Biblia Todo Logo
Bìoball air-loidhne

- Sanasan -

Zaburi 68 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002


Wimbo wa ushindi

1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Zaburi ya Daudi.

2 Mungu asimame sasa, na waadui zake watawanyike! Wanaomuchukia wakimbie mbali naye!

3 Kama moshi unavyopeperushwa na upepo, ndivyo nao wanavyopeperushwa; kama inta inavyoyeyuka karibu na moto, ndivyo waovu wanavyoangamia mbele ya Mungu!

4 Lakini watu wa haki wanafurahi Mungu anapokuja, wanashangilia na kuimba kwa furaha.

5 Mumwimbie Mungu, musifu jina lake; mumutengenezee njia yeye anayetembea juu ya mawingu. Jina lake ni Yawe; mufurahi mbele yake.

6 Mungu anayekaa pahali pake patakatifu, ni Baba ya wayatima na mulinzi wa wajane.

7 Mungu anawapatia wenye ukiwa jamaa, anawafungua wafungwa na kuwapa uheri. Lakini waasi wataishi katika inchi yenye kukauka.

8 Ee Mungu, ulipowaongoza watu wako, uliposafiri kule katika jangwa,

9 dunia ilitetemeka, mbingu zilitiririsha mvua; mbele yako, Mungu wa Sinai, mbele yako, Mungu wa Israeli!

10 Ee Mungu, ulinyeshea inchi mvua nyingi, ulitia tena inchi yako nguvu ilipokuwa imechakaa.

11 Watu wako wakapata makao ndani yake, uliyotayarishia wamasikini kwa uzuri wako.

12 Bwana alitoa amri, nao wanawake wengi wakatangaza habari:

13 “Wafalme na majeshi yao wanakimbia ovyo!” Wanawake waliobaki ndani ya nyumba waligawanya vitu vilivyonyanganywa,

14 ingawa walibaki ndani ya mazizi: sanamu za njiwa zilizotengenezwa na feza, na mabawa yao yanayoangaa zahabu.

15 Mungu Mukubwa alipowatawanya wafalme, teluji ilianguka juu ya mulima Salmoni.

16 Ewe mulima wa Basani, murefu na wenye vichwa vingi,

17 mbona unauonea kijicho mulima Mungu aliouchagua akae juu yake? Yawe atakaa huko milele!

18 Bwana anakuja kwenye pahali pake patakatifu kutoka Sinai, akikuwa na kundi kubwa, na maelfu na maelfu ya magari ya kukokotwa.

19 Anapanda juu akichukua wafungwa, anapokea zawadi kutoka kwa watu, hata kutoka kwa watu walioasi, Yawe apate kukaa huko.

20 Yawe asifiwe siku kwa siku! Yeye anatubebea mizigo yetu, yeye ndiye Mungu mwokozi wetu.

21 Mungu wetu ni Mungu mwenye kutuokoa; Bwana wetu Yawe pekee ndiye anayeokoa katika kifo.

22 Mungu ataviponda vichwa vya waadui zake, ndivyo vichwa vya wanaoendelea katika njia mbaya.

23 Bwana wetu alisema: “Nitawarudisha waadui kutoka Basani; nitawarudisha kutoka shimo la bahari,

24 usafishe miguu katika damu ya waadui zako, nao imbwa wako wapate posho yao.”

25 Ee Mungu, maandamano yako ya ushindi yanaonekana; maandamano ya Mungu wangu, mufalme wangu, katika pahali patakatifu!

26 Mbele waimbaji, nyuma wanamuziki, katikati wabinti wanavumisha ngoma.

27 “Mumusifu Mungu katika mukutano. Mumusifu Yawe, enyi wazao wa Israeli!”

28 Kwanza ni Benjamina, mudogo wa wote; kisha waongozi wa Yuda na kundi lao, halafu wakubwa wa Zebuluni na Nafutali.

29 Onyesha, ee Mungu, nguvu yako kubwa; nguvu yako uliyotumia kwa ajili yetu.

30 Kutoka katika hekalu lako, Yerusalema, ambapo wafalme watakufikia na zawadi zao,

31 uwakaripie wale nyama wanaokaa katika matete, kundi la mabeberu na ngombe dume, mpaka mataifa hayo yakupe heshima na kodi. Uwatawanye hao watu wenye kupenda vita!

32 Wajumbe watakuja kutoka Misri, Waetiopia watamuletea Mungu mali zao.

33 Enyi falme za dunia, mumwimbie Mungu, mumwimbie Bwana wetu nyimbo za sifa,

34 mumwimbie yeye anayepita katika mbingu, mbingu za tangu zamani. Mumusikilize akinguruma kwa kishindo.

35 Mutambue nguvu za Mungu; yeye anatawala juu ya Israeli, mamlaka yake yanafika katika mbingu.

36 Mungu ni wa kutisha tangia pahali pake patakatifu, yeye ni Mungu wa Israeli! Anawapa watu wake nguvu na uwezo. Mungu asifiwe!

Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.

Bible Society of the Democratic Republic of Congo
Lean sinn:



Sanasan