Zaburi 80 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maombi kwa ajili ya taifa 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo. Zaburi ya Asafu. 2 Unitegee sikio, ewe Muchungaji wa Israeli, unayewaongoza wazao wa Yosefu kama kondoo. Ewe unayekaa juu ya makerubi, uangaze, 3 mbele ya kabila la Efuraimu, la Benjamina na la Manase. Uonyeshe nguvu yako, ukuje kutuokoa! 4 Utengeneze tena maisha yetu, ee Mungu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. 5 Ee Yawe, Mungu wa majeshi, mpaka wakati gani utakasirikia maombi ya watu wako? 6 Umefanya huzuni ikuwe chakula chetu; umetukunywesha machozi kwa wingi. 7 Umetufanya jambo la mazarau kwa jirani zetu; waadui zetu wanatuchekelea. 8 Ee Mungu wa majeshi, utengeneze tena maisha yetu, utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. 9 Uliongoa muzabibu kutoka Misri; ukawafukuza watu wa mataifa, na kuupandikiza katika inchi yao. 10 Uliupalilia upate kukomaa, nao ukatoa mizizi na kuenea katika inchi yote. 11 Uliifunika milima kwa kivuli chake, na matawi yake yakakuwa kama mierezi mikubwa. 12 Matawi yake yalienea mpaka kwa bahari; navyo vichipukizi vyake mpaka kando ya muto Furati. 13 Mbona ulibomoa kuta zilizouzunguka? Sasa kila anayepita anachuma zabibu zake; 14 nguruwe wa mwitu wanauharibu, na wanyama wa pori wanautafuna! 15 Utugeukie tena, ee Mungu wa majeshi. Uangalie toka mbinguni, uone; uutunze muzabibu huu. 16 Ulinde kijiti ulichokipanda kwa mukono wako; hicho kichipukizi ulichokomalisha wewe mwenyewe. 17 Watu walikikata na kukiteketeza, uwaangalie kwa ukali, waangamie. 18 Mukono wako umukinge huyo uliyemurehemu; huyo uliyemuchagua kwa ajili yako. 19 Hatutakuacha tena; utujalie uzima, nasi tutakusifu. 20 Ee Yawe, Mungu wa majeshi, utengeneze tena maisha yetu; utuangalie kwa wema, nasi tutaokoka. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo