Zaburi 42 - BIBLIA Maandiko Matakatifu Kwa Watu Wote 2002SEHEMU YA PILI (Zaburi 42–72 ) Maombi ya mukimbizi 1 Kwa mukubwa wa waimbaji. Mashairi ya Wakora. 2 Kama pongo anavyotamani maji ya kijito, ndivyo ninavyokutamani, ee Mungu wangu! 3 Ninasikia kiu ya Mungu, kiu ya Mungu Mwenye Uzima. Nitafika kwake wakati gani na kuuona uso wake? 4 Machozi ni chakula changu muchana na usiku; ninaambiwa kila siku: “Mungu wako yuko wapi?” 5 Katika huzuni yangu, ninakumbuka jinsi nilivyokwenda na kundi la watu na kuwaongoza kwenda katika nyumba ya Mungu wakipiga vigelegele vya shukrani, kundi la watu likifanya sherehe! 6 Mbona ninaugua hivyo katika moyo? Kwa nini ninahangaika hivyo ndani yangu? Nitamutumainia Mungu, maana nitamusifu tena yeye anayekuwa musaada wangu na Mungu wangu. 7 Roho yangu imeregea kabisa, kwa hiyo ninakukumbuka wewe, ee Mungu, kutoka katika eneo la Yordani, kutoka mulima Hermoni na Mizari. 8 Mafuriko juu ya mafuriko yananguruma, mawimbi na zoruba yako vinanifunika. 9 Yawe atanijalia wema wake muchana; nami nitamwimbia wimbo wa sifa usiku, nitamwomba Mungu anayenipa uzima. 10 Ninamwambia Mungu, yeye kikingio changu: “Kwa nini umenisahau? Kwa nini niende huko na huko nikiomboleza kwa kuteswa na adui yangu?” 11 Nimepondekana kwa ajili ya matukano yao, wanaponiuliza kila siku: “Mungu wako, yupo wapi?” 12 Mbona ninaugua hivyo katika moyo? Kwa nini ninahangaika hivyo ndani yangu? Nitamutumainia Mungu, maana nitamusifu tena Mungu, anayekuwa musaada wangu na Mungu wangu. |
Bible in Swahili Congo © Bible Society of the Democratic Republic of Congo (DRC), 2002.
Bible Society of the Democratic Republic of Congo