Zaburi 60 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002Ushindi nyuma ya kushindwa vita 1-2 Kwa mukubwa wa waimbaji. Kwa mutindo wa wimbo “Ushuhuda wa mayungiyungi.” Mashairi ya Daudi ya kufundisha yanayoelekea wakati alipopigana na Wasuria katika Mesopotamia na Zoba naye Yoabu aliporudi nyuma na kuwaua Waedomu elfu kumi na mbili katika bonde la Chumvi. 3 Ee Mungu, umetutupilia na kutuponda, umewaka hasira. Tafazali uturudishie nguvu. 4 Umeitetemesha inchi na kuipasua; uzibe nyufa zake kwa maana imetikisika. 5 Umewaletea watu wako mateso; umetukunywesha divai tuyumbeyumbe. 6 Uwaarifu kwa vitambulisho wale wanaokuheshimu, wapate kuuepuka mushale. 7 Uwaponyeshe hao watu unaowapenda! Utuokoe kwa mukono wako! Utusikilize! 8 Mungu amesema kutoka pahali pake patakatifu: “Sasa kwa shangwe nitaigawanya inchi ya Sekemu; Bonde la Sukoti nitalipima sehemu sehemu. 9 Gileadi ni yangu, na Manase ni yangu; Efuraimu ni kofia yangu ya chuma, na Yuda ni fimbo yangu ya kifalme. 10 Moabu ni kama bakuli langu la kunawia. Nitatupia Edomu kiatu changu kwa kuirizi. Nitapiga kelele la ushindi juu ya Filistia.” 11 Ni nani atakayenipeleka kwenye muji unaozungukwa na kuta? Ni nani atakayeniongoza mpaka Edomu? 12 Si wewe Mungu ambaye umetutupilia? Lakini hauendi tena na jeshi letu. 13 Utusaidie kwa kuwashinda waadui zetu, maana musaada wa mwanadamu haufai kitu. 14 Mungu akikuwa upande wetu, tutashinda. Yeye atawaponda waadui zetu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo