Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Zaburi 89 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wakati wa taabu ya kitaifa

1 Mashairi ya Etani, Mwezra.

2 Ee Yawe, nitayaimba mema yako kwa milele; nitatangaza uaminifu wako kwa vizazi vyote.

3 Nitasema kwamba wema wako unadumu kwa milele, uaminifu wako ni imara kama mbingu.

4 Wewe umesema: “Nimefanya agano na muchaguliwa wangu, nimemwapia mutumishi wangu Daudi hivi:

5 ‘Siku zote nitamuweka mumoja wa wazao wako kuwa mufalme, tena nitaudumisha ufalme wako milele.’ ”

6 Ee Yawe, mbingu zinasifia maajabu yako, uaminifu wako unasifiwa katika kusanyiko la watakatifu.

7 Nani katika mbingu anayeweza kulinganishwa nawe, ee Yawe? Nani anayekuwa sawa nawe kati ya miungu?

8 Wewe unatisha katika baraza la watakatifu; wote wanaokusanyika mbele yako wanakuheshimu na kukuogopa.

9 Ee Yawe, Mungu wa majeshi, ni nani mwenye nguvu kama wewe? Ee Yawe, uaminifu umekuzunguka pande zote.

10 Wewe unaamuru machafuko ya bahari; mawimbi yake yakiinuka, unayatuliza.

11 Ulimuponda nyama mukubwa Rahaba na kumwua; uliwatawanya waadui zako kwa nguvu yako.

12 Mbingu ni zako na dunia ni yako pia; ni wewe uliyeumba ulimwengu na vyote vinavyokuwa ndani yake.

13 Wewe uliumba kaskazini na kusini; milima Tabori na Hermoni inakushangilia.

14 Mukono wako unajaa nguvu, mukono wako una nguvu na umeshinda!

15 Haki na sheria ndio musingi wa utawala wako; wema na uaminifu vinakutangulia!

16 Heri watu wanaojua kukushangilia, wanaoishi katika mwangaza wa wema wako, ee Yawe.

17 Wanafurahi muchana kutwa kwa sababu yako, na kukusifu kwa ajili ya haki yako.

18 Wewe ndiwe utukufu na nguvu yao; kwa upendo wako tunapata ushindi.

19 Ee Yawe, ngao yetu ni chini ya ulinzi wako. Mufalme wetu ametoka kwako, ewe Mutakatifu wa Israeli.


Ahadi ya Mungu kwa Daudi

20 Zamani ulisema katika maono, ukawaambia watumishi wako waaminifu: “Nimemupa nguvu shujaa mumoja, nimemwinua huyo niliyemuchagua kati ya watu.

21 Nimemupata mutumishi wangu Daudi; nimemuchagua kwa kumupakaa mafuta yangu matakatifu.

22 Mukono wangu wa nguvu utakuwa naye siku zote; mukono wangu mimi mwenyewe utamwimarisha.

23 Waadui hawataweza kumushinda, wala waovu hawatamwonea.

24 Mimi nitawaponda wapinzani wake; nitawaangamiza wote wanaomuchukia.

25 Nitakuwa mwaminifu na mwema kwake. Kwa jina langu atapata ushindi mukubwa.

26 Nitaongeza nguvu na utawala wake, kutoka bahari ya Mediteranea mpaka muto Furati.

27 Yeye atasema, ‘Wewe ni baba yangu, Mungu wangu, mulima wa wokovu wangu.’

28 Nami nitamufanya kuwa muzaliwa wangu wa kwanza, mukubwa kuliko wafalme wote wa dunia.

29 Nitamwonyesha wema wangu kwa milele, na agano langu kwake litadumu siku zote.

30 Nitaudumisha ukoo wake wa kifalme siku zote, nao ufalme wake kama mbingu.

31 “Lakini wazao wake wakiiacha sheria yangu, wasipoishi kufuatana na maagizo yangu,

32 kama wakivunja masharti yangu, na kuacha kutii amri zangu,

33 hapo nitayaazibu makosa yao; nitawapiga kwa sababu ya maovu yao.

34 Lakini sitaacha kumutendea mema Daudi, wala sitavunja uaminifu wangu kwake.

35 Sitavunja agano langu naye, wala kugeuza neno nililosema kwa mudomo wangu.

36 “Nimeapa mara moja tu kwa utakatifu wangu; nami sitamwambia Daudi uongo.

37 Ukoo wake utadumu milele, nao ufalme wake kama jua.

38 Utadumu milele kama mwezi unaokuwa mushuhuda mwaminifu asiyetoka katika anga.”


Masikitiko ya sasa

39 Lakini sasa, ee Mungu, umemutupa na kumukataa, umejaa kasirani juu ya huyo uliyemuchagua.

40 Umefuta agano ulilofanya na mutumishi wako; umeitupa taji yake ya kifalme ndani ya mavumbi.

41 Umebomoa kuta zote za muji wake; umezivunjavunja nafasi zake za kukimbilia.

42 Wote wanaopita wanaiba mali zake; wajirani zake wanamuzarau.

43 Umewapatia waadui ushindi; umewafurahisha waadui zake wote.

44 Umepoteza ukali wa silaha zake; ukamwachilia ashindwe katika vita.

45 Umemuvua madaraka yake ya kifalme, ukauangusha utawala wake chini.

46 Umezipunguza siku za ujana wake, ukamufunika haya tele.


Kuomba usalama

47 Ee Yawe, utajificha hata milele? Mpaka wakati gani hasira yako itawaka kama moto?

48 Unikumbuke, ee Bwana. Maisha ni mafupi! Umewaumba wanadamu wote kwa bure?

49 Ni mutu gani anayeweza kuishi pasipo kufa? Nani anayeweza kujiepusha na kifo?

50 Ee Bwana, yako wapi yale mema yako ya zamani uliyomwahidi Daudi kwa uaminifu wako?

51 Ee Bwana, ukumbuke matusi ya mutumishi wako, jinsi ninavyovumilia mazarau ya mataifa.

52 Ee Yawe, ona jinsi wanavyomuzomea muchaguliwa wako. Wanamuzomea kila fasi anapokwenda.

53 Yawe asifiwe milele! Amina! Amina!

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan