Zaburi 75 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Mungu ni mwamuzi wa haki 1 Kwa mukubwa wa waimbaji: kwa mutindo wa wimbo “Usiharibu”. Zaburi ya Asafu: wimbo. 2 Tunakushukuru, ee Mungu, tunakushukuru! Tunatangaza ukubwa wa jina lako na kueleza matendo yako makubwa. 3 Mungu anasema: “Mimi nimeweka wakati kamili! Wakati huo nitahukumu kwa haki. 4 Inchi ikitetemeka na vyote vinavyokuwa ndani yake, mimi ndiye ninayeimarisha misingi yake. 5 Ninawaambia wenye kiburi: ‘Mwache kiburi’, na waovu: ‘Musiote mapembe! 6 Musijione kuwa watu wa maana sana, wala kusema maneno ya majivuno.’ ” 7 Ukubwa hautoki mashariki au magaribi, wala hautoki katika jangwa au kwa milima. 8 Mungu mwenyewe ndiye mwamuzi; anamushusha mumoja na kumwinua mwingine. 9 Yawe anashika kikombe katika mukono, kimejaa divai kali ya hasira yake. Anaimimia, nao waovu wote wanaikunywa; wanaikunywa mpaka tone la mwisho. 10 Lakini mimi nitafurahi milele, nitamwimbia Mungu wa Yakobo sifa. 11 Atavunja mapembe yote ya watu waovu; lakini ataotesha mapembe ya watu wa haki. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo