ZAKARIA 6 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maono ya nane: Magari ya vita 1 Niliona maono mengine tena. Niliona magari mane ya vita yakitoka katikati ya milima miwili ya shaba nyeusi. 2 Gari la kwanza lilikokotwa na farasi wekundu, la pili lilikokotwa na farasi weusi, 3 la tatu lilikokotwa na farasi weupe, na la ine lilikokotwa na farasi wa kijivujivu. 4 Basi, nikamwuliza yule malaika aliyeongea nami: Bwana, magari haya ya vita yana maana gani? 5 Malaika akanijibu: Magari haya ni upepo kutoka pande ine za mbingu. Yalikuwa mbele ya Yawe wa dunia nzima, na sasa yanaondoka. 6 Lile gari linalokokotwa na farasi weusi linakwenda upande wa kaskazini, lile linalokokotwa na farasi weupe linakwenda upande wa magaribi, na lile linalokokotwa na farasi wa kijivujivu linakwenda upande wa kusini. 7 Farasi hao walipotokea walikuwa na hamu sana ya kwenda kuichunguza dunia. Naye malaika akawaambia: Basi! Muende muichunguze dunia. Basi, wakaenda na kuichunguza dunia. 8 Kisha yule malaika aliyeongea nami akaniambia kwa sauti: Wale farasi waliokwenda katika inchi ya kaskazini wameituliza kasirani ya Yawe. Yoshua anavalishwa taji 9 Neno la Yawe lilinifikia kusema hivi: 10 Pokea zawadi za watu wanaokuwa katika uhamisho zilizoletwa na Heldai, Tobia na Yedaya. Kwenda leo hii katika nyumba ya Yosia mwana wa Zefania ambamo watu hao wamekwenda mbele ya kufika kutoka Babeli. 11 Utatwaa feza na zahabu hiyo, utengeneze taji ambalo utamuvalisha Kuhani Mukubwa Yoshua mwana wa Yosadaki, 12 na kumwambia kwamba Yawe wa majeshi anasema hivi: Hapa kuna mutu anayeitwa Tawi. Yeye atastawi pale anapokuwa na kulijenga hekalu la Yawe. 13 Yeye ndiye atakayelijenga hekalu la Yawe. Atapewa heshima ya kifalme na kuikaa kwenye kiti chake cha kifalme kuwatawala watu wake. Kuhani Mukubwa ataikaa karibu na kiti cha kifalme cha mutawala yule, nao wawili watafanya kazi pamoja kwa amani. 14 Taji hiyo italindwa katika hekalu la Yawe kwa heshima ya Heldai, Tobia, Yedaya na Yosia mwana wa Zefania. 15 Watu wanaokaa katika inchi za mbali watakuja kusaidia kwa kulijenga hekalu langu mimi Yawe. Nanyi mutajua kwamba Yawe wa majeshi, ndiye aliyenituma kwenu. Haya yote yatatukia kama mukiitii sauti ya Yawe, Mungu wenu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo