Zaburi 86 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Kuomba musaada 1 Maombi ya Daudi. Unitegee sikio, ee Yawe, unijibu, maana mimi ni masikini na mukosefu. 2 Ulinde maisha yangu maana mimi ni mwaminifu mbele yako; uniokoe mimi mutumishi wako ninayekutegemea. 3 Wewe ni Mungu wangu; basi, unionee huruma, maana ninakulilia muchana kutwa. 4 Ee Bwana wetu, ninakutolea moyo wangu. Ufurahishe roho yangu mimi mutumishi wako. 5 Ee Bwana, wewe ni muzuri na mwenye kusamehe, mwingi wa wema kwa wote wanaokuomba. 6 Ee Yawe, utegee maombi yangu sikio; usikilize kilio cha ombi langu. 7 Siku za taabu ninakuita, maana wewe unaniitikia. 8 Ee Bwana, hakuna mungu mwingine anayekuwa kama wewe; hakuna anayeweza kufanya unayofanya wewe. 9 Mataifa yote uliyoumba, yatakuja kukuabudu, ee Bwana; yatatangaza ukubwa wa jina lako. 10 Wewe ndiwe mukubwa, unafanya maajabu; wewe peke yako ndiwe Mungu. 11 Unifundishe njia yako, ee Yawe, nipate kuwa mwaminifu kwako; uongoze moyo wangu nikuheshimu. 12 Ee Bwana, Mungu wangu, nitakusifu kwa moyo wote; nitatangaza ukubwa wa jina lako milele. 13 Wema wako kwangu ni mwingi sana! Umeniokoa kutoka katika kuzimu. 14 Ee Mungu, watu wenye kiburi wamenishambulia; kundi la watu wakali lilitaka kuniua, wala halikujali wewe hata kidogo. 15 Lakini wewe, Bwana, ni Mungu wa rehema na huruma; wewe ni muvumilivu, mwingi wa wema na uaminifu. 16 Unigeukie, unihurumie; unijalie nguvu yako mimi mutumishi wako, umwokoe mutoto wa mujakazi wako. 17 Unionyeshe kitambulisho cha wema wako, ee Yawe, kusudi wale wanaonichukia wafezeheke, wanapoona umenisaidia na kunifariji. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo