ZAKARIA 7 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Shauri la kufunga kula chakula 1 Katika mwaka wa ine wa utawala wa mufalme Dario, siku ya ine ya mwezi wa kenda, ni kusema mwezi wa Kisileu, neno la Yawe lilimufikia Zakaria. 2 Watu wa muji wa Beteli walikuwa wamewatuma Sareseri na Regemu-Meleki pamoja na watu wao kumwomba Yawe rehema zake, 3 na kuwauliza makuhani wa hekalu la Yawe wa majeshi maneno haya: Tuendelee kuomboleza na kufunga kula chakula katika mwezi wa tano kama tulivyofanya kwa muda wa miaka mingi sasa? 4 Halafu, neno la Yawe wa majeshi lilinifikia kusema hivi: 5 Uwaambie wakaaji wote wa inchi na makuhani hivi: Kwa muda wa miaka makumi saba iliyopita, ninyi mulikuwa mukifunga na kuomboleza katika mwezi wa tano na wa saba. Munazani mulifunga kwa ajili yangu? 6 Munapokula na kunywa, si munakula na kunywa kwa ajili yenu wenyewe? 7 Haya ndiyo mambo ambayo mimi Yawe niliyowaambia kupitia kwa manabii wa zamani, wakati Yerusalema ulikuwa umestawi na wenye wakaaji tele, na wakati ambapo kulikuwa wakaaji wengi katika miji ya kandokando yake na katika eneo la Negebu na mabonde ya Sefela. 8 Neno la Yawe lilimufikia Zakaria kusema hivi: 9 Yawe wa majeshi anasema hivi: Mutoe hukumu kwa haki, mutende mema na kuwa na huruma ninyi kwa ninyi. 10 Musiwatese wajane, wayatima, wageni au wamasikini; musipange kutendeana mabaya ndani ya mioyo yenu. 11 Lakini watu walikataa kunisikiliza, waligeuza mabega na kuziba masikio yao kusudi wasisikie. 12 Wakaifanya mioyo yao kuwa migumu kama jiwe, wasipate kusikia sheria yangu mimi Yawe wa majeshi niliyoitangaza kwa roho yangu kwa kupitia manabii waliotangulia. Kwa hiyo, mimi Yawe wa majeshi nikawaka hasira juu yao, 13 nikasema: Kwa sababu niliwaita nao hawakunisikiliza, basi, nao waliponiita, sikuwasikiliza. 14 Nami niliwatawanya kwa upepo mukali kati ya mataifa yote ambayo hawakuyajua. Hivyo inchi waliyoiacha ikabaki tupu; hapakuwa mutu yeyote aliyekaa mule; inchi hiyo ya kupendeza ikakuwa ukiwa. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo