ZAKARIA 5 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maono ya sita: Kitabu kinachoruka 1 Nilipoangalia tena niliona kitabu kinaruka katika anga. 2 Yule malaika akaniuliza: Unaona nini? Nami nikamujibu: Ninaona kitabu kinaruka katika anga; urefu wake ni metre kenda na upana wake ni metre ine na nusu. 3 Basi, yeye akaniambia: Ndani ya kitabu hicho kumeandikwa laana ambayo inchi nzima itakayoipata. Upande mumoja imeandikwa kwamba wizi wote watafukuzwa katika inchi, na upande mwingine imeandikwa kwamba wote wenye kuapa uongo watafanyiwa vile vile. 4 Yawe wa majeshi anasema kwamba yeye mwenyewe ataipeleka laana hiyo. Itapenya kila nyumba ya mwizi na kila nyumba ya mwenye kuapa uongo kwa kutumia jina lake; itakaa mule na kuteketeza nyumba hiyo yote, mbao na mawe. Maono ya saba: Mwanamuke ndani ya kikapu 5 Yule malaika aliyeongea nami alinikaribia, akaniambia: Inua macho uone kile kinachokuja. 6 Nami nikamwuliza: Ni kitu gani hicho? Naye akanijibu: Hicho ni kikapu chenye makosa ya inchi nzima. 7 Kikapu chenyewe kilikuwa na mufuniko uliotengenezwa kwa chuma cha risasi; kilifunuliwa, nami nikaona mwanamuke ameikaa mule ndani. 8 Yule malaika akaniambia: Mwanamuke yule ni mufano wa uovu! Kisha yule malaika akamusukumia ndani ya kikapu mwanamuke yule na kukifunika. 9 Nilipoangalia, niliona wanawake wawili wanatokea; walikuwa wakirushwa na upepo, nao walikuwa na mabawa yenye nguvu kama ya korongo. Wanawake wale wakakiinua kile kikapu katika anga. 10 Basi, nikamwuliza yule malaika aliyezungumuza nami: Wanakipeleka wapi kile kikapu? 11 Naye akaniambia: Wanakipeleka katika inchi ya Sinari. Kule watakijengea hekalu na litakapokuwa tayari, watakiweka kikapu hicho ndani. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo