Zaburi 97 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu ni mutawala mukubwa 1 Yawe anatawala! Furahi, ee dunia! Mufurahi, enyi visanga vingi! 2 Mawingu na giza nzito vinamuzunguka; haki na sheria ni musingi wa utawala wake. 3 Moto unatangulia mbele yake, na kuwateketeza waadui zake pande zote. 4 Umeme wake unaangaza ulimwengu; dunia inauona na kutetemeka. 5 Milima inayeyuka kama inta mbele ya Yawe, mbele ya Bwana wa dunia yote. 6 Mbingu zinatangaza haki yake; na mataifa yote yanauona utukufu wake. 7 Wote wanaoabudu sanamu na kujisifia miungu ya bure wanafezeheshwa. Miungu yote inainama mbele yake. 8 Watu wa Sayuni wanasikia hayo na kufurahi; watu wa Yuda wanashangilia kwa ajili ya hukumu zako, ee Mungu. 9 Wewe Yawe ni mukubwa juu ya dunia yote; wewe unatukuzwa juu ya miungu yote. 10 Yawe anawapenda wale wanaochukia uovu, anayalinda maisha ya watu wake, anawaokoa kutoka makucha ya waovu. 11 Mwangaza unamwangazia mutu wa haki, nayo furaha ni kwa watu wenye moyo wa usawa. 12 Mufurahi kwa sababu ya Yawe, enyi watu wa haki; mumushukuru kwa ajili ya utakatifu wake. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo