Namna gani muji uliokuwa mwaminifu sasa umegeuka kuwa kahaba! Wakati mumoja sheria ya Mungu ilifuatwa kabisa, haki ilikaa ndani yake. Sasa, ni muji wa wauaji.
Ninyi munajidai mumefanya agano na kifo mumefanya mapatano na kuzimu! Ninyi munasema kwamba hasara itakapokuja haitawapata, kwa sababu mumefanya uongo kuwa tegemeo lenu, na udanganyifu kuwa kikingio chenu!
Hapana! Mawazo yao yameambatana na hicho ambacho ni majivu tu! Mutu huyo amepotoka hata hawezi kujiokoa mwenyewe na kusema: Kweli, hiki ninachokuwa nacho katika mukono wangu ni udanganyifu mutupu!
Tumekuasi na kukukana, ee Yawe, tumekataa kukufuata, ewe Mungu wetu. Tunasema maneno ya kutesa na uasi, katika mioyo yetu tunatunga na kutoa maneno ya uongo.
Basi, mimi nikasema: Ole kwangu! Mimi nimeangamia, maana, midomo yangu ni michafu, na watu ninaoishi nao ni wenye midomo michafu. Hata hivyo, kwa macho yangu mwenyewe, nimemwona Mufalme, Yawe wa majeshi.
Lakini macho yako wewe na moyo wako, vinaelekea tu mapato yasiyokuwa ya haki. Unamwanga damu ya wasiokuwa na kosa, nawe unawatesa watu na kuwatendea kwa ukali.
Ndimi zao ni hatari kama pinde; wameimarika kwa ajili ya uongo na si kwa ajili ya haki. Wanaendelea kutenda uovu kisha uovu, wala hawanitambui mimi. –Ni ujumbe wa Yawe.–
Ndimi zao ni kama mishale yenye sumu, hawachoki kudanganya; kila mutu anaongea vema na jirani yake, lakini anafanya mipango ya kumushambulia ndani ya moyo wake.
Basi, Bwana wetu Yawe anasema hivi: Kwa kuwa maneno yenu ni udanganyifu na maono yenu ni ya uongo mutupu, basi, mimi nitapingana nanyi. –Ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe!
Kwa hiyo, kama vile ninavyoishi, –ni ujumbe wa Bwana wetu Yawe– kifo kinakungoja na hautaweza kukiepuka. Uko na makosa ya mauaji, basi mauaji nayo yatakuandama.
Naye akaniambia: Uovu wa Waisraeli na watu wa Yuda ni mukubwa sana. Inchi imejaa umwagaji wa damu na katika muji hakuna haki, kwa maana wanasema: Yawe ameiachilia inchi; Yawe haoni.
Hakuna mutu mwaminifu kwa Mungu aliyebaki katika inchi, hakuna mutu yeyote mwenye usawa kati ya watu. Kila mumoja anavizia kumwanga damu; kila mumoja anamwinda mwenzake kusudi amunase.