Zaburi 90 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002SEHEMU YA INE (Zaburi 90–106 ) Mungu wa milele na mwanadamu 1 Maombi ya Musa, mutu wa Mungu. Ee Bwana, tangia vizazi vyote, wewe umekuwa usalama wetu. 2 Mbele milima haijakuwa, mbele haujauumba ulimwengu, wewe ndiwe Mungu, milele na milele. 3 Unawarudisha watu katika mavumbi walimotoka, ukisema: “Wanadamu, murudi!” 4 Kwako miaka elfu moja ni kama siku moja tu, ni kama jana ambayo imekwisha pita, ni kama makesha ya usiku mumoja. 5 Unatowesha mbali watu kama ndoto! Wanadamu ni kama majani yanayochipuka asubui: 6 asubui yanachipuka na kuchanua, magaribi yamekwisha nyauka na kukauka. 7 Hasira yako inatuangamiza; tunatishwa na kasirani yako. 8 Maovu yetu umeyaweka mbele yako; zambi zetu za siri ziko wazi mbele yako. 9 Kwa hasira yako maisha yetu yanatoweka, yanaisha kama pumzi. 10 Muda wa maisha yetu ni miaka makumi saba, au tukikuwa wenye afya, miaka makumi nane; lakini yote ni shida na taabu! Siku zinapita mbio, nasi tunatoweka! 11 Nani anayetambua uzito wa hasira yako? Nani anayeona matokeo ya kasirani yako? 12 Utufundishe ufupi wa maisha yetu kusudi tuweze kuwa na hekima. 13 Ee Yawe, urudie! Utakasirika mpaka wakati gani? Utuonee huruma sisi watumishi wako. 14 Utushibishe wema wako kila asubui, tupate kushangilia na kufurahi maisha yetu yote. 15 Utujalie sasa miaka mingi ya furaha, kama ulivyotupa miaka mingi ya shida na taabu. 16 Utuonyeshe matendo yako sisi watumishi wako; uwaonyeshe wazao wetu utukufu wako. 17 Utuonyeshe uzuri wako, ee Bwana, Mungu wetu; uimarishe kazi zetu, uziimarishe. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo