Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

ZAKARIA 9 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Hukumu juu ya mataifa jirani

1 Ujumbe wa Yawe: Neno la Yawe ni juu ya azabu ya miji Hadiraki na Damasiki. Maana inchi ya Aramu ni mali ya Yawe, kama vile makabila yote ya Israeli yanavyokuwa,

2 vilevile muji wa Hamati unaopakana na Hadiraki, na hata miji ya Tiro na Sidona ingawa inajiona kuwa na hekima sana.

3 Muji wa Tiro umejijengea kuta kubwa, umejilundikia feza kama mavumbi, na zahabu kama takataka katika barabara.

4 Lakini Bwana atatwaa mali yake yote, atautumbukiza utajiri wake katika bahari, na kuuteketeza muji ule kwa moto.

5 Muji wa Askeloni utaona hayo na kuogopa, nao muji wa Gaza utagaagaa kwa uchungu; hata Ekroni, maana tumaini lake litatoweka. Gaza utapoteza mufalme wake, nao Askeloni hautakaliwa na watu.

6 Muji wa Asidodi utakaliwa na wana haramu. Yawe anasema hivi: Nitakikomesha kiburi cha Wafilistini.

7 Nitawakomesha kula nyama yenye damu, na chakula ambacho ni chukizo. Watakaobaki watakuwa mali yangu, kama ukoo mumoja katika Yuda. Watu wa Ekroni watakuwa kama Wayebusi.

8 Mimi mwenyewe nitailinda inchi yangu, nitazuia majeshi yasipitepite ndani. Hakuna mutu atakayewatesa tena watu wangu, maana, kwa macho yangu mwenyewe, nimeona jinsi walivyoteseka.


Mufalme wa amani

9 Mushangilie sana enyi watu wa Sayuni! Mupige vigelegele, enyi watu wa Yerusalema! Angalia, mufalme wenu anawakujia, anakuja kwa shangwe na ushindi! Ni mupole, amepanda juu ya punda, juu ya mwana-punda, mutoto wa punda.

10 Ataondoa kabisa magari ya vita katika inchi ya Efuraimu, na farasi wa vita kutoka katika Yerusalema; pinde za vita zitatupwa mbali. Naye ataleta amani kati ya mataifa; utawala wake utaenea toka bahari mpaka bahari, toka muto Furati hata miisho ya dunia.


Kurudishwa kwa watu wa Mungu

11 Yawe anasema hivi: Kwa sababu ya agano langu pamoja nanyi, agano lililokamilishwa kwa njia ya damu, nitawakomboa wafungwa wenu wanaokuwa kama wamefungwa katika shimo tupu.

12 Enyi wafungwa wenye tumaini, murudi kwenye ukuta wa muji wenu. Sasa mimi ninawatangazia: nitawarudishia mema mara mbili.

13 Yuda nitamutumia kama upinde wangu; Efuraimu nimemufanya mushale wangu. Ee Sayuni, watu wako nitawatumia kama upanga kwa kuwashambulia watu wa Ugriki; watakuwa kama upanga wa shujaa.

14 Yawe atawatokea watu wake; atafyatua mishale yake kama umeme. Bwana wetu Yawe atapiga baragumu; atafika pamoja na upepo mukali wa kusini.

15 Yawe wa majeshi atawalinda watu wake, nao watawaangamiza waadui zao. Watapiga kelele katika vita kama walevi, wataimwanga damu ya waadui zao. Itatiririka kama damu ya nyama wanaotolewa kwa sadaka iliyomiminwa juu ya mazabahu kutoka ndani ya bakuli.

16 Wakati ule, Yawe, Mungu wao, atawaokoa, maana wao ni kundi lake; nao watangaa katika inchi yake kama mawe ya bei kali katika taji.

17 Angalia jinsi gani uzuri na urembo wake unavyokuwa! Vijana wanaume na wanawake watastawi kwa wingi wa ngano na divai mupya.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan