Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

ZAKARIA 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Muji Yerusalema utakuwa tena muji wa amani

1 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: Yawe wa majeshi anasema hivi:

2 Ninachomwa na upendo mukubwa kwa ajili ya Sayuni, na ninawaka kasirani nyingi juu ya waadui zake.

3 Yawe wa majeshi anasema hivi: Nitaurudilia Sayuni na kufanya makao yangu katika Yerusalema. Muji Yerusalema utaitwa “Muji Mwaminifu”, na mulima wa Yawe wa majeshi utaitwa “Mulima Mutakatifu”.

4 Yawe wa majeshi anasema hivi: Wazee, wanaume na wanawake, wataonekana tena wakiikaa kwenye barabara za Yerusalema, kila mumoja na fimbo yake kwa sababu ya kuishi miaka mingi.

5 Barabara za Yerusalema zitajaa vijana wanaume na wanawake, wakichezacheza mule.

6 Yawe wa majeshi anasema hivi: Kwa watu hawa waliobaki, hali hii inaonekana kuwa kitu kisichowezekana; lakini munazani haiwezekani kwangu mimi? –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.

7 Yawe anasema hivi: Nitawaokoa watu wangu kutoka inchi ya mashariki na kutoka inchi ya magaribi

8 na kuwafanya wakae katika Yerusalema. Wao watakuwa watu wangu, nami nitakuwa Mungu wao; nitatawala juu yao kwa uaminifu na haki.

9 Yawe wa majeshi anasema hivi: Mujipe moyo! Sasa munayasikia maneno ambayo mulitangaziwa na manabii wakati musingi wa hekalu langu ulipowekwa kulijenga upya.

10 Mbele ya wakati huo, watu hawakupata mushahara kwa kazi zao wala mali kwa ajili ya kutumikisha nyama. Hamukuwa na usalama kwa sababu ya waadui zenu, maana nilisababisha uadui kati ya watu wote.

11 Lakini sasa sitawatendea hao watu wa taifa hili wanaobaki kama vile zamani. –Ni ujumbe wa Yawe wa majeshi.–

12 Sasa nitaleta tena amani katika dunia, mvua itanyesha kama kawaida, udongo utatoa mazao, na mizabibu itazaa kwa wingi. Nitawapa watu wanaobaki wa taifa hili yale yote yakuwe mali yao.

13 Enyi watu wa Yuda na watu wa Israeli! Wakati uliopita ninyi mulionekana kuwa watu waliolaaniwa kati ya watu wa mataifa. Lakini sasa mimi nitawaokoa, nanyi mutakuwa watu waliobarikiwa. Basi, musiogope tena, lakini mujipe moyo!

14 Yawe wa majeshi anasema hivi: Kama nilivyokusudia kuwatendea ninyi maovu kwa sababu babu zenu walinikasirikisha wala sikuwaonea huruma,

15 vile vile nimekusudia kuutendea wema Yerusalema na watu wa Yuda. Basi, musiogope.

16 Hivi ndivyo munavyopaswa kufanya: Kila mumoja wenu amwambie mwenzake ukweli. Tribinali zenu zitoe siku zote hukumu za haki zinazoleta amani.

17 Mutu yeyote asikusudie kumutendea mwenzake ubaya wala musiape uongo, maana ninayachukia sana matendo hayo. Ni mimi Yawe ninayesema hivyo.

18 Yawe wa majeshi akanitolea mimi Zakaria ujumbe huu:

19 Yawe wa majeshi anasema hivi: Siku za mafungo ya kula chakula ya mwezi wa ine, mwezi wa tano, mwezi wa saba na mwezi wa kumi, zitakuwa nyakati za furaha na shangwe; zitakuwa sikukuu za shangwe kwa watu wa Yuda. Basi, mupende ukweli na amani.

20 Yawe wa majeshi anasema hivi: Watu wengi wa mataifa ya kigeni na wakaaji wa miji mingi watajaa katika Yerusalema.

21 Wakaaji wa muji mumoja watawaendea wakaaji wa muji mwingine na kuwaambia: Tuende pamoja kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka!

22 Kweli, mataifa yenye nguvu na watu wengi watakuja Yerusalema kumwabudu Yawe wa majeshi na kumwomba baraka.

23 Yawe wa majeshi anasema hivi: Wakati ule, watu kumi kutoka mataifa ya kila luga watamukamatilia Muyuda mumoja na kushika nguo yake na kumwambia: Tunataka kwenda pamoja nanyi, kwa sababu tumesikia kwamba Mungu yuko pamoja nanyi.

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan