Zaburi 81 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Wimbo wa sikukuu 1 Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa watu wa Gati. Zaburi ya Asafu. 2 Mumwimbie Mungu kwa sauti, maana ni nguvu yetu, mumushangilie Mungu wa Yakobo, 3 muvumishe wimbo wa shangwe, mupige ngoma, mucheze zeze na kinubi cha sauti nzuri. 4 Mupige baragumu kutangaza mwandamo wa mwezi, na pia mbalamwezi wakati wa sikukuu yetu. 5 Hilo ndilo sharti katika Israeli; hilo ndilo agizo la Mungu wa Yakobo. 6 Aliwapa watu wa Israeli agizo hilo, aliposhambulia inchi ya Misri. Ninasikia sauti nisiyoitambua ikisema: 7 “Mimi nilikutua mizigo yako toka kwenye mabega, nilikuondolea matofali uliyochukua katika mikono. 8 Katika shida uliniita, nami nikakuokoa. Nilikujibu kutokea katika ngurumo. Nilikujaribu kwenye maji ya Meriba. 9 Enyi watu wangu, musikie onyo langu. Heri ungenisikiliza, ee Israeli! 10 Usikuwe na mungu wa kigeni; usiabudu hata kidogo mungu mwingine. 11 Mimi ni Yawe, Mungu wako, niliyekutoa katika inchi ya Misri. Fungua kinywa chako, nami nitakulisha. 12 “Lakini watu wangu hawakunisikiliza; Israeli hakunitaka kabisa. 13 Hivyo, nikawaacha wabaki katika ugumu; wafuate mashauri yao wenyewe. 14 Heri watu wangu wangenisikiliza! Heri Israeli angefuata njia zangu! 15 Ningewashinda waadui zao haraka; ningenyoosha mukono juu ya wapinzani wao. 16 Wanaonichukia wangenipigia magoti kwa hofu, na azabu yao ingekuwa ya milele. 17 Lakini wewe ningekulisha kwa ngano bora, ningekushibisha kwa asali ya pori.” |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo