Zaburi 8 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Utukufu wa Mungu na cheo cha mwanadamu 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa watu wa Gati. Zaburi ya Daudi. 2 Ee Yawe, Bwana wetu, jina lako linatukuzwa sana katika dunia yote! Utukufu wako unaenea mpaka juu ya mbingu! 3 Kutoka maneno ya watoto wadogo, hata wachanga, unaimarisha nguvu mbele ya waadui zako na kuwakomesha waasi na wapinzani wako. 4 Nikiangalia mbingu uliyoumba kwa vidole vyako, mwezi na nyota ulizozisimika huko, 5 mutu ni nini, ee Mungu, hata umufikirie? Mwanadamu ni nini hata umujali? 6 Umemufanya kuwa karibu sawa na Mungu, umemujaza utukufu na heshima. 7 Ulimupa utawala juu ya vyote ulivyoviumba; uliweka viumbe vyote chini ya mamlaka yake: 8 kondoo, ngombe, na nyama wa pori, 9 ndege, samaki, na viumbe vyote vya bahari. 10 Ee Yawe, Bwana wetu, jina lako linatukuzwa sana katika dunia yote! |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo