1 Samweli 19 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Saulo anamufuatilia Daudi 1 Saulo alimwelezea mwana wake Yonatani na wakubwa wake juu ya mupango wake wa kumwua Daudi. Lakini Yonatani, mwana wa Saulo, alimupenda sana Daudi. 2 Kwa hiyo, akamwambia: “Baba yangu anakusudia kukuua. Hivyo, ufanye angalisho. Kesho asubui, ujifiche pahali pa siri, ukae pale. 3 Mimi nitakuja na kusimama karibu na baba yangu kule katika shamba pahali utakapokuwa. Pale nitaongea naye juu yako, na kitu chochote nitakachogundua kutoka kwake, nitakuelezea.” 4 Yonatani alimusifu Daudi mbele ya baba yake, akamwambia: “Usitende zambi juu ya mutumishi wako Daudi maana yeye hajatenda zambi yoyote juu yako. Matendo yake yote siku zote yamekuwa mazuri kwako. 5 Alipomwua yule Mufilistini Goliati, alihatarisha maisha yake, naye Yawe aliwapa Waisraeli ushindi mukubwa. Wewe ulipoona jambo lile ulifurahi. Kwa nini unataka kutenda zambi kwa kumwanga damu isiyokuwa na kosa kwa kumwua Daudi bila sababu?” 6 Saulo alimusikiliza Yonatani, kisha akaapa: “Kama vile Yawe anavyoishi, sitamwua Daudi.” 7 Hivyo, Yonatani akamwita Daudi na kumwelezea mambo hayo yote. Yonatani akamupeleka Daudi kwa Saulo, na Daudi akamutumikia Saulo kama hapo zamani. 8 Kisha kulikuwa vita tena kati ya Wafilistini na Waisraeli. Daudi alitoka akapigana na Wafilistini, akawaua Wafilistini wengi na waliobaki wakamukimbia. 9 Halafu, pepo muchafu kutoka kwa Yawe akamushika Saulo alipokuwa akiikaa ndani ya nyumba yake, akishika mukuki katika mukono, wakati Daudi alikuwa akipiga kinubi. 10 Saulo alijaribu kumuchoma Daudi kwa mukuki ule. Lakini Daudi aliepa mukuki wa Saulo na mukuki ukapiga ukuta. Daudi akakimbia na kutoroka. 11 Usiku ule, Saulo akatuma watu kwenye nyumba ya Daudi wamwangalie kama yuko kusudi apate kumwua asubui. Lakini Mikali muke wa Daudi akamwambia Daudi: “Kama hauopoi maisha yako usiku huu, kesho utauawa.” 12 Kwa hiyo Mikali akamutelemusha Daudi kupitia katika dirisha, naye akatoka na kutoroka. 13 Mikali akatwaa sanamu, akailalisha kwenye kitanda na kwenye kichwa chake akaweka kiegemeo cha manyoya ya mbuzi. Kisha akafunika kwa nguo. 14 Saulo alipotuma watu kwa kumukamata Daudi, Mikali akawaambia kwamba Daudi ni mugonjwa. 15 Kisha Saulo akawatuma warudie kule tena, akawaagiza akisema: “Mumulete Daudi kwangu hata akiwa katika kitanda kusudi auawe.” 16 Wale watu walipoingia ndani ya nyumba ya Daudi na kukiangalia kitanda, waliona kuna sanamu na kiegemeo cha manyoya ya mbuzi kwenye kichwa. 17 Halafu Saulo akamwuliza Mikali: “Kwa nini umenidanganya? Umemwacha adui yangu atoroke?” Naye Mikali akamujibu Saulo: “Aliniambia: ‘Uniache niende kusudi nisipate kukuua.’ ” 18 Daudi alipotoroka, alikwenda Rama kwa Samweli. Alimwelezea Samweli mambo yote aliyomufanyia Saulo. Basi, Daudi na Samweli walikwenda na kukaa kule Nayoti. 19 Kisha Saulo aliambiwa kwamba Daudi yuko kule Nayoti katika muji wa Rama. 20 Kwa hiyo Saulo akatuma watu kwenda kumukamata. Lakini walipokuta kundi la manabii likitabiri na Samweli akiliongoza, Roho wa Mungu aliwafikia wale watumishi wa Saulo, nao vilevile wakaanza kutabiri. 21 Saulo alipopata habari zile, alituma watumishi wengine, nao vilevile wakaanza kutabiri. Saulo akatuma watumishi wengine kwa mara ya tatu, nao vilevile wakaanza kutabiri. 22 Kwa hiyo yeye mwenyewe akaenda Rama. Alipofika kwenye kisima kikubwa kinachokuwa kule Seku, akamukuta mutu fulani ambaye alimwuliza: “Samweli na Daudi wako wapi?” Yule mutu akamujibu: “Wako Nayoti, katika muji wa Rama.” 23 Naye Saulo akaenda kule Nayoti katika muji wa Rama. Alipofika kule, Roho wa Mungu akamufikia, naye alianza kutabiri akiwa katika njia mpaka alipofika Nayoti katika muji wa Rama. 24 Alivua nguo zake, akatabiri mbele ya Samweli. Alibaki uchi kwa siku moja, muchana na usiku. Kwa hiyo watu walianza kujiuliza: “Hata Saulo ni mumoja wa manabii?” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo