Zaburi 77 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Maombi ya kufarijiwa wakati wa shida 1 Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa Yedutuni. Zaburi ya Asafu. 2 Ninamulilia Mungu kwa sauti. Kwa sauti ninamulilia Mungu, anisikie. 3 Wakati wa taabu ninamutafuta Bwana wetu; ninamunyooshea mikono yangu usiku bila kuchoka, lakini sifarijiwi na mutu yeyote. 4 Ninafikiri juu ya Mungu na kuugua; ninamukumbuka na kufa moyo. 5 Unanizuiza hata kupata usingizi, ninahangaika hata siwezi kusema. 6 Ninafikiri juu ya siku za zamani; ninakumbuka miaka ya hapo kale. 7 Usiku ninawazawaza; moyo wangu unafikiri, nayo roho yangu inajiuliza: 8 “Bwana ametuachilia kabisa? Hatapendezwa tena nasi? 9 Wema wake umekwisha kabisa? Hatatimiza tena ahadi zake? 10 Mungu amesahau kuwa na huruma? Hasira yake imeondoa rehema yake?” 11 Kisha nikasema: “Kinachoniumiza zaidi ni kwamba Mungu Mukubwa hatendi tena kitu kwa ajili yetu!” 12 Nitayakumbuka matendo yako, ee Yawe, nitafikiri juu ya maajabu yako ya hapo kale. 13 Ninafikiri juu ya kazi zako, ninawaza juu ya matendo yako makubwa. 14 Kila unachofanya, ee Mungu, ni kitakatifu. Ni mungu gani anayekuwa mukubwa kama Mungu wetu? 15 Wewe ni Mungu unayetenda maajabu; wewe umeyaonyesha mataifa uwezo wako. 16 Kwa mukono wako wa kuume uliwakomboa watu wako; uliwakomboa wazao wa Yakobo na Yosefu. 17 Maji yalipokuona, ee Mungu, maji yalipokuona, yaliogopa sana; bahari ilitetemeka mpaka chini. 18 Mawingu yalinyesha mvua nyingi, ngurumo zikavuma katika anga, mishale ya umeme ikaangaza kila upande. 19 Kishindo cha ngurumo yako kilitokea katika zoruba, umeme wako ukaangaza ulimwengu, dunia ikatikisika na kutetemeka. 20 Wewe ukajifanyia njia juu ya bahari; ulitembea juu ya maji yale mengi, lakini pahali ulipopita hapakuonekana. 21 Uliwaongoza watu wako kama kondoo, chini ya uongozi wa Musa na Haruni. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo