake mia sita wakaenda kwa Akisi mwana wa Maoki, mufalme wa Gati.

3 Daudi na watu wake pamoja na jamaa yake wakaishi na Akisi kule Gati. Daudi alikuwa na wake wawili: Ahinoamu kutoka Yezereheli na Abigaili mujane wa Nabali kutoka muji wa Karmeli.

4 Saulo aliposikia kwamba Daudi amekimbilia Gati, hakumufuata tena.

5 Siku moja, Daudi akamwambia Akisi: “Kama nimepata kukubaliwa mbele yako, ninakuomba unipe muji mumoja katika inchi yako kusudi ukuwe pahali pangu pa kuishi. Hakuna faida kwangu kuishi nawe katika muji huu wa kifalme.”

6 Siku hiyo, Akisi akamupa muji wa Ziklagi. Kwa hiyo, tangu siku hiyo muji wa Ziklagi ukakuwa mali ya wafalme wa Yuda.

7 Daudi aliishi katika inchi ya Wafilistini kwa muda wa mwaka mumoja na miezi mine.

8 Katika muda huo, Daudi na watu wake waliwashambulia Wagesuri, Wagirzi na Waamaleki, ambao walikuwa wenyeji wa inchi hiyo tangu zamani. Aliwashambulia katika inchi yao mpaka Suri, hata kwa mupaka na Misri.

9 Daudi aliipiga inchi hiyo pasipo kuacha mutu yeyote muzima, akuwe mwanaume au mwanamuke, akateka kondoo, ngombe, punda, ngamia na nguo; kisha akarudi na kufika kwa Akisi.

10 Akisi alipomwuliza: “Leo mashambulizi yako yalikuwa juu ya nani?” Daudi alimwambia: “Juu ya Negebu ya Yuda” au “Juu ya Negebu ya Wayerameli” au “Juu ya Negebu ya Wakeni”.

11 Daudi hakumwacha mutu yeyote muzima akuwe mwanaume au mwanamuke kusudi aletwe Gati; alifikiri ndani ya moyo: “Wanaweza kueleza juu yetu na kusema: ‘Daudi alifanya kitendo hiki na kile.’ ” Hivyo ndivyo Daudi alivyozoea kutenda wakati wote alipoishi katika inchi ya Wafilistini.

12 Kwa hiyo, Akisi alimusadiki Daudi, akifikiri: “Wanainchi wenzake Waisraeli hawamupendi kabisa. Kwa hiyo, atanitumikia maisha yake yote.”

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
ကြှနျုပျတို့နောကျလိုကျပါ:



ကြော်ငြာတွေ